Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 7/1 kur. 26-29
  • Tukio Lisiloweza Kusahaulika Katika Ufaransa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tukio Lisiloweza Kusahaulika Katika Ufaransa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Yehova Hukuza
  • Mkusanyiko wa Pekee Sana
  • “Chemchemi Jangwani”
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 7/1 kur. 26-29

Tukio Lisiloweza Kusahaulika Katika Ufaransa

“HATUTAKI JIJI LA YEHOVA!” yakatangaza makaratasi yaliyobandikwa kotekote jijini. “Sote na Tuungane Dhidi ya Mradi Huu wa Yehova,” kikahimiza kikundi kimoja cha upinzani. Mamia ya makala za waandishi wa habari ziliwajulisha watu juu ya jambo hilo. Maombi yalitiwa sahihi, na trakti nyingi sana, zaidi ya nusu milioni, zilizokuwa zikitaja juu ya mradi huo zilijaa kwenye masanduku ya barua. Ni mradi gani huo uliovuruga mji wa Louviers, Ufaransa kaskazini-magharibi, ambao kwa kawaida huwa mji mtulivu? Ujenzi uliopendekezwa wa ofisi ya tawi mpya na makao ya Mashahidi wa Yehova.

Yehova Hukuza

Utendaji wa Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa ulianza nyuma huko mwishoni mwa karne ya 19. Depo ya kwanza ya fasihi ya Biblia ilifunguliwa mwaka wa 1905 huko Beauvène, kusini mwa Ufaransa, na tangu mwaka wa 1919, ofisi ndogo ilikuwa ikifanya kazi katika Paris. Ofisi ya tawi ilifunguliwa rasmi katika jiji hilo mwaka wa 1930, na mwaka uliofuata wafanyakazi wa ofisi hiyo wakaanza kukaa katika makao ya Betheli yaliyokuwa Enghien-les-Bains, kaskazini mwa Paris. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, familia ya Betheli ilihamia Paris tena, na mwaka wa 1959 ofisi ya tawi ilihamishwa hadi jengo lenye orofa tano huko Boulogne-Billancourt, kwenye viunga vya magharibi vya jiji hilo.

Kwa sababu ya kupanuka kwa kazi ya kuhubiri Ufalme, mwaka wa 1973 matbaa na idara ya upakizi zilihamishwa hadi Louviers, kilometa 100 magharibi mwa Paris, ilhali ofisi zilibaki Boulogne-Billancourt. Hata hivyo, ongezeko la idadi ya wahubiri katika Ufaransa lilifanya majengo yaliyo Louviers yasitoshe, licha ya kupanuliwa mwaka wa 1978 na mwaka wa 1985. Kwa hiyo iliamuliwa upanuzi ufanywe na familia yote ya Betheli ikae pamoja mahali pamoja. Mradi huo haukukubaliwa na watu wote, kama ilivyotajwa mwanzoni. Ujapokuwa upinzani huo, mahali pa kujenga palipatikana kilometa moja na nusu tu kutoka mahali penye hiyo matbaa. Miaka sita ya kazi ngumu ilifuata, na hatimaye, baada ya miaka 23 ya kutengana, familia nzima ya Betheli iliungana huko Louviers mwezi wa Agosti 1996.

Msongamano wa watu wenye shangwe kubwa, wapatao 1,187, kutia ndani washiriki 300 wa familia ya Betheli ya Ufaransa, na wajumbe 329 kutoka ofisi nyingine za tawi zipatazo 42, walikusanyika Jumamosi, Novemba 15, 1997, ili kusikiliza hotuba ya kuweka wakfu iliyotolewa na Ndugu Lloyd Barry, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Hata hivyo, kuweka wakfu huko kungefanyika wakati ambapo kulikuwako uhasama na kampeni ya kuchongea ya waandishi wa habari iliyoendelea kwa muda mrefu dhidi ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika Ufaransa. Basi, iliamuliwa kwamba Mashahidi wote katika Ufaransa wapaswa kushiriki katika kusherehekea ushindi huo. Kwa hiyo, Jumapili, Novemba 16, mkutano wa pekee wenye kichwa “Endeleeni Kukaa Katika Upendo wa Kristo” ulipangwa kufanywa katika Villepinte Exhibition Center (mahali pa maonyesho), kaskazini tu mwa Paris. Mashahidi wa Yehova wote katika Ufaransa pamoja na Mashahidi wasemao Kifaransa katika Ubelgiji na Uswisi walialikwa, pamoja na makutaniko katika Uingereza, Ujerumani, Luxembourg, na Uholanzi.

