Malisho kwa Ajili ya Wenye Mfano wa Kondoo Katika Eneo la Navajo
NENO hózhóní, katika lugha ya Wahindi wa Navajo, lamaanisha “uzuri,” na hivyo ndivyo watu wa Navajo hufafanua eneo lao. Tangu mwaka wa 1868 serikali ya Marekani imewagawia Wanavajo kilometa za mraba 62,000 za eneo lililotengwa kaskazini-mashariki mwa Arizona, karibu na zile ziitwazo pembe nne, ambako majimbo manne ya Arizona, Colorado, New Mexico, na Utah hukutana. Bonde la Monument, lililofanywa maarufu na sinema za Magharibi, sasa limehifadhiwa likiwa Navajo Tribal Park na huvutia watalii kutoka ulimwenguni pote. Bonde hilo lina nguzo zenye kustaajabisha za mawe-mchanga zenye urefu wa meta 300 ambazo zasimama kwa upweke wenye fahari juu ya nyanda za juu za jangwa. Kwa kufaa, neno la Kinavajo kwa hilo bonde humaanisha “nafasi iliyo katikati ya mawe.”
Kwa ujumla watu wa Navajo wanajulikana kwa adabu zao zenye unyenyekevu, ukaribishaji-wageni mchangamfu, na kushikamana kwa ukaribu kwa familia zilizo pana. Wakazi 170,000 wa hilo eneo lililotengwa huishi hasa katika vijiji vidogo vilivyojitenga, kwa kufuata njia za kidesturi. Baadhi yao bado hufuga kondoo na hukaa katika nyumba za magogo yaliyofunikwa kwa udongo ziitwazo hogans. Sanaa na kazi za mkono za Wanavajo zimependwa na watu wengi sana. Yaliyo ya thamani hasa ni mazulia na mablanketi yenye michoro ya kupendeza ya kijiometri au ya kimapokeo, yaliyofumwa kutokana na sufu ya kondoo. Yenye umashuhuri sawa na huo ni mapambo ya vito vya fedha vya Navajo vyenye feruzi na vifaa vingine vya asili.
Kupeleka Habari Njema Katika Eneo la Navajo
Kwa miaka zaidi ya 30, Mashahidi wa Yehova wamekuja katika eneo la Navajo si kutalii tu bali pia kuwapelekea watu wa eneo hili lililo mbali habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Wahudumu mapainia wa kawaida na wa pekee wa Mashahidi wa Yehova wameongoza katika kazi ya kuhubiri. Wengi wao wamekuja kwa kuitikia miito kutoka kwa waangalizi wasafirio na Mashahidi wa hapo ili kusaidia mahali ambapo uhitaji umekuwa mkubwa zaidi. Baadhi yao wametoka makutaniko ya karibu, huku wengine, kutia ndani washiriki wa makabila tofauti ya Wenyeji wa Marekani, wakitoka sehemu mbalimbali za Marekani.
Wanaume na wanawake hawa wenye kujidhabihu wamelinganisha utumishi wao hapa na mgawo wa umishonari. Kwa nini? Kwanza kabisa, lugha za wenyeji ni ngumu sana kujifunza kwa sababu ya mvumo wenye utata, muundo, na maneno yake. Kisha, wenyeji kwa ujumla, wameshikamana na njia zao za kimapokeo katika dini, muundo wa familia, na kutegemea ardhi ili kupata riziki. Kwa kuongezea, makao na kazi ni haba kwa wasio Wahindi, ikifanya iwe vigumu kwa wale ambao wamehamia hapa kukaa. Hatimaye, historia ndefu juu ya kutendwa vibaya kwa hao watu mikononi mwa mtu mweupe, kwa kueleweka, imetia ndani yao kadiri fulani ya kutokuwa na itibari na wasio Wahindi.a
Hapo kwanza, Mashahidi walipoenda nyumba hadi nyumba wakiwa wamevalia kirasmi na wamevalia tai, walidhaniwa isivyo kweli kuwa Wamormon, na wengi walikuwa hawafungui mlango. Walipobadili mavazi kuwa ya kawaida zaidi, walikaribishwa, mara nyingi kwa muda wa saa moja au zaidi. Sasa watu wanawatambua Mashahidi wa Yehova, hata ingawa mavazi rasmi yanatumiwa mara nyingine tena katika huduma.
Kupata tu kuwafikia watu wanaoishi kwenye eneo lililotengwa la Navajo ni jambo gumu sana. Kuendesha gari kilometa nyingi kupitia njia ambazo huenda zikawa zenye mawe, mchanga, na matope ni jambo la kawaida. Kiasili, hilo huongezea uchakavu wa magari na kuchosha abiria. Huenda magari yakakwama, lakini wapita-njia kwa kawaida huwa tayari kusaidia. Nyakati nyingine kuwatembelea wenye kupendezwa, kwenda funzo la Biblia nyumbani, au kupeleka mtu kwenye mkutano wa Kikristo hutaka safari ya kwenda na kurudi ya saa kadhaa. Lakini Mashahidi hujitumikisha kwa kupenda, hivyo wakionyesha kupenda kwao wenyeji.—Linganisha 1 Wathesalonike 2:8.
Wanavajo hufurahia kuwa na mazungumzo ya Biblia. Kwa kawaida wao hukusanya pamoja familia nzima—watoto, wazazi, na wazakuu—ili kusikia juu ya tumaini la makao ya paradiso ya wakati ujao kwa wanadamu. Alipoulizwa jinsi ambavyo alifikiri Paradiso itakuwa, mwanamume mmoja Mnavajo alijibu, “Kijani kibichi, na kondoo wengi,” akidhihirisha kupenda kwao bara na makundi yao ya kondoo. Wao pia huthamini fasihi za Biblia, nyakati nyingine wakionyesha hivyo, kwa kutoa upaji wa shanga, mche wa sabuni, maziwa ya kopo, na vitu vya aina hiyo katika kutegemeza huduma ya Ufalme. Painia mmoja wa pekee alipata maandikisho 200 ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika muda wa mwaka mmoja, kutia ndani mawili kutoka kwa mwanamume aliyekuwa amepanda farasi.
Kuanzisha “Kambi za Kondoo”
Kiangazi kijapo, huo ndio wakati wa mchungaji Mnavajo kupeleka kundi lake kwenye kambi ya kondoo. Makao hayo ya kiangazi kwa ajili ya kondoo, yaliyochaguliwa kwa sababu yako karibu na malisho ya kijani kibichi na chanzo kizuri cha maji, husaidia kundi la kondoo kusitawi. Katika maana ya kitamathali, Jumba la Ufalme laweza kufananishwa na kambi kama hiyo—malisho ya kiroho na chanzo cha maji ya kweli. Watu wanaokuja wanaweza kupata lishe la kiroho ambalo huwafanya wawe wenye nguvu na wenye afya kiroho.
Kwa muda fulani, mikutano ilifanywa katika darasa la shule katika Kayenta, Arizona. Kisha katika Agosti 1992, kwa msaada wa mamia ya Mashahidi wenye kujitolea kutoka majimbo kadhaa, Jumba la Ufalme jipya lilijengwa katika Kayenta. Jumba la Ufalme hilo na mengine kadhaa katika hilo eneo huwaonyesha watu wa hapo kwamba Mashahidi wa Yehova wako katika eneo lao kwa kudumu. Majumba ya Ufalme mengine yanayotumikia eneo hili kubwa yatia ndani yale yaliyo Jiji la Tuba na Chinle, yote mawili yakiwa katika eneo lililotengwa, moja likiwa katika Keams Canyon kwenye ardhi ya kabila la Hopi ndani ya eneo lililotengwa la Navajo, na mengine kadhaa katika miji inayopakana na hili eneo lililotengwa. Ni nini limekuwa tokeo?
Itikio Lenye Kutokeza Sana kwa Ujumbe wa Ufalme
Katika Kayenta watu wapatao 12 wa hapo wamebatizwa tangu Jumba la Ufalme lijengwe, kuonyesha baraka za Yehova kwa mahali hapo pa ibada ya kweli. Hilo jumba hutoa uthibitisho kwamba Mashahidi wa Yehova wataendelea kuwapo na hujenga uhakika katika habari njema ya Ufalme wahubiriyo. Hivi majuzi hotuba ya Biblia ya watu wote ya kwanza katika lugha ya Kinavajo ilitolewa huko. Washiriki 40 wa kutaniko walifurahia kukaribisha watu 245 kusikiliza hotuba juu ya madaraka ya kuwa mzazi. Ikiwa na mioyo yenye uthamini, familia moja ya watu wanane ilisafiri kwa muda wa saa tatu mwendo mmoja ili kusikiliza hotuba hiyo—ziara yao ya kwanza kabisa kwenye Jumba la Ufalme.
Chombo kingine chenye mafaa ambacho Yehova ameandaa ni broshua Furahia Milele Maisha Duniani! katika lugha ya Kinavajo. Kutafsiri hiyo broshua katika lugha ya Kinavajo, lugha iliyo tata sana, kulitokeza ugumu mkubwa. Kwa ujumla watafsiri walitumia muda wa saa zaidi ya 1,000 ili wahakikishe kwamba hiyo broshua yawakilisha ujumbe wa Ufalme ifaavyo. Tangu itolewe mwisho-mwisho wa 1995, Mashahidi wa hapo wameangusha nakala maelfu kadhaa yake, ikitokeza mafunzo ya Biblia mengi pamoja na wenye kutafuta kweli.
Kadiri wahubiri wa Ufalme wajifunzavyo lugha ya Kinavajo, ndivyo inavyozidi kutumika katika huduma. Makutaniko katika hilo eneo yameanza kutumia lugha ya Kinavajo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na kuwa na madarasa ya lugha ya Kinavajo ili kuwazoeza wahubiri. Kwa kuongezea, programu kwenye makusanyiko ya hapo inatafsiriwa katika lugha ya Kinavajo. Jitihada hizo zote kwa hakika zitaongoza kwenye itikio kubwa hata zaidi katika hilo eneo lililotengwa.
Zisizo za kupuuzwa kati ya matunda ya Ufalme katika eneo hilo la Wahindi lililotengwa ni sifa njema za kiroho zionyeshwazo na ndugu zetu wa Navajo. Kwa muda wa miaka saba, Jimmy na Sandra waliwapeleka watoto wao watano umbali wa kilometa 120 mwendo mmoja ili wahudhurie mikutano ya kila juma. Hiyo familia ina kumbukumbu wazipendazo za kuimba nyimbo za Ufalme na kujifunza Biblia pamoja wakati wa safari zao ndefu. Upendo na bidii ya wazazi kwa ajili ya kweli ilichochea watoto wafuate kielelezo chao katika kuwa wasifaji wa Yehova waliojiweka wakfu. Wanne kati yao sasa hutumikia wakiwa mapainia wa kawaida, na Jimmy ni mzee wa kutaniko. Kwa kuongezea shangwe ya familia hiyo, majuzi dadake Jimmy aitwaye Elsie alipata kuwa ndiye mtu wa kwanza aongeaye lugha ya Kinavajo pekee kubatizwa.
Wachungaji wa hapo na makundi yao ya kondoo huongezea kwa kiasi fulani hali tulivu ya uchungaji zile nguzo za mawe zinazorembesha eneo hilo la Navajo lililotengwa. Nabii Isaya alitabiri zamani sana hivi juu ya Yehova: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake, nao wanyonyeshao atawaongoza polepole.” (Isaya 40:11) Kupitia Mchungaji wake Mwema, Yesu Kristo, Yehova anawakusanya katika malisho ya kiroho wale wote walio katika eneo lililotengwa la Navajo ambao hutamani kusikia habari njema za Ufalme na kuwa na fursa ya kupata baraka zake zinazodumu milele.
[Maelezo ya Chini]
a Ona matoleo ya Amkeni! ya Mei 8, 1948; Februari 22, 1952; Juni 22, 1954 (ya Kiingereza); na Septemba 8, 1996.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mwanamke mchungaji wa Navajo asikia habari njema