Kuishi na Kuhubiri Karibu na Volkeno
“NI JAMBO lenye kuogofya sana. Laweza kuwa tu kama mwisho wa ulimwengu ambao Biblia husema juu yake. Lazima tuendelee kuwa chonjo na kuwa na msimamo mzuri mbele za Yehova Mungu kila wakati.” Hayo ni maneno ya Víctor, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akisimulia jambo aliloona la kuishi karibu sana na volkeno ya Popocatépetl, inayojulikana sana kuwa Popo, katika Mexico.
Volkeno hii yenye kunguruma imekuwa katika habari za kimataifa tangu 1994.a Wenye mamlaka walikata kauli kwamba kila kitu kilichoko kilometa 30 kuzunguka eneo la kreta kiko katika eneo lenye hatari kubwa sana. Upande wa kusini wa volkeno hasa ni wenye hatari kwa sababu kreta imeinama kuelekea upande huo na kuna mabonde kadhaa yenye kina kirefu ambayo kupitia hayo lava na matope yaweza kutapanywa nje ya kreta.
Kiasili, wengi hujiuliza kile ambacho kingeweza kuipata Mexico City endapo mlipuko mkubwa wa volkeno hiyo ungetokea. Je, jiji hilo limo hatarini? Kisha pia kuna wale watu wote walio katika jimbo la Morelos kuelekea kusini mwa volkeno hiyo. Je, wote walio katika eneo hilo pia wamo hatarini? Na kuishi karibu na volkeno hiyo kukoje, bila kujua ni nini kiwezacho kutukia siku yoyote?
Tisho la Volkeno
Kitovu cha Mexico City kiko karibu kilometa 70 kaskazini-magharibi mwa Popocatépetl, ijapokuwa baadhi ya vitongoji viko umbali wa kilometa 40 tu. Kihalisi, eneo lote la mji mkuu, lenye idadi ya watu milioni 20, liko nje ya eneo la hatari. Hata hivyo, ikitegemea unakoelekea upepo, eneo hili laweza kuathiriwa, jivu jingi mno likitolewa na volkeno hiyo.
Matokeo ya jivu la volkeno kwa ukawaida ni mabaya zaidi upande wa mashariki wa volkeno hiyo. Eneo hili latia ndani jiji la Puebla na idadi ya majiji na miji midogo-midogo, iliyo na watu wapatao 200,000 wanaoishi katika eneo lenye hatari kubwa sana. Jumapili, Mei 11, 1997, volkeno hiyo ilirusha tani nyingi za jivu hewani na kulieneza kote katika eneo hili, likifika hadi kwenye jimbo la Veracruz, zaidi ya kilometa 300 upande wa mashariki. Katika eneo lililo kusini mwa volkeno hiyo, katika jimbo la Morelos, kuna majiji na miji kadhaa iliyo na idadi ya watu wapatao 40,000 ambao pia wangeweza kuwa katika hatari kubwa.
Katikati ya haya yote, Mashahidi wa Yehova huishi na kuhubiri. Katika Mexico City, wako zaidi ya 90,000 katika makutaniko yapatayo 1,700. Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society iko nje ya Mexico City kuelekea kaskazini-mashariki, karibu kilometa 100 kutoka kwenye volkeno hiyo. Kuna wajitoleaji zaidi ya 800 wanaotumikia kwenye ofisi ya tawi, mbali na wajitoleaji wengine 500 wanaofanya kazi katika mradi mkubwa wa ujenzi. Wote hao wako nje ya eneo lenye hatari.
Katika jimbo la Morelos, kuna karibu makutaniko 50 ya Mashahidi wa Yehova kukiwa na wahubiri wa Ufalme zaidi ya 2,000. Baadhi ya hayo, yakiwa Tetela del Volcán na Hueyapan, yako umbali wa kilometa 20 tu kutoka kwenye kreta. Kwa kuongezea, kuelekea mashariki katika jimbo la Puebla, kuna makutaniko yaliyo na wahubiri wapatao 600 wanaoishi kati ya kilometa 20 hadi 30 kutoka kwenye volkeno hiyo. Bila shaka, hawa wanaweza kuwa katika hatari kubwa sana.
