Je, Utatii Onyo?
MEI 19, 1997, tufani ilikumba wilaya ya Chittagong, Bangladesh. Pepo zilizovuma kwa mwendo wa kilometa 250 kwa saa zilirekodiwa katika mji wa Cox Bazaar. Katika sehemu za mashambani, vibanda vilivyoezekwa kwa nyasi vilipotea tu, ikibaki miraba ya matope mahali ambapo vilikuwa vimesimama wakati mmoja. Miti na fito za simu ziling’olewa; mingine ikavunjwa katikati kama vijiti vya kiberiti. Kichwa kikuu cha gazeti la habari Bhorar Kagoj kiliripoti kwamba watu 105 waliuawa na tufani hiyo.
Watabiri wa hali ya hewa walitangaza tufani hiyo muda wa saa 36 hivi kabla ya kutokea. Bila shaka, uhai wa watu wengi uliokolewa kwa kuwa mamia ya maelfu ya watu walikimbilia kwenye majengo ya kujisetiri na tufani.
Kwa miaka zaidi ya mia moja sasa, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitangaza habari za msiba unaokaribia sana ambao ni wenye kuangamiza zaidi ya tufani yoyote. Biblia huuita “siku ya BWANA iliyo kuu na itishayo.” (Yoeli 2:31) Kwa kutii ujumbe mbalimbali wa kiunabii wa onyo unaopatikana katika Biblia, sisi twaweza kuepuka ukali wake.—Sefania 2:2, 3.
La, Mashahidi wa Yehova si manabii wa maangamizi. Ujumbe wao ni wa tumaini. Wanatamani kusaidia watu wajifunze juu ya Ufalme wa Mungu, ambao hivi karibuni utaondolea dunia ukosefu wote wa uadilifu. Neno la Mungu, Biblia, hutuambia hivi: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
WHO/League of Red Cross