Kuna Wakati Ujao Gani kwa Dunia Yetu?
“Hakuna karne nyingine yoyote iliyorekodiwa ambayo yaweza kuwa sawa na karne ya 20 katika jeuri ya raia yenye ukatili, katika idadi ya mapambano ambayo yamefanywa, watu wengi ambao wamefanywa kuwa wakimbizi, mamilioni ya watu ambao wameuawa katika vita, na matumizi ya juu sana kwa ajili ya ‘ulinzi,’” chataarifu kitabu World Military and Social Expenditures 1996. Je, hali hiyo itabadilika wakati wowote?
Mtume Petro aliwakumbusha Wakristo juu ya ahadi iliyofanywa na Mungu karne kadhaa mapema: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi [ya Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Awali maneno hayo yalikuwa sehemu ya unabii wa Isaya. (Isaya 65:17; 66:22) Israeli la kale lilipata kuona utimizo wa kwanza wa unabii huo wakati ambapo hilo taifa lilirudishwa kwenye bara lake lililoahidiwa baada ya kuchukuliwa mateka huko Babiloni kwa muda wa miaka 70. Kwa kurudia kutaja hiyo ahadi ya “mbingu mpya na dunia mpya,” Petro alionyesha kwamba, huo unabii bado ungetimizwa kwa kiwango kikubwa hata zaidi—ulimwenguni pote!
Ni mapenzi ya Mungu kuanzisha hali zenye uadilifu katika dunia yote, nazo zitatokezwa na Ufalme wake wa kimbingu, Kristo akiwa Mfalme. “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Amani kamili kama hiyo na usalama duniani ndiyo mambo ambayo Yesu alifunza wafuasi wake watarajie na kusali kuyapata, katika ile iitwayo kwa kawaida Baba Yetu, au Sala ya Bwana, akisema hivi: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.
Je, ungefurahia kuishi katika ulimwengu ulio mwadilifu kama vile mbingu ilivyo? Hilo ndilo tumaini ambalo Biblia humtolea kila mtu ambaye kwa moyo wote atafuta kumjua Mungu na kuishi kulingana na njia zake za uadilifu.