Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 10/15 kur. 25-29
  • Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Kuanzisha Kazi
  • Programu ya Kielimu Yenye Matokeo
  • Makusanyiko ya Pekee Yaleta Shangwe
  • Badiliko la Ajabu Latokea
  • Msongo Kutoka kwa Marafiki wa Zamani
  • Kuwa Watumishi wa Mungu Waliojiweka Wakfu
  • Wakuu wa Gereza Wakiri
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 10/15 kur. 25-29

Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia

KATIKA 1989, MASHAHIDI WA YEHOVA KATIKA POLAND walitambuliwa kisheria kuwa tengenezo la kidini. Mashahidi ambao walikuwa wametiwa gerezani kwa sababu ya kutokuwamo kwao kwa Kikristo hatimaye walifunguliwa, wakiacha wafungwa wengi gerezani ambao walitamani kujifunza mengi juu ya Biblia kutoka kwao. Hiki ni kisa cha jinsi ambavyo katika gereza kama hilo, Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kusaidia wale waliokuwa hapo awali na mioyo migumu kuitikia nguvu ya Neno la Mungu.

KATIKA Wołów, mji wenye idadi ya watu 12,000 ulio kusini-magharibi mwa Poland, kuna gereza la miaka 200 la kurekebishia wahalifu sugu ambamo, baadhi ya wahalifu sugu wa Poland huwekwa. Tangu kutambuliwa kisheria kwa kazi yao, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kupelekea wafungwa huko habari njema za Ufalme, nao hufanya hivyo kwa uchangamfu mkubwa sana.

Kilichoandaa njia kwa urahisi kilikuwa barua iliyotolewa na Wizara ya Haki katika Februari 1990 kwa wakurugenzi wote wa gereza katika Poland. Barua ilishauri kwamba “hawapaswi kufanya iwe vigumu” kwa mfungwa yeyote anayetaka kupokea vichapo vya Watch Tower au kukutana na Mashahidi wa Yehova. Hao Mashahidi, baadhi yao wakiwa wametumia miaka mingi katika gereza la Wołów, waliwajua vizuri wafungwa wengi sugu waliokuwa hapo. Hata hivyo, walimtegemea Yehova abariki jitihada zao za kufanya kweli ya Biblia ilainishe mioyo iliyo migumu ya wafungwa wengine.

Kuanzisha Kazi

“Haikuwa rahisi kuanzisha programu hiyo,” asema Ndugu Czesław kutoka jiji la Wrocław, umbali wa kilometa zipatazo 40, ambaye ameidhinishwa kutembelea gereza katika Wołów. “Ilihitaji mazungumzo ya muda mrefu pamoja na wakuu wa gereza ili wasadikishwe kwamba ‘huduma zetu za kidini’ zilikuwa zenye manufaa kwa wafungwa.”

Ili kutatanisha mambo, akumbuka Paweł mwandamani wa Czesław, “afisa wa cheo cha juu alisisitiza kwamba wafungwa walikuwa wakitumia huduma za kidini tu kuwa kisingizio cha kupata faida za vitu vya kimwili.” Lakini wakati wahalifu watatu waliokuwa hatari walipojitoa kwa ubatizo katika 1991, wakuu wa gereza walibadilisha mtazamo wao na ushirikiano wao ukawa mzuri.

“Tulianza kwa kutolea wafungwa ushahidi, familia zao waliokuja kuwatembelea gerezani, na vilevile wafanyakazi wa gereza hilo la kurekebishia wahalifu sugu,” aeleza Czesław. “Kisha tukaruhusiwa kuhubiri habari njema seli hadi seli, kibali kisicho cha kawaida kabisa. Hatimaye, tulipopata watu wa kwanza waliopendezwa, tulipewa jumba dogo la kuongozea mafunzo ya Biblia na kufanyia mikutano ya Kikristo.” Naam, Yehova alifungua njia kuifikia mioyo migumu ya wafungwa.