Mkusanyiko wa Pekee Sana

Mkusanyiko huo ulianza kutayarishwa miezi sita mapema. Kisha, majuma mawili tu kabla ya kuweka wakfu, madereva wa malori wa Ufaransa wakagoma, wakifunga njia kuu na pia ugavi wa mafuta ya gari. Je, viti na vifaa vingine vingefika kwa wakati? Je, vizuizi vya barabarani vingewazuia ndugu wasije? Watu wote walitulizwa kwa sababu katika juma moja mgomo huo ulikuwa umeisha, na barabara zote zilikuwa zimefunguliwa tena. Ijumaa jioni kabla ya mwisho-juma wa kuweka wakfu, malori 38 yalileta viti 84,000 kwenye yale majumba mawili makubwa yaliyokodishwa kwa ajili ya pindi hiyo. Ndugu na dada zaidi ya 800 walifanya kazi usiku kucha hadi saa tatu na nusu Jumamosi asubuhi wakitayarisha viti, jukwaa, mfumo wa sauti, na skrini kubwa tisa za vidio.

Milango ilifunguliwa saa 12:00 Jumapili asubuhi, nao umati wa watu ukaanza kumiminika. Treni 17 zilizokodishwa zilileta Mashahidi zaidi ya 13,000 kwenye jiji kuu hilo. Ndugu na dada wenyeji zaidi ya mia mbili walikuwapo kwenye vituo vya reli ili kuwalaki wasafiri na kuandamana nao katika vikundi-vikundi hadi mahali pa mkusanyiko. Dada mmoja alisema kwamba mpango huo wenye upendo uliwafanya “wahisi usalama na hali nzuri.”

Wengine walikuja Paris kwa ndege au kwa gari. Hata hivyo, walio wengi walikuja kwa mabasi 953, ilhali Mashahidi kutoka Paris walitumia usafiri wa umma kusafiri kwenda Exhibition Center. Wengi walikuwa wamesafiri usiku kucha au walikuwa wametoka nyumbani kwao mapema sana asubuhi, lakini msisimko wao kwa sababu ya kuhudhuria mkutano huo ulionekana. Vilio vya shangwe na kukumbatiana kwa shauku kulitambulisha kuungana tena kwa marafiki ambao hawakuwa wameonana kwa miaka kadhaa. Mavazi yenye kupendeza ya mataifa mbalimbali yalifanya umati huo wenye furaha uonekane kuwa wa kimataifa. Bila shaka, jambo fulani lisilo la kawaida lilikuwa likiendelea.

Kufikia wakati ambapo programu ilianza, saa 4:00 asubuhi, kila kiti kilikuwa kimekaliwa, na bado mamia ya watu walikuwa wakifika kila dakika. Popote ambapo mtu alitazama, aliona nyuso nyingi zenye kutabasamu. Maelfu ya watu walisimama au kukaa sakafuni. Wakionyesha roho ya kichwa cha kusanyiko, wachanga wengi walisimama kwa upendo ili wazee waketi. “Tulikuwa wenye furaha kama nini kuwapa viti vyetu ndugu na dada zetu ambao hatukuwajua, lakini ambao tuliwapenda sana!” wakaandika wenzi fulani wa ndoa. Wengi walionyesha mtazamo mzuri wa kujidhabihu: “Tulisimama wakati wote wa programu kando ya vitu tulivyosaidia kutayarisha usiku kucha Ijumaa. Lakini kuwepo tu, kulifanya tujawe na shukrani kwa Yehova.”

Ujapokuwa uchovu na kutostarehe, wajumbe walisikiliza kwa makini ripoti kutoka katika nchi nyingine na hotuba zilizotolewa na Lloyd Barry na Daniel Sydlik, ambaye pia ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Ndugu Barry alizungumza juu ya “Yehova Huongeza Nguvu,” naye alionyesha waziwazi jinsi ambavyo Yehova amewabariki watu wake kwa ongezeko licha ya majaribu mbalimbali. Hotuba ya Ndugu Sydlik ilikuwa na kichwa “Wenye Furaha Ni Watu Ambao Mungu Wao Ni Yehova!” Hotuba zote mbili zilitolewa wakati barabara kwa sababu ya upinzani ambao Mashahidi wa Yehova wanakabili sasa hivi Ufaransa. Ndugu Sydlik alionyesha kwamba furaha ya kweli haitegemei mambo ya nje bali hutegemea uhusiano wetu na Yehova na mtazamo wetu kuelekea uhai. Swali alilouliza wasikilizaji, “Je, mna furaha?” lilijibiwa kwa makofi yaliyopigwa kwa mshindo.

Dada mmoja aliyekuwa “amepoteza shangwe yake” aliandika hivi baadaye: “Sasa natambua kwamba naweza kupata furaha. Nilikuwa nikijitahidi kupata furaha kwa njia isiyofaa, na kupitia hotuba hiyo, Yehova amenionyesha jinsi ninavyohitaji kubadilika.” Ndugu mwingine alijulisha hivi: “Sasa nataka kupambana ili kuufanya moyo wa Yehova ufurahi. Sitaki kuacha kitu chochote kiondoe shangwe ambayo nimeanza kuihisi ndani, ndani sana.”

Mkutano huo ulipokaribia kwisha, kulikuwa na shauku kubwa mwenyekiti alipotangaza hudhurio: 95,888—mkusanyiko mkubwa zaidi wa Mashahidi wa Yehova uliopata kufanywa Ufaransa!

Baada ya wimbo wa kumalizia, ambao wengi waliuimba wakitokwa na machozi ya shangwe, na sala ya mwisho, ndugu hao walifunga safari ya kurudi nyumbani wakiwa na hisia tofauti-tofauti. Ile hali ya kirafiki yenye shauku ya mkusanyiko huo ilionwa na wengine. Madereva wengi walisema mambo mazuri juu ya mtazamo wa wajumbe hao. Pia walivutiwa na utaratibu uliowezesha mabasi yote 953 kuondoka Exhibition Center kwa muda wa saa mbili bila msongamano wowote wa magari! Mwenendo wa wajumbe ulithaminiwa sana pia na waajiriwa wa reli na wa usafiri wa umma. Mazungumzo mengi mazuri yalianzishwa, na ushahidi mzuri ulitolewa.

“Chemchemi Jangwani”

Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, . . . kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Bila shaka, mkutano huo wa pekee uliwatia wote moyo, ulikuwa “chemchemi jangwani” kama alivyoufafanua dada mmoja. “Tuliondoka tukiwa tumechochewa, tumetiwa moyo, tumeimarishwa, na tukiwa tumeazimia hata zaidi kuliko wakati mwingine wowote kushangilia katika utumishi wa Yehova,” wakaandika akina ndugu kutoka ofisi ya tawi ya Togo. “Waliokuwa wenye huzuni walienda nyumbani wakiwa na furaha,” akasema mwangalizi mmoja wa mzunguko. “Akina ndugu walichochewa na kutiwa nguvu,” akasema mwingine. “Hatujapata kuhisi tukiwa karibu sana na tengenezo la Yehova kama tuhisivyo sasa,” wenzi wa ndoa fulani walichochewa kuandika.

“Mguu wangu umesimama palipo sawa; katika makusanyiko nitamhimidi BWANA,” akasema mtunga-zaburi. (Zaburi 26:12) Makusanyiko kama hayo ya Kikristo huwezesha wote kupata tena msimamo hakika wa kiroho wajapokabili vizuizi. “Hata kuwe na dhiki gani,” dada mmoja akasema kwa uhakika, “pindi hizi za pekee zimekuwa na athari kubwa mioyoni mwetu nazo zitatufariji sikuzote.” Vivyo hivyo, mwangalizi asafiriye aliandika hivi: “Nyakati ngumu zizukapo, kumbukumbu ya mwonjo huo wa kimbele wa Paradiso itatusaidia kukabiliana nazo.”

“Mpeni [“mhesabieni sifa,” NW] BWANA, enyi jamaa za watu; mpeni [“mhesabieni sifa,” NW] BWANA utukufu na nguvu,” yahimiza Zaburi 96:7. Bila shaka, kuwekwa wakfu kwa tawi la Ufaransa ni ushindi mkubwa kwa Yehova. Yeye tu ndiye angeweza kuufanya mradi huo ufanikiwe ujapokabili upinzani huo wa kuazimia na ulioenea sana. Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa wameazimia zaidi ya wakati mwingine wowote ‘kukaa katika upendo wa Kristo’ na ‘kuacha nuru yao ing’ae.’ (Yohana 15:9; Mathayo 5:16) Wote waliohudhuria programu ya kuweka wakfu hawawezi kujizuia kuhisi kama mtunga-zaburi: “Neno hili limetoka kwa BWANA, nalo ni ajabu machoni petu.”—Zaburi 118:23.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Lloyd Barry

[Picha katika ukurasa wa 26]

Daniel Sydlik

[Picha katika ukurasa wa 26]

Watu 95,888 walihudhuria programu ya pekee kwenye Villepinte Exhibition Center

[Picha katika ukurasa wa 28]

Maelfu ya waliohudhuria ama walisimama ama waliketi sakafuni ili kusikiliza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki