Habari Njema ya Paradiso Tahiti
TAHITI! Hilo jina laonekana kuwasilisha uvutio fulani usio wa kawaida. Lilifanywa maarufu na wasanii na waandishi kama vile Paul Gauguin, Robert Louis Stevenson, na Herman Melville, ambao michoro na maandishi yao juu ya uzuri na utulivu wa kitropiki wa Visiwa vya Bahari ya Kusini, yaliwapendeza watu wengi.
Tahiti ndicho kisiwa kikubwa zaidi kati ya visiwa zaidi ya 120 katika Polynesia ya Ufaransa, iliyo Pasifiki ya Kusini. Ingawa kisiwa hiki cha Bahari ya Kusini chakaribia kufanana na paradiso katika akili za watu wengi, watu kule Tahiti bado wahitaji kusikia juu ya paradiso nyingine ijayo karibuni. (Luka 23:43) Mashahidi wa Yehova, wanaojumlika kuwa 1,918 Tahiti leo, ni wenye shughuli nyingi wakiwaambia watu 220,000 juu ya habari njema kwamba Ufalme wa Mungu karibuni utaleta hali halisi za kiparadiso si Tahiti tu bali pia duniani kote.—Mathayo 24:14; Ufunuo 21:3, 4.
Kwa miaka mingi kazi ya kuhubiri Tahiti ilielekezwa na ofisi ya tawi ya Watch Tower Society iliyo Fiji, umbali upatao kilometa 3,500. Umbali mkubwa uliohusika ulifanya mambo kuwa magumu, na maendeleo yakawa ya polepole. Hivyo, Aprili 1, 1975, ofisi ya tawi ilianzishwa Tahiti, na jambo hili likatia alama wakati wa badiliko la maana katika utendaji wa Wakristo wa kweli katika eneo hili. Ni nini kilichoongoza kwenye badiliko hilo, na kazi ya kuhubiri ilianzishwaje Tahiti?
Mwanzo Mdogo
Habari njema ya Ufalme ilisikiwa Tahiti kwa mara ya kwanza miaka ya 1930 na wengi wa wakazi wa hivyo visiwa, wanaostahi sana Biblia, waliitikia kwa upendezi mkubwa. Hata hivyo, kwa sababu ya marufuku ya serikali na vizuizi vingine, bado hakukuwa na Mashahidi kisiwani humo kufikia mwisho-mwisho wa miaka ya 1950. Wakati huo, Agnès Schenck, mzaliwa wa Tahiti aliyekuwa akiishi Marekani, aliamua kurudi Tahiti pamoja na mume na mwana wake. Yeye aeleza jinsi mambo yote yalivyotukia.
“Kwenye mkusanyiko wa wilaya Los Angeles mwaka wa 1957, Ndugu Knorr [aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo] alifafanua kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme Tahiti. Nilikuwa nimebatizwa kwa muda wa mwaka mmoja wakati huo, na nilisema kwa mkazo, ‘Hivyo acheni twende Tahiti!’ Familia mbili, akina Neill na akina Carano, marafiki wetu wema, walitukia kunisikia. Walituambia kwamba wangependa kwenda nasi, lakini hatukuwa na fedha nyingi. Mume wangu alikuwa amekuwa mgonjwa kwa muda mrefu, na mwanangu alikuwa mchanga sana. Hivyo ilikuwa vigumu kwetu kuondoka. Marafiki kutoka makutaniko jirani walipata kusikia juu ya mradi wetu, wakatupelekea fedha na vitu vya nyumbani. Kisha Mei 1958 tulisafiri kwa meli kwenda Tahiti tukiwa na shiti 36 miongoni mwa vitu vingine tulivyokuwa navyo!
“Tulipofika Tahiti, nilijihisi mgeni kabisa kwa sababu nilikuwa nimeondoka kisiwani humo kwa muda wa miaka 20. Tulianza kuhubiri, lakini tulilazimika kuwa waangalifu kwa sababu kazi yetu ya Kikristo ilikuwa chini ya marufuku. Tulilazimika kuficha magazeti, tukatumia Biblia pekee. Mwanzoni tulihubiri tu watu waliokuwa tayari wameandikisha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
“Clyde Neill na David Carano, pamoja na familia zao, walijiunga nasi baada ya mkusanyiko wa kimataifa huko New York City mwaka wa 1958. Tulihubiri pamoja na kualika watu waje kusikiliza hotuba zilizotolewa nyumbani mwa akina ndugu. Hatua kwa hatua mambo yalipangwa, tukaanza kikundi cha funzo la Biblia kikiwa na watu 15. Baada ya miezi mitatu akina Neill na akina Carano walilazimika kuondoka kwa sababu muda wa kutumika kwa viza zao za kutalii uliisha. Hivyo akina ndugu wakaamua kwamba kabla ya kuondoka kwao, wangebatiza wote wale wenye kupendezwa waliokuwa na sifa za kustahili. Nilikuwa na pendeleo la kuwa mtafsiri wa hotuba ya kwanza ya ubatizo. Wakati huo wenyeji wanane wa visiwa walifananisha wakfu wao kwa Yehova kupitia ubatizo. Kisha akina Neill na akina Carano wakarudi Marekani.
“Kazi ya kuhubiri iliendelea. Tulijipanga katika vikundi vidogo na kutolea watu ushahidi jioni. Mara nyingi mazungumzo na wenye kupendezwa yaliendelea hadi usiku wa manane. Mara kwa mara hata wahudumu wa Kiprotestanti walijiunga na mazungumzo. Kufikia mwaka wa 1959 kutaniko la kwanza lilifanyizwa. Kisha, mwaka 1960 serikali ikatambua rasmi ushirika wa Mashahidi wa Yehova, jambo lililotupendeza sana. Miaka hiyo ya mapema ilijawa na shangwe, na mambo makuu ya kiroho. Yehova kwa kweli alibariki uamuzi wetu wa kuhamia mahali uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi.” Sasa Dada Schenck ana umri wa miaka 87, na bado anamtumikia Yehova kwa uaminifu kutanikoni mwake.
Kazi Ilisonga Mbele
Mwaka wa 1969 Mashahidi wawili kutoka Ufaransa, Jacques na Paulette Inaudi, walipewa mgawo wa kwenda Tahiti wakiwa mapainia wa pekee. Jacques akumbuka: “Tulipowasili Tahiti, kulikuwa na wahubiri 124 tu, kutaniko moja Papeete, na mapainia wa pekee wawili Vairao, kwenye rasi.” Hiyo rasi imeunganishwa na Tahiti kwa shingo ya nchi. “Amani Duniani” Kusanyiko la Kimataifa lilikuwa lifanywe karibuni. “Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kupanga mkusanyiko,” Jacques aendelea. “Tulilazimika kupanga programu ya Kiingereza kwa ajili ya wageni wa kimataifa, kuanzisha kikundi cha waimbaji wa nyimbo za Ufalme, na kufanya mazoezi ya drama mbili. Kazi hiyo yote ilitimizwa kukiwa na wahubiri 126 tu. Nina hakika kwamba Yehova alifanya kazi iliyo kubwa zaidi.” Hudhurio la watu 488 lilisisimua wakazi wa kisiwani. Kwa wengi wao hiyo ilikuwa mara ya kwanza kukutana na Mashahidi wenzao kutoka nchi nyinginezo.
Baadaye kidogo, Jacques Inaudi alipewa mgawo kuwa mwangalizi asafiriye. Yeye alipozuru visiwa mbalimbali, aliona kwamba kulikuwa na upendezi mwingi lakini wahubiri wachache wa Ufalme kuuendeleza. “Hiyo ndiyo sababu nilizitia moyo familia nyingi kuhamia visiwa hivi ili kutumikia mahali ambako uhitaji ulikuwa mkubwa,” aeleza Jacques. “Kwa hiyo, hatua kwa hatua habari njema ilienezwa hadi jamii-visiwa mbalimbali.” Ndugu Inaudi alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye kutoka 1969 hadi 1974, na leo yeye ni mzee katika mojawapo ya makutaniko Tahiti.
Miongoni mwa walioitikia kitia-moyo cha Ndugu Inaudi alikuwa Auguste Temanaha, aliyekuwa mmojawapo wa wale watu wanane waliobatizwa mwaka wa 1958. Yeye asimulia yaliyotukia. “Mwaka wa 1972 mwangalizi wa mzunguko, Jacques Inaudi, alitutia moyo kufikiria kuhama ili kutumikia Huahiné, mojawapo ya Visiwa vya Pasifiki ya Kusini. Nilikuwa mwenye kusita kwa sababu nilikuwa nimefanya tu usomaji wa Biblia kutanikoni na sikuhisi mwenye kustahili kukabidhiwa daraka kama hilo. Hata hivyo, Ndugu Inaudi akafuliza kuniambia, ‘Usiwe na wasiwasi, waweza kufaulu!’ Baada ya muda fulani tuliamua. Hivyo, mwaka wa 1973 tukauza kila kitu na tukiwa na watoto wetu wachanga watatu tulihamia Huahine.
“Tulipowasili, nilipata kwamba ilikuwa lazima nianze kila kitu—Funzo la Mnara wa Mlinzi, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na kadhalika. Haikuwa rahisi, lakini tulipata kinga na msaada wa Yehova. Nyakati kadhaa alitusaidia kupata mahali pa kuishi. Kisha, kikundi cha wapinzani kilipojaribu kuwaondoa Mashahidi kisiwani, mwanasiasa wa hapo akajitokeza kututetea. Kwa kweli, Yehova alitulinda wakati huo wote.” Sasa, kuna makutaniko mawili Huahine—kutaniko la Kifaransa lenye wahubiri 23 na la Kitahiti lenye wahubiri 55.
Mwaka wa 1969, Hélène Mapu alipewa mgawo kuwa painia wa pekee ili kuhubiri hiyo rasi. “Kulikuwa na upendezi mwingi sana rasini, na katika wakati mfupi, nikaanzisha mafunzo mengi ya Biblia,” asema Hélène. Kutaniko dogo lilifanyizwa Vairao, lakini kulikuwa na uhitaji wa wazee. Halafu, Colson Deane, aliyekuwa akiishi Papara umbali wa kilometa 35, aliweza kuandaa msaada. “Ilitubidi kujipanga vizuri ili kutumikia katika Vairao,” Ndugu Deane asimulia. “Nilikuwa nikifanya kazi Faaa, umbali wa kilometa 70 kutoka Vairao upande ule mwingine wa kisiwa. Baada ya kazi, ilinibidi kurudi nyumbani haraka, kuchukua familia yangu, na kisha kuendelea hadi Vairao. Baadaye tulilazimika kuhamia Faaa kwa sababu ya kazi yangu. Je, bado tungeweza kulitegemeza Kutaniko la Vairao? Kwa kweli tulitaka kuwasaidia akina ndugu huko, hivyo tukaamua kuendelea kulitegemeza. Siku za mikutano ya usiku ni mara chache ambapo tulifika nyumbani kabla ya usiku wa manane kwa sababu ilitupasa kufanya safari ndogo kadhaa ili kuwasafirisha nyumbani wale ambao hawakuwa na magari. Tulifanya hivyo kwa miaka mitano. Sasa ni shangwe kuu kuona makutaniko manne katika sehemu hii ya kisiwa, na tuna kumbukumbu zenye kupendeza juu za hizo.”
Tahiti Yapata Kuwa Ofisi ya Tawi
Kufikia mwaka wa 1974 idadi ya wahubiri wa Ufalme Tahiti ilikuwa imekua kufikia watu 199. Mwaka uliofuata wakati N. H. Knorr na F. W. Franz waliokuwa wakati huo msimamizi na makamu-msimamizi wa Watch Tower Society, walipotembelea Polynesia ya Ufaransa, waliona kwamba lingekuwa jambo lenye kutumika zaidi kuelekeza kazi ya kuhubiri Polynesia ya Ufaransa kutoka Tahiti, si kutoka Fiji kisiwa kilichoko umbali wa kilometa zaidi ya 3,500. Hivyo, Aprili 1, 1975, ofisi ya tawi ya Tahiti ilianzishwa, na mwangalizi wa mzunguko, Alain Jamet, akawekwa rasmi kuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi.
Miaka kadhaa iliyopita, Ndugu Jamet aliweza kusimulia baraka za kustaajabisha kutoka kwa Yehova. “Tangu mwaka wa 1975 jitihada kubwa imefanywa ili kupeleka habari njema kwenye visiwa na jamii-visiwa mbalimbali katika eneo letu, vyenye ukubwa ulio sawa na Ulaya Magharibi. Matokeo yamekuwa yenye kufurahisha. Kufikia mwaka wa 1983 idadi ya wahubiri ilikuwa imekua hadi watu 538. Mwaka huo jengo kwa ajili ya ofisi ya tawi na Makao ya Betheli lilijengwa Paea. Sasa, kuna wahubiri wapatao 1,900 waliotawanyika miongoni mwa makutaniko 30 katika Visiwa vya Pasifiki ya Kusini, kutaniko moja na kikundi kimoja kilicho peke yake katika Visiwa vya Austral, kutaniko moja na vikundi viwili vilivyo peke yake Marquesas, na vikundi kadhaa vilivyo peke yake katika Visiwa vya Tuamotu na Gambier. Majumba ya Ufalme mapya mengi yanajengwa—matatu Marquesas na saba Tahiti—ili kushughulikia idadi yenye kukua daima ya wapya ambao wanakuja mikutanoni. Katika miaka 20 iliyopita, Yehova amebariki kwa kweli jitihada zetu za kusitawisha shamba la Tahiti.”
Kuna Mengi Bado ya Kufanywa
Matazamio ya ukuzi katika Polynesia ya Ufaransa ni bora kabisa. Machi 23, 1997, watu wapatao 5,376 walikusanyika pamoja na Mashahidi wa Yehova kotekote Polynesia ya Ufaransa kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo. Ili kutimiza mahitaji ya kiroho ya watu hao wenye kupendezwa, vichapo vyetu vya Biblia vinatolewa katika lugha kadhaa za hapa. Kwa kuongezea Kitahiti, fasihi imetayarishwa katika Kipaumotu, lugha inayozungumzwa katika Jamii-Visiwa vya Tuamotu katika Visiwa vya Marquesa Kaskazini na Marquesa Kusini.
Ukuzi wenye kuendelea na mambo mazuri yaliyoonwa yamesaidia wahubiri wa Ufalme Tahiti kuthamini kwa ukamili zaidi upendo na subira ya Yehova, “ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli,” hata katika visiwa vya mbali sana vya Bahari ya Kusini. (1 Timotheo 2:4) Mashahidi wa Yehova katika Tahiti na visiwa vingine vya Polynesia ya Ufaransa ni wenye imani kamili katika ahadi hii ya Yehova: “Visiwa vitaningoja, navyo vitautumainia mkono wangu.”—Isaya 51:5.
[Ramani katika ukurasa wa 26]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Ofisi ya tawi ya Tahiti hushughulikia mahitaji ya Polynesia ya Ufaransa
AUSTRALIA
[Picha katika ukurasa wa 25]
Kuanzia kushoto kuelekea kulia: Alain Jamet, Mary-Ann Jamet, Agnès Schenck, Paulette Inaudi, na Jacques Inaudi
[Picha katika ukurasa wa 27]
Ofisi ya tawi ya Tahiti