Programu ya Kielimu Yenye Matokeo

Punde jumba hilo dogo likawa dogo sana. Kwa kuwa wafungwa waliobatizwa na ndugu waliokuwa wakija kutoka nje walishiriki katika kazi ya kuhubiri, wafungwa wapatao 50 walianza kuhudhuria mikutano. “Kwa zaidi ya miaka mitatu, tulikutana huko, nao wafungwa walihudhuria mikutano ya kila juma kwa ukawaida,” aeleza mmoja wa wazee wa hapo. Kwa hiyo, katika Mei 1995 walipewa jumba kubwa zaidi.

Ndugu wenye daraka wanaamuaje wale wawezao kuja kwenye mikutano inayofanywa gerezani? “Tuna orodha ya wafungwa wanaoonyesha kupendezwa na kweli kwa moyo mweupe,” aeleza Ndugu Czesław na Zdzisław. “Mfungwa asipofanya maendeleo au akikosa mikutano bila sababu nzuri, hivyo akionyesha ukosefu wa uthamini kwa maandalizi hayo, sisi hufuta jina lake katika orodha na kumjulisha mkurugenzi wa gereza.”

Wakati wa mafunzo yao ya Biblia, ndugu hao pia hufundisha wafungwa jinsi ya kujitayarisha kwa ajili ya mikutano na jinsi ya kutumia fasihi kwa matokeo. Hivyo, wafungwa hao wakija mikutanoni, huwa wamejitayarisha vema nao hushiriki kwa uhuru. Wao hutoa maelezo yajengayo, hutumia Biblia zao kwa ustadi, na kutumia shauri kujihusu, mara nyingi wakitia ndani ya maelezo yao mambo kama, ‘Naona ni lazima nifanye hivi au vile.’

“Kwa ujumla, mafunzo ya Biblia 20 yanaongozwa katika gereza la Wołów. Nane kati ya hayo yanaongozwa na wahubiri wafungwa watatu,” asema mwandishi wa kutaniko hilo. Wamekuwa na matokeo mazuri pia wanapohubiri seli hadi seli na wakati wa kutembea kwao katika eneo la gereza. Kwa mfano, katika miezi kumi, kuanzia Septemba 1993 hadi Juni 1994, waligawanya vitabu 235, karibu broshua 300, na magazeti 1,700. Hivi majuzi, maafisa wawili wa gereza waliomba kuwa na funzo la Biblia.

Makusanyiko ya Pekee Yaleta Shangwe

Baada ya muda, sehemu nyingine muhimu iliongezwa kwenye programu ya kielimu katika gereza hilo, yaani, makusanyiko ya pekee. Waangalizi wasafirio na ndugu wengine wenye sifa za ustahili wangetoa sehemu kuu za programu ya kusanyiko la mzunguko na siku ya kusanyiko la pekee katika ukumbi wa michezo wa gereza. Kusanyiko la pekee la kwanza lilifanywa katika Oktoba 1993. Wafungwa 50 walihudhuria, na “familia nzima-nzima, kutia ndani wanawake na watoto wadogo, wamekuja kutoka Wrocław,” likaripoti gazeti la habari Słowo Polskie, kukiwa na hudhurio la watu 139. Mapumziko ya programu ya kusanyiko yalitoa fursa ya kula chakula kilichotayarishwa na akina dada, na vilevile wakati wa ushirika mzuri wa Kikristo.

Makusanyiko mengine saba ya pekee yamefanywa tangu wakati huo, na manufaa zimefikia si wale walio gerezani tu bali pia walio nje. Dada mmoja Shahidi alipomtembelea mfungwa wa zamani wa Wołów anayeishi mjini sasa, mfungwa huyo alikuwa mwenye shaka mara ya kwanza. Lakini alipoambiwa kwamba mfungwa fulani amekuwa Shahidi, mtu huyo alishindwa kusadiki: “Muuaji kimakusudi huyo sasa ni Shahidi?” Tokeo likawa kwamba, mtu huyo alikubali funzo la Biblia.

Badiliko la Ajabu Latokea

Je, programu hii ya kiwango kikubwa kweli imelainisha mioyo iliyo migumu ya wafungwa? Acheni wasimulie.

“Sijapata kamwe kuwajua wazazi wangu kwa sababu waliniacha nilipokuwa mdogo, nami nilikuja kukosa kwa uchungu sana hisi za kupendwa,” akiri Zdzisław, mwanamume ambaye kiasili ni mwenye kutafakari. “Mapema katika maisha yangu, nilihusika na uhalifu, hatimaye nikaua kimakusudi. Hisia ya hatia ilinisukuma nifikirie kujiua, nami nilikuwa nikitafuta sana tumaini la kweli. Ndipo, katika 1987, nikapata gazeti Mnara wa Mlinzi. Kutokana nalo nilijifunza juu ya tumaini la ufufuo na uhai wa milele. Nikitambua kwamba bado kulikuwa na tumaini, niliacha lile wazo la kujiua nami nikaanza kujifunza Biblia. Sasa nimejifunza maana ya upendo kutoka kwa Yehova na akina ndugu.” Tangu 1993, huyu muuaji kimakusudi wa zamani amekuwa akitumikia akiwa mtumishi wa huduma na painia-msaidizi, na mwaka uliopita akawa painia wa kawaida.

Kwa upande ule mwingine, Tomasz, alikubali mara moja funzo la Biblia. “Hata hivyo, hiyo haikuwa hatua ya moyo mweupe,” yeye akiri. “Nilikuwa najifunza tu kwa sababu nilitaka kujionyesha nilipokuwa nikieleza wengine itikadi za Mashahidi wa Yehova. Lakini sikuwa nikifanya mengi sana kuhusu kweli ya Biblia. Siku moja, niliazimia nami nikaenda kwenye mkutano wa Kikristo. Wafungwa waliobatizwa walinikaribisha kwa uchangamfu. Nilitambua kwamba badala ya kujaribu kujionyesha na ujuzi, nilipaswa kulainisha moyo wangu ulio mgumu na kugeuza akili yangu.” Tomasz alianza kujivika utu mpya wa Kikristo. (Waefeso 4:22-24) Leo, yeye ni Shahidi aliyejiweka wafu na kubatizwa naye hufurahia kuhubiri seli hadi seli.

Msongo Kutoka kwa Marafiki wa Zamani

Wale waliojifunza kweli ya Biblia wakiwa gerezani walipata msongo mkali kutoka kwa marafiki wa zamani katika jela na kutoka kwa maafisa wa gereza. Mmoja wao akumbuka: “Nilikuwa nikidhihakiwa kila mara na kudharauliwa. Lakini nilikumbuka maneno yenye kutia moyo ya akina ndugu. ‘Endelea kutoa sala kwa Yehova,’ wakaniambia. ‘Soma Biblia yako nawe utahisi amani ya kindani.’ Kwa kweli hilo lilinisaidia.”

“Wafungwa wenzangu hawakukosa kuniambia maneno makali,” asema Ryszard, ndugu mwenye nguvu aliyebatizwa. “‘Waweza kwenda kwenye mikutano yako, lakini usijaribu kujitokeza na kujifanya wewe ni bora zaidi, Sawa?’ walikuwa wakinionya. Nilipofanya mabadiliko maishani mwangu kwa sababu ya kutumia kanuni za Biblia, ilinibidi niteseke kwa sababu hiyo. Walipindua kitanda changu, wakatupa fasihi zangu za Biblia, na kuchafua sehemu yangu katika seli. Nilitoa sala kwa Yehova anipe nguvu ya kujidhibiti kisha kwa utulivu nikaanza kufanya hiyo sehemu yangu ya seli iwe nadhifu. Baada ya muda fulani, mashambulio hayo yalikoma.”

“Wafungwa wenzetu waonapo kwamba tumefanya uamuzi imara wa kumtumikia Yehova,” wasimulia ndugu wengine wafungwa waliobatizwa, “msongo wa aina tofauti hutokea. Wao huelekea kusema hivi, ‘Kumbuka, haupaswi kunywa, kuvuta sigareti, au kudanganya tena.’ Aina hiyo ya msongo humsaidia mtu adhibiti mwili wake, akiacha haraka maovu yoyote au uraibu wowote. Pia husaidia mtu asitawishe matunda ya roho.”—Wagalatia 5:22, 23.

