“Umoja wa Ufalme’’ Makusanyiko ya Wilaya
“UMOJA WA UFALME.” Ni kichwa kizuri na chenye kufaa kama nini cha makusanyiko ya wilaya yetu ya mwaka wa 1983! Hakuna wakati umepata kuwa na ukosefu mwingi wa umoja ulimwenguni kama sasa. Matengenezo ya kidini, ya Kikatoliki na Kiprotestanti pia, yameenewa na mizozo na ugomvi. Vyama vya kisiasa vinataka kuuana. Hakujapata wakati mwingine kuwako mvurugo mwingi katika jamii ya kibiashara kama ule ulioko siku hizi. Hapo kwanza jamaa hazijapata kutatanishwa na ukosefu mwingi wa umoja kama ilivyo sasa, huku mume na mke wakipigana, wakitorokana na kutalikana. Tena ni wakati gani mwingine umepata kuwa na pengo linalozidi kupanuka la kutopashana habari kati ya wazazi na watoto wao kama ilivyo leo?
Lakini tengenezo lionekanalo la Yehova, yaani, jamii ya mashahidi Wakristo wa Yehova, liko tofauti sana katika hali zote hizo. Wao wameungana, wakiwa zaidi ya 2,400,000, ingawa wametawanyika katika nchi na visiwa vya bahari vyenye jumla ipatayo 205. Umoja wao ni ule unaoshinda vizuizi vya ubaguzi wa kitaifa, lugha na vya kikabila, vya kitamaduni na vya kiuchumi. Ni kitu gani kimewaunganisha? Ni ibada safi ya Yehova Mungu.—Sefania 3:9.
Hivyo ndivyo inavyopasa kuwa kati ya wafuasi wa kweli wa Kristo, kwa maana mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho nini kwenye 1 Wakorintho l:10? Kwamba ‘pasiwe faraka kwao, bali wote wanene mamoja, na wahitimu katika nia moja na shauri moja.’ Vivyo hivyo, kwenye Wafilipi 3:15, 16 anashauri kwamba waliokomaa wawe na nia ile ile moja. Na je! kwani umoja haupasi kuwa alama ya kutambulisha walio wafuasi wa kweli wa Kristo kulingana na maneno yake ya kwamba kwa kupendana wao kwa wao Wakristo wote wa kweli wangetambuliwa? Kwa uhakika, upendo unaleta umoja.—Yohana 13:34, 35.
Kwa kweli umoja huo ulitabiriwa kwenye Isaya 52:8, kwa maneno haya: “Sauti ya walinzi wako! Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja; maana wataona jicho kwa jicho, jinsi [Yehova arejezavyo] Sayuni.” Mambo yenye kuonekana wazi yanaonyesha kwamba kurejezwa kwa Sayuni kulianza mwaka wa 1919.
Si jambo jepesi hata kidogo kuendeleza umoja huo. Hiyo ni kwa sababu ya hasira kuu ambayo Ibilisi anaonyesha, akijua ana kipindi kifupi cha wakati, na pia kwa sababu ya kuharibika-haribika kwa kanuni za kidini na za kibinadamu katika siku zetu. (Ufunuo 12:9, 12) Chakula cha kiroho kitakachopakuliwa kwenye makusanyiko ya mwaka huu hakika kitaikaza nia ya watumishi wa Yehova wote wasikuze udhaifu, makosa na hali za kutokamilika kwa kibinadamu za wenzao, kwa faida ya jina na kazi ya Yehova Mungu. Programu hiyo nzuri ya kusanyiko itaanza alasiri ya Alhamisi mpaka alasiri ya Jumapili. Itakuwa yenye kuufaa wakati huu na yenye kujenga. Na bila shaka wote wataondoka kusanyikoni wakiwa wametayarishwa vizuri zaidi kumtumikia Yehova Mungu kwa umoja pamoja na ndugu zao na wakiwa na nia iliyokazwa ya kufanya hivyo.