Je, Maria Alikufa Kutokana na Sababu za Kiasili?
KULINGANA na gazeti la habari la Vatican liitwalo L’Osservatore Romano, fundisho la Kikatoliki la Kupazwa Mbinguni lasema hivi: “Bikira Mkingiwa Dhambi ya Asili, aliyekingwa na kila waa la hatia ya dhambi ya asili, alichukuliwa mwili na nafsi hadi kwenye utukufu wa mbingu maisha yake ya kidunia yalipofikia mwisho.” Fundisho hilo limefanya wanatheolojia fulani Wakatoliki wadai kwamba, Maria “hakufa, bali alichukuliwa mara moja kutoka duniani kwenda kuishi katika utukufu wa kimbingu,” lasema gazeti hilo.a
Hivi majuzi, Papa John Paul wa Pili alifafanua fundisho hilo kwa njia tofauti. Kwenye Baraza Kuu lililokuwa Vatican katika Juni 25, 1997, yeye alisema hivi: “Agano Jipya halisemi lolote juu ya hali za kifo cha Maria. Ukimya huo hufanya mtu afikiri kwamba kifo cha Maria kilitokea kiasili, bila jambo lolote hasa listahililo kutajwa. . . . Maoni ya kutaka kumtenga na kifo kilichotokana na sababu za kiasili yaonekana kuwa bila msingi.”
Taarifa ya Papa John Paul hufichua kasoro kubwa katika fundisho la Kuchukuliwa Mimba Bila Dhambi ya Asili. Ikiwa mama ya Yesu ‘alikingwa asipatwe na doa lolote la dhambi ya asili,’ Maria angeweza kufaje kutokana na “sababu za kiasili,” zitokanazo na dhambi iliyopitishwa kutoka kwa Adamu mwenye dhambi? (Waroma 5:12) Jambo hilo la kitheolojia lenye kutatanisha, husababishwa na maoni yaliyopotoka ya Kanisa Katoliki juu ya mama ya Yesu. Si ajabu kwamba mgawanyiko na mvurugo umetokea ndani ya Kanisa Katoliki juu ya jambo hilo.
Ingawa Biblia humfafanua Maria kuwa mtu mnyenyekevu, mwaminifu, na mwenye kumcha Mungu, haisemi sifa hizo zatokana na “kuchukuliwa mimba bila dhambi ya asili.” (Luka 1:38; Matendo 1:13, 14) Biblia yasema tu hivi: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Naam, Maria alirithi dhambi na hali ya kutokamilika sawa na jamii yote ya kibinadamu, na hakuna uthibitisho wa kwamba yeye hakufa kutokana na sababu za kiasili.—Linganisha 1 Yohana 1:8-10.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala yenye kichwa “Kuchukuliwa Mbinguni—Je, Ni Fundisho Lililofunuliwa na Mungu?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 1994, ukurasa wa 26-29.