Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti
Kujipatanisha kwa Unyenyekevu na Njia ya Yehova
“MTAFUTENI BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia.” Mwaliko huo uliotangazwa karne 26 zilizopita, na nabii Mwebrania, Sefania, ungali unatolewa kwa watu duniani kote leo. (Sefania 2:3) Kumtafuta Yehova kwamaanisha nini? Kufanya hivyo huanza kwa kutwaa ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli na aliye hai, Yehova.—Yeremia 10:10; Yohana 17:3.
Hata hivyo, kutwaa ujuzi tu kwenyewe hakuandai msimamo wa kukubaliwa na Mungu. Ili kupata upendeleo wa Mungu, ni lazima mtu atumie ujuzi huo. Jinsi gani? Kwa kufanya kwa unyenyekevu, fikira na mwenendo wake zipatane na viwango vya Mungu, kama inavyotolewa kielezi na jambo hili lililoonwa kutoka Suriname.—Waefeso 4:22-24.
Eddy, mwalimu wa shule mwenye miaka 30 na kitu, alitamani sana kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali kama haya: ‘Dini hutimiza fungu gani katika jamii leo?’ na ‘Je, Biblia ikiwa kitabu cha kale, inapatana na sayansi ya kisasa?’ Mashahidi wa Yehova walipozuru na kumjibu maswali hayo kwa kutumia Biblia, Eddy alisikiliza kwa makini. Hata aliandika mambo fulani ili kuchunguza maelezo ya Mashahidi hao akinuia kuhakikisha.
Hapo awali, Eddy alikuwa ameshirikiana na dini iliyomfundisha kwamba Mungu alifanya sokwe wageuke na kuwa watu hatimaye. Kwa hiyo, Mashahidi walipomtolea kichapo Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? alikikubali bila kusita. Maelezo ya kitabu hicho yenye kueleweka wazi juu ya masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji yalimvutia. Kupitia kujifunza kwake Biblia, alipata kusadikishwa kwamba alikuwa ameipata kweli!
Lakini sasa alikabili jaribu. Eddy aliishi katika nyumba ambamo wizi na ukosefu wa kufuatia haki ulikuwa ndio mtindo. Hivyo alipaswa kuchagua: ama afuate namna ya maisha yenye ufisadi ya wanachumba wenzake au kukatalia mbali mwenendo huo ili afuate mtindo-maisha unaomtukuza Mungu. Kwa hekima, Eddy aliamua kufuata mtindo-maisha unaomtukuza Mungu. Alijitenga na mashirika yote mabaya na kuhama kutoka nyumba hiyo.—1 Wakorintho 15:33, 34.
Eddy alifanya maendeleo ya haraka baada ya kuanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Alirekebisha mavazi na mapambo yake na kuanza kueleza rafiki zake na jamaa zake juu ya yale aliyokuwa akijifunza. Baadaye, shangwe yake iliongezeka alipoidhinishwa kushiriki katika kuhubiri “habari njema” hadharani. (Mathayo 24:14; Matendo 20:20) Siku iliyotarajiwa sana ilifika Desemba 1996 alipoonyesha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.
Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu wenye mioyo ya haki huitikia mwaliko wa ‘kumtafuta BWANA.’ Kwa kufanya hivyo, wao huona ukweli wa andiko la Mithali 22:4, lisemalo hivi: “Thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha BWANA ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.” Naam, kwa kujipatanisha na njia za Yehova, wapenda-kweli hufurahia baraka kama hizo leo, na kutazamia kwa uhakika baraka za milele papa hapa duniani.—Zaburi 37:29.
[Ramani katika ukurasa wa 18]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa.)
Bahari ya Karibea
GUYANA
SURINAME
GUIANA ya UFARANSA
BRAZILI
[Hisani]
Tufe: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.