Kuwa Watumishi wa Mungu Waliojiweka Wakfu

Kwa ruhusa ya wakuu wa gereza, ubatizo wa kwanza ulifanyiwa katika jumba la ukumbi wa michezo katika masika ya 1991. Zdzisław alikuwa ndiye mtaka-kubatizwa mwenye furaha. Wafungwa 12 walihudhuria, na ndugu na dada 21 kutoka nje walikuja kwa ajili ya pindi hiyo. Mkutano huo ulikuwa na matokeo yenye kutia moyo kwa wafungwa. Idadi fulani kati yao walifanya maendeleo makubwa sana hivi kwamba wafungwa wengine wawili walibatizwa baadaye mwaka huohuo. Miaka miwili baadaye, katika 1993, ubatizo ulifanywa mara mbili, na wafungwa saba wengine walionyesha wakfu wao kwa Yehova!

Gazeti la mahali hapo la kila siku Wieczór Wrocławia, likiripoti kuhusu ubatizo uliofanywa Desemba, lilisema hivi: “Watu wanaendelea kumiminika katika jumba la ukumbi wa michezo, wakisalimiana na wote kwa mikono. Hakuna mtu asiyemfahamu mwingine hapo. Wanafanyiza familia moja kubwa, iliyounganisha katika kufikiri, katika njia yao ya maisha, na katika kumtumikia Mungu mmoja, Yehova.” “Familia [hiyo] moja kubwa” wakati huo ilikuwa na watu 135, kutia ndani wafungwa 50. Acheni tukutane na baadhi yao.

Jerzy, aliyebatizwa Juni asimulia: “Ijapokuwa nilikuwa nimesikia kweli ya Biblia miaka kadhaa iliyopita, nilikuwa na moyo mgumu kwelikweli. Upunjaji, talaka kutoka kwa mke wangu wa kwanza, uhusiano wa haramu na Krystyna, mtoto nje ya kifungo cha ndoa, na kurudi-rudi gerezani—ndivyo yalivyokuwa maisha yangu.” Alipoona jinsi wahalifu wengine sugu walivyokuja kuwa Mashahidi wakiwa gerezani, alianza kujiuliza mwenyewe, ‘Je, siwezi kuwa mtu mzuri pia?’ Aliomba funzo la Biblia naye akaanza kuja kwenye mikutano. Hata hivyo, wakati wa badiliko la maana kwake ulikuja alipojua kutoka kwa mwendesha mashtaka wa umma kwamba Krystyna alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova miaka mitatu mapema. “Nilishangaa sana!” asema Jerzy. “Nilifikiri, ‘Vipi mimi? Nafanya nini?’ Nilitambua kwamba ili nikubaliwe na Yehova, ilinibidi nirekebishe maisha yangu.” Tokeo likawa kwamba, muungano wenye furaha ulitokea gerezani—pamoja na Krystyna na binti yao mwenye umri wa miaka 11, Marzena. Kabla ya muda mrefu, walihalalisha ndoa yao. Ingawa bado yumo gerezani, anamokuwa na nyakati za heri na shari, majuzi Jerzy alijifunza lugha ya ishara naye anaweza kuwasaidia wafungwa viziwi.

Mirosław alikuwa tayari amehusika na mambo ya uhalifu alipokuwa katika shule ya msingi. Alipendezwa sana na vile rafiki zake walivyokuwa wakifanya, na upesi akaanza kufanya vivyo hivyo. Alinyang’anya na kupiga watu wengi. Kisha akajipata gerezani. “Nilipojipata gerezani, nilimgeukia kasisi ili nipate msaada,” akiri Mirosław. “Lakini nilitamaushwa sana. Basi nikaamua kwamba ningejiua kwa kunywa sumu.” Siku hiyo hiyo aliyopanga kujiua, alihamishwa hadi kwenye seli nyingine. Hapo alipata nakala ya Mnara wa Mlinzi iliyoongea kuhusu kusudi la uhai. “Habari sahili iliyo wazi ilithibitika kuwa tu kile nilichohitaji,” yeye aongezea. “Sasa nilitaka kuishi! Kwa hiyo, nilisali kwa Yehova na kuwaomba Mashahidi funzo la Biblia.” Alifanya maendeleo ya haraka katika funzo lake la Biblia naye akabatizwa katika 1991. Sasa yeye hutumikia akiwa painia-msaidizi gerezani, akiwa na pendeleo la kuhubiri seli hadi seli.

Jumla ya wafungwa 15 kufikia sasa wamebatizwa. Hukumu zao zikijumlishwa zafikia jumla ya miaka karibu 260. Wengine walifunguliwa kabla ya kumaliza hukumu zao. Mfungwa mmoja alipunguziwa kwa miaka 10 hukumu yake ya miaka 25. Na wengine kadhaa walioonyesha kupendezwa wakiwa gerezani walikuja kuwa Mashahidi waliobatizwa baada ya kufunguliwa. Kwa kuongezea, kuna wafungwa wengine wanne gerezani wanaojitayarisha kwa ajili ya ubatizo.

Wakuu wa Gereza Wakiri

“Badiliko la mtazamo wa wafungwa limetambulikana kabisa,” yasema ripoti moja ya gereza. “Wengi huacha kuvuta sigareti, nao husafisha seli zao. Mabadiliko kama hayo katika mwenendo yako dhahiri kwa wafungwa wengine.”

Gazeti la habari Życie Warszawy laripoti kwamba usimamizi wa gereza la kurekebishia wahalifu sugu katika Wołów lilikiri kwamba “wafungwa wametiwa nidhamu; hawawaletei askari wa gereza matatizo yoyote.” Makala hiyo yaendelea kuonyesha kwamba wale waliofunguliwa kabla ya kumaliza hukumu zao wameungana ifaavyo na kikundi cha Mashahidi wa Yehova nao hawafanyi uhalifu tena.

Na maoni ya mkurugenzi wa gereza ni yapi? “Kazi ya Mashahidi wa Yehova katika gereza hili la kurekebishia wahalifu sugu ni yenye kupendeza zaidi na yenye kusaidia,” yeye asema. Huyo mkurugenzi akiri kwamba “katika funzo lao la Biblia [pamoja na Mashahidi], sifa na viwango vya wafungwa hubadilika, vikiwapa nguvu mpya ya mwongozo maishani mwao. Mwenendo wao ni wenye busara na mpole. Wao ni wafanyakazi wenye bidii, wasiotokeza matatizo yoyote.” Maelezo hayo mazuri kutoka kwa wakuu hao, bila shaka yanafurahisha Mashahidi wanaofanya kazi pamoja na wafungwa katika gereza la Wołów.

Mashahidi wenye kutembelea huko wanathamini kikamili maneno ya Yesu: “Najua kondoo wangu na kondoo wangu wanijua mimi. . . . Nao watasikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yohana 10:14, 16) Hata kuta za gereza haziwezi kumzuia Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, kukusanya walio mfano wa kondoo. Mashahidi katika Wołów ni wenye shukrani kwamba wana pendeleo la kushiriki utumishi huu wenye shangwe. Nao wanamtumaini Yehova kwa baraka zake zenye kuendelea katika kusaidia mioyo ya wengi zaidi wenye mioyo migumu, waitikie habari njema za Ufalme kabla mwisho haujaja.—Mathayo 24:14.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Tatizo la “Mtoto Mkubwa”

“Baada ya kuwa gerezani kwa muda fulani, mfungwa mara nyingi huwa haelewi kinachomaanishwa na kuishi akiwa huru, au kujitegemea,” ndivyo wanavyoona Mashahidi wanaohubiri katika gereza la kurekebishia wahalifu sugu katika Wołów. “Lile tulilo nalo hasa ni tatizo la ‘mtoto mkubwa,’ mtu ambaye akifunguliwa kutoka gerezani hajui jinsi ya kujitunza mwenyewe. Hiyo ndiyo sababu daraka la kutaniko lahusu mengi zaidi ya kumfundisha tu kweli ya Biblia. Lazima tumtayarishe kuwa sehemu ya jumuiya, kumwonya juu ya hatari mpya na majaribu ambayo huenda akakabili. Ingawa twawa waangalifu tusiwe wenye kulinda kupita kiasi, lazima tumsaidie aanze maisha upya.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki