Kulea Watoto Wenye Maadili—Je, Kwawezekana Bado?
“SASA twaishi katika jamii iliyo tata sana, utamaduni ulio tofauti-tofauti, usio na mfumo wa adili ulio sawa,” asema Robert Glossop wa Taasisi ya Vanier kwa Ajili ya Familia katika Ottawa, Kanada. Kukiwa na tokeo gani? Ripoti fulani katika gazeti la habari la The Toronto Star yasema hivi: “Mimba za matineja, ujeuri wa vijana na kujiua kwa matineja yote yanaongezeka.”
Hilo tatizo laenea ng’ambo ya Amerika Kaskazini. Mkurugenzi wa Kitovu cha Maendeleo ya Kibinadamu kwenye Chuo Kikuu cha Brown huko Kisiwa cha Rhode, Marekani, Bill Damon, amechunguza matatizo hayo Uingereza na katika mataifa mengine ya Ulaya, na vilevile Australia, Israeli, na Japani. Yeye ataja kulegea kwa makanisa, shule, na mashirika mengine katika kuandaa mwelekezo kwa vijana. Utamaduni wetu, yeye aamini, “haufahamu yale ambayo watoto huhitaji ili kufanyiza tabia na uhodari.” Akitaja wataalamu wa malezi ya watoto ambao hufundisha kwamba “nidhamu ni hatari kwa afya na hali-njema ya watoto,” Damon asisitiza kwamba fundisho hilo ni “mbinu ya kulea watoto wakaidi, wasiotii.”
Vijana wa leo wanahitaji nini? Wahitaji daima kuzoezwa kwa upendo ambako husahihisha akili na moyo. Vijana tofauti huhitaji aina tofauti za nidhamu. Mara nyingi nidhamu yaweza kuwasilishwa kwa kusababu, ichochewapo na upendo. Hiyo ndiyo sababu tunaambiwa kwenye Mithali 8:33 “[tusikilize] mafundisho [“nidhamu,” NW].” Ingawa hivyo, vijana fulani “[hawaonywi] kwa maneno.” Kwao, adhabu ifaayo kwa sababu ya kutotii, ikitolewa kwa kiwango kifaacho, huenda ikahitajiwa. (Mithali 17:10; 23:13, 14; 29:19) Kwa kutoa pendekezo hilo, Biblia haikubali kuchapa viboko kwa hasira, au kupiga vikali, ambako huenda kukachubua au kumjeruhi mtoto. (Mithali 16:32) Badala ya hivyo, mtoto apaswa aelewe ni kwa nini anasahihishwa na apaswa ahisi kwamba ni kwa sababu mzazi yuko upande wake na anapendezwa kikweli na hali-njema yake.—Linganisha Waebrania 12:6, 11.
Shauri hilo la Biblia lenye kutumika na lililo timamu linakaziwa katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia.