Je, Wakumbuka?
Je, umethamini kusoma matoleo ya juzi ya Mnara wa Mlinzi? Basi, ona ikiwa waweza kujibu maswali yafuatayo:
◻ Ni nini kusudi kubwa la elimu kwa kijana Mkristo?
Kusudi kubwa la elimu lapaswa kuwa kumtayarisha kijana kuwa mhudumu mwenye matokeo wa Yehova. Na elimu ya maana zaidi ya zote ili kufikia mradi huo ni elimu ya kiroho.—8/15, ukurasa wa 21.
◻ Ni zipi sababu za kuripoti kosa zito la Mkristo mwenzetu kwa wazee?
Sababu moja ya kuripoti kosa zito ni kwamba jambo hilo huhifadhi usafi wa kutaniko. Sababu nyingine ni kwamba kufanya hivyo ni tendo la upendo wenye kanuni wa Kikristo kuelekea Mungu, kuelekea kutaniko, na kuelekea mkosaji.—8/15, ukurasa wa 28, 30.
◻ Kufuliza “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova” kwamaanisha nini? (2 Petro 3:12)
Kufanya hivyo kwamaanisha kutoiondoa akilini mwetu “siku ya Yehova.” Hatupaswi kusahau kwamba siku ambayo Yehova ataharibu mfumo huu wa mambo iko karibu. Yapaswa kuwa halisi sana kwetu hivi kwamba twaiona waziwazi, kana kwamba iko karibu sana mbele yetu. (Sefania 1:7, 14)—9/1, ukurasa wa 19.
◻ Kwa nini siku za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo zimeendelea muda mrefu kuliko vile watu wengi walivyotarajia?
Yehova huangalia mambo yawezayo kuwafaidi wanadamu wote. Yeye huhangaikia uhai wa watu. (Ezekieli 33:11) Twaweza kuwa na uhakika kwamba mwisho utakuja wakati ufaao ili kutimiza kusudi la Muumba wetu mwenye hekima yote na mwenye upendo.—9/1, ukurasa wa 22.
◻ Wale walio katika utumishi wa wakati wote waweza kudumishaje shangwe yao yajapokuwa matatizo ambayo huenda yakawakabili?
Wapaswa kufikiria baraka nyingi walizo nazo na kutambua kwamba maelfu ya wengine wanapatwa na magumu makubwa zaidi. (1 Petro 5:6-9)—9/15, ukurasa wa 24.
◻ Ni upi uliokuwa mradi wa Tyndale wa kuitafsiri Biblia?
Mradi wa Tyndale ulikuwa kufanya Maandiko yapatikane kwa mtu wa kawaida katika lugha sahihi na sahili iwezekanavyo.—9/15, ukurasa wa 27.
◻ Twaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni wateteaji wa Neno la Mungu wenye uaminifu-mshikamanifu?
Twaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Neno la Mungu kwa kulihubiri kwa bidii kwa wengine. Tukiwa walimu, twapaswa kuitumia Biblia kwa uangalifu, bila kupotoa wala kutanua kamwe yale isemayo ili yafae mawazo yetu. (2 Timotheo 2:15)—10/1, ukurasa wa 20.
◻ Roho yenye kutia sumu ya ulimwengu yaweza kudhoofishaje uaminifu-maadili wetu?
Roho ya ulimwengu yaweza kudhoofisha uaminifu-maadili wetu kwa kutufanya tusiridhike na tuliyo nayo na kuhangaikia kutanguliza mahitaji na mapendezi yetu wenyewe mbele ya yale ya Mungu. (Linganisha Mathayo 16:21-23.)—10/1, ukurasa wa 29.
◻ Kumtumikia Yehova kwa nafsi yote kwamaanisha nini?
“Nafsi” hurejezea mtu mzima, akiwa na uwezo wake wote wa kimwili na kiakili. Kumtumikia Yehova kwa nafsi yote kwamaanisha kujitoa wenyewe, tukitumia uwezo wetu wote na kuelekeza nishati zetu kikamili iwezekanavyo katika utumishi wa Mungu. (Marko 12:29, 30)—10/15, ukurasa wa 13.
◻ Ni nini ufunguo wa kuwa mtu wa kanuni ya kimungu?
Ufunguo kwa kweli ni kumjua Yehova, yampendezayo, yasiyompendeza, na makusudi yake. Kanuni hizi juu ya Mungu ziongozapo maisha zetu, huwa kwa kweli kanuni zenye uhai. (Yeremia 22:16; Waebrania 4:12)—10/15, ukurasa wa 29.
◻ Watumishi wa Yehova wana mtazamo gani wenye usawaziko kuelekea utawala wa kibinadamu?
Wao hawamo katika mambo ya kisiasa kwa kuwa watumikia wakiwa mabalozi au wajumbe wa Ufalme wa Mungu. (2 Wakorintho 5:20) Kwa upande ule mwingine, wao hujitiisha kwa kudhamiria chini ya wale walio mamlakani.—11/1, ukurasa wa 17.
◻ Twaweza kujifunza somo gani kutokana na mwendo aliofuata nabii Elisha?
Alipotolewa mwaliko wa utumishi wa pekee pamoja na Eliya, Elisha aliacha shamba lake mara moja ili amhudumie Eliya, hata ingawa baadhi ya kazi zake zingekuwa za hali ya chini. (2 Wafalme 3:11) Baadhi ya watumishi wa Mungu leo wameonyesha roho hiyohiyo ya kujidhabihu kwa kuacha riziki zao ili kuhubiri habari njema katika maeneo ya mbali.—11/1, ukurasa wa 31.
◻ Barua ya Yakobo ina shauri gani lenye manufaa?
Yatuonyesha jinsi ya kukabili majaribu, yatushauri dhidi ya kutokuwa na upendeleo, na hutuhimiza tushiriki katika kazi nyoofu. Yakobo atuhimiza tuudhibiti ulimi, tukinze uvutano wa ulimwengu, na kuendeleza amani. Maneno yake yaweza kutusaidia pia tuwe wenye subira na wenye kusali sana.—11/15, ukurasa wa 24.
◻ Kwa nini Yehova yuko “tayari kusamehe”? (Zaburi 86:5)
Yehova husamehe kwa utayari kwa sababu yeye hasahau kwamba sisi tu viumbe wa mavumbi, wenye kasoro, au wenye udhaifu mbalimbali, zisababishwazo na kutokamilika. (Zaburi 103:12-14)—12/1, ukurasa wa 10, 11.
◻ Kwa nini tuwe tayari kuwasamehe wengine?
Tukikataa kusamehe wengine wakati ambapo kuna msingi wa rehema, jambo hilo laweza kuathiri vibaya uhusiano wetu na Mungu. (Mathayo 6:14, 15)—12/1, ukurasa wa 17.