Mashahidi wa Yehova Hudumu Wakiwa Watendaji
Kujapokuwa tisho la daima, Mashahidi wa Yehova hawajaacha kazi yao ya kuhubiri katika eneo hili. Pia wameendeleza ratiba yao ya mikutano ya Kikristo, ambayo huwafanya wahisi kuwa na muungano na uhakika chini ya hali hizi mbaya. (Waebrania 10:24, 25) Ripoti kutoka kutaniko moja yasema: “Kumekuwa na badiliko kubwa ajabu katika mtazamo wa watu kuelekea habari njema ya Ufalme. Kwa mfano, katika kijiji kidogo, hivi majuzi watu 18 wamekubali mafunzo ya Biblia nyumbani.”
Kutaniko jingine, lililo kilometa 20 kutoka kwenye volkeno hiyo, laripoti hivi: “Ukuzi umekuwa wenye kutokeza. Kutaniko lilianzishwa katika Novemba 1996. Miezi sita iliyofuata, watu 10 walistahili kushiriki katika huduma ya shambani. Wahubiri kadhaa wanaishi kilometa 20 hivi kutoka katika kreta. Mikutano ya Kikristo inafanywa huko, nao wana hudhurio la watu 40 hivi.”
Magdalena, anayeishi San Agustín Ixtahuixtla, Puebla, kilometa 25 tu kutoka kwenye volkeno, ameendelea kuwa mwenye shughuli katika kuongoza mafunzo ya Biblia. Yeye asimulia lililotukia baada ya mlipuko mmoja mkubwa sana.
“Tulitaarifiwa kwamba twapaswa kuondoka nyumbani kwetu, tulifanya hivyo—tukiwa twanyeshewa na jivu. Licha ya hali ya dharura, niliifikiria familia ya Dorado niliyokuwa nikijifunza Biblia nayo. Ndugu kadhaa nami tulikwenda nyumbani kwa akina Dorado kuwasaidia wahamie mahali palipo salama zaidi. Katika jiji la karibu la Puebla, halmashauri ya kutoa msaada ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa tayari imeanza kutenda. Familia ya Dorado ilivutiwa sana na njia ambayo sisi sote tulitendewa huko. Mahali pa kuishi katika sehemu mbalimbali, palitayarishwa mapema na ndugu zetu Wakristo. Hatukukosa kitu chochote, hata ingawa tulikuwa mbali na nyumbani. Familia hii ilikuwa imehudhuria mikutano kadhaa kwenye Jumba la Ufalme, lakini ilishangazwa na upendo walioonyeshwa na ndugu zetu ambao hawakuwa wamekutana nao wakati wowote. Majuma kadhaa baada ya kurudi nyumbani kwetu, familia hii ilianza kuhudhuria mikutano yote kwa ukawaida. Upesi wakastahili kuwa wahubiri wa habari njema. Wawili kati yao sasa wamebatizwa. Wametumikia wakiwa wahudumu mapainia-wasaidizi kwa miezi kadhaa nao wanafanya mipango ya kuingia utumishi wa painia wa kawaida.”
Martha, msichana mwenye umri wa miaka 20 anayeishi kilometa 21 kutoka kwenye kreta, hakuruhusu kutojiweza kwake kumzuie kutumia kwa manufaa kila fursa ya kuhubiri. Alijifunza kweli miaka mitatu iliyopita wakati volkeno hiyo ilipoanza kuwa hai tena. Badala ya kutumia kiti chenye magurudumu, ambacho hakingekuwa rahisi kutumia katika eneo lenye mteremko mkali anakoishi, yeye hupanda punda ili kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Yeye hupanda punda huyo kwenda mikutanoni. Martha anamshukuru Yehova sana kwa sababu ya kuwa sehemu ya udugu wenye upendo, kwa kuwa hutegemea msaada wa akina dada kupanda na kushuka kwenye punda. Kila mwezi, yeye hutumia muda wa saa 15 katika huduma.
Katika maeneo hayo yaliyotengwa, Mashahidi wa Yehova mara nyingi hukabili msongo kutoka kwa jirani zao wajiunge nao kusherehekea sikukuu za kidini. Katika Tulcingo, kijiji kilichoko kilometa 20 hivi kutoka kwenye volkeno, mwanamume mmoja alipewa mgawo wa kuwatembelea Mashahidi ili akusanye michango ya sherehe. Kwa subira, akina ndugu walimweleza sababu ya kutoweza kushiriki katika sikukuu hizo za kidini. Mwanamume huyo alijitahidi sana kupata fedha kutoka kwa akina ndugu hivi kwamba alianza kushirikiana nao, akapata kujua baadhi ya itikadi zao. Alifurahia kupata majibu ya maswali yake katika Biblia yake mwenyewe ya Katoliki. Pamoja na mke wake na binti yake, yeye amekuwa akihudhuria mikutano kwa ukawaida kwa mwaka mmoja na ameonyesha tamaa ya kuwa mhubiri wa habari njema.
Waweza Kujitayarishaje?
Wastadi wa volkeno hufanya uchunguzi wao na kutoa ripoti rasmi kuhusu Popocatépetl itishayo, lakini kwa kweli hakuna ajuaye ni nini kitakachotukia au ni wakati gani. Kulingana na vyombo vya habari na watu wanaoishi karibu na hapo, volkeno yaweza kulipuka wakati wowote. Tisho hilo ni la kweli. Bila shaka, wenye mamlaka wanahangaika sana nao wanataka kufanya yote wawezayo kuwa tayari endapo dharura itatokea. Lakini yaeleweka kwamba lazima wawe waangalifu kuhusu kutoa onyo, kwa kuwa hawataki kuanzisha kuhama kwa watu wengi ikiwa hakuna hatari inayokaribia. Basi, mtu afanyeje?
“Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia,” yasema mithali ya Biblia. (Mithali 22:3) Kwa hiyo, jambo la hekima ni kuchukua hatua zinazohitajiwa ili kuhakikisha usalama wa mtu binafsi wakati fursa ingalipo, si ‘kuendelea mbele’ kana kwamba hakuna chochote kitakachotukia, wala kungojea mlipuko kimakusudi kabla ya kuchukua hatua kana kwamba unataka kuona litakalotukia. Hivi ndivyo Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanavyoona jambo hilo.
Hivi majuzi, wawakilishi kutoka ofisi ya tawi ya Watch Tower Society walikutana na waangalizi wasafirio katika jimbo la Puebla, ambao huwasiliana sana na makutaniko yaliyo katika eneo lenye hatari. Mipango ilifanywa ili waangalizi wasafirio na washiriki wa halmashauri ya kutoa msaada watembelee kila moja ya familia zinazoishi umbali wa kilometa 25 kutoka kwenye kreta. Familia hizo zilisaidiwa kufikiria kwa uangalifu kuhama eneo lenye hatari kabla ya mlipuko. Usafiri na mahali pa kuishi palipangwa ili kupatia nafasi watu 1,500 katika jiji la Puebla. Familia nyingine zilihama zikaishi na watu wa jamaa katika majiji mengine.
Onyo kwa Kiwango Kikubwa Zaidi
Moshi, moto, na ngurumo kutoka Popocatépetl ni dalili zilizo wazi za kwamba mlipuko uko karibu. Wale wote wanaotaka kuponyoka lazima watii maonyo yanayotolewa na wenye mamlaka na wachukue hatua inayofaa. Mashahidi wa Yehova katika eneo la karibu na volkeno hiyo huendelea kuwa waangalifu kuhakikisha usalama wao wenyewe na kusaidia wengine waone hatari na kuchukua hatua fulani kabla haijawa kuchelewa mno.
Kwa kiwango kikubwa zaidi, Mashahidi wa Yehova pia wako chonjo kuhusu matukio ya ulimwengu wakiyatazama kulingana na unabii mbalimbali wa Biblia. Vita, matetemeko ya dunia, njaa, maradhi, na uhalifu ni matukio ya pekee kama yalivyo ya volkeno. Hayo ni sehemu muhimu ya ishara ya mambo mengi ambayo Yesu Kristo alitabiri kwamba yangetia alama “umalizio wa mfumo wa mambo.” Ingawa hakuna mtu ajuaye kabisa wakati mwisho utakapokuja, hakuna shaka kwamba unakuja na kwamba uko karibu sana.—Mathayo 24:3, 7-14, 32-39.
Uhitaji wa haraka leo ni kwamba watu kila mahali wachukue kwa uzito onyo hili la Yesu: “Lakini kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe kwamba mioyo yenu isiwe kamwe yenye kulemewa na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara hiyo.” (Luka 21:34) Huu kwa wazi ndio mwendo wa hekima. Kama vile ishara za onyo za volkeno hazipaswi kuchukuliwa hivihivi, ni lazima tusipuuze kukaribia kwa Mwana wa binadamu, Yesu Kristo, aliyesihi hivi: “Kwa sababu hiyo nyinyi pia jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.”—Mathayo 24:44.
[Maelezo ya Chini]
a Gazeti la Amkeni! la Machi 8, 1997, liliripoti juu ya volkeno hiyo itishayo.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Martha (akiwa juu ya punda) pamoja na wengine wanatoa ushahidi karibu na Popocatépetl