Walioungana Katika Njia Bora Zaidi ya Maisha
Ikiwa idadi ya watu duniani itaendelea kuongezeka, karibuni kutakuwa na watu bilioni sita duniani. Ingawa wote wametoka kwa mzazi mmoja, walio wengi wana mwelekeo wa kukataa kuwa wao ni sehemu ya familia moja ya duniani kote inayowajibika kwa Muumba mwenye hekima na upendo. Ile migawanyiko na ugomvi kati ya mataifa, jamii za watu, na tamaduni hutoa ushuhuda wenye kuhuzunisha juu ya hali hii mbaya ya mambo.
TUKITAZAMA hali ya sasa ya mambo ulimwenguni, muungano wa duniani kote huenda ukaonekana kuwa mradi usioweza kufikiwa. Kichapo The Columbia History of the World chasema: “Kulihusu lile swali la muhimu sana juu ya jinsi ya kuishi pamoja, ulimwengu wa sasa hauna wazo lolote jipya juu ya namna ya kufikia hilo, la, hauna hata wazo moja.”
Ingawa hivyo, kule kuunganisha watu wote duniani hakuhitaji wazo jipya. Njia iongozayo kwenye muungano imeonyeshwa katika Maandiko Matakatifu. Njia hiyo yategemea kumwabudu Yule aliyeiumba dunia na uhai wote uliomo duniani. Muungano wa kweli katika fikira, kusudi, na njia ya maisha tayari umo miongoni mwa watu wa Mungu. Wakiwa zaidi ya milioni tano na nusu katika mabara 233, watu hao wameungana katika usadikisho wao kuwa njia ya Mungu ya maisha ndiyo njia bora zaidi. Kama mtunga-zaburi, wao husali hivi: “Ee BWANA, unifundishe njia yako; nitakwenda katika kweli yako; moyo wangu na ufurahi [“unganisha moyo wangu,” NW] kulicha jina lako.”—Zaburi 86:11.
Hali hii ya watu kuungana katika ibada safi ilitabiriwa zamani sana na nabii Isaya. Yeye aliandika: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isaya 2:2, 3.
Muungano wa Mashahidi wa Yehova ni wa kipekee. Katika makutaniko zaidi ya 87,000 ulimwenguni kote, wao hushiriki chakula kilekile cha kiroho katika mikutano yao juma baada ya juma. (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, kuanzia katikati mwa mwaka wa 1998 hadi mapema mwaka wa 1999, Mashahidi waliudhihirisha muungano wao kwa njia iliyo tofauti—kwa kukusanyika katika Mikusanyiko yao ya siku tatu yenye kichwa “Njia ya Mungu ya Maisha” iliyofanywa ulimwenguni kote. Katika nchi 13, mikusanyiko hiyo ilihudhuriwa na wajumbe kutoka nchi mbalimbali na iliitwa mikusanyiko ya kimataifa. Mingine iliitwa mikusanyiko ya wilaya. Hata hivyo, mikusanyiko hiyo yote ilikuwa na programu ileile ya mambo ya kiroho yenye kujenga.
Lilikuwa jambo la kupendeza wee kuwaona wajumbe wenye furaha, waliovalia kinadhifu wakimiminika kwenye kumbi na wanja za michezo ili kufundishwa na Yehova! Yenye kutokeza ni maelezo yaliyotolewa na mmoja wa wajumbe waliohudhuria mkusanyiko wa kimataifa uliofanywa mjini Michigan, Marekani. Alisema: “Ilikuwa shangwe kubwa kuwaona ndugu zetu kutoka sehemu zote ulimwenguni—Jamhuri ya Cheki, Barbados, Nigeria, Hungaria, Uingereza, Uholanzi, Ethiopia, Kenya, na nchi nyinginezo nyingi—wakikumbatiana! Lilikuwa jambo zuri sana kuwaona ndugu wakiishi pamoja kwa muungano, wakitoa machozi ya shangwe kwa sababu ya upendo walio nao kwa mmoja na mwenzake na kwa Mungu wao mkuu, Yehova.” Makala ifuatayo itachunguza programu hiyo ya mkusanyiko iliyofurahiwa na mamilioni ya watu duniani kote.
[Picha katika ukurasa wa 3 zimeandaliwa na 3]
Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.