“Ningeweza Kuihisi Hali Hiyo ya Amani”
MWANAMUME mmoja anayesema Kijerumani alienda kwenye mkusanyiko uliopangwa na Mashahidi wa Yehova ili “kuwapeleleza” Mashahidi. Kwa nini? Lengo lake lilikuwa “kulifichua dhehebu hili na kuwazuia rafiki zake wasipotoshwe.” Baada ya kuhudhuria huo mkusanyiko, aliwaandikia rafiki zake barua ifuatayo:
“Nilipolikaribia eneo la mkusanyiko, nilianza kuwazia kama kweli hiyo ndiyo sehemu niliyokuwa nikiitafuta. Hapakuwa na yeyote nje ya stediamu, wala hapakuwa takataka yoyote au mikebe ya bia kwenye sakafu. Nilipokaribia, niliwaona wanaume wawili langoni mwa stediamu hiyo. Walinisalimu na kunikaribisha ndani.
“Nilitarajia kusikia kelele kutoka kwa maelfu waliotarajiwa kuwa humo, lakini hali ilikuwa tulivu sana. ‘Haya,’ nikafikiri, ‘labda mna watu wachache tu waliotawanyika mahali pote.’
“Nilipoingia ndani, nilivutiwa mara moja na drama iliyokuwa ikiendelea jukwaani. Ni baadaye tu ndipo nilipotambua kwamba stediamu hiyo ilikuwa imejaa kabisa maelfu ya wasikilizaji wenye makini. Ningeweza kuihisi hali hiyo ya amani. Yale niliyosikia, kuona, na kuhisi sehemu iliyobaki ya mkusanyiko huo yaliniathiri sana.
“Nilipoendelea kuchangamana na Mashahidi hao, nilitambua kwamba walikuwa na nyuso zenye furaha na usemi wenye upendo. Kwa ghafula, sikuweza kujizuia kuwaza, ‘Kwa kweli hawa ni watu wa Mungu!’”
Badala ya ‘kuwazuia rafiki zake wasipotoshwe,’ huyo mwanamume mchanga aliwaomba Mashahidi wamfunze Biblia. Tokeo likawa nini? Leo, yeye ni mzee Mkristo. Yeye na familia yake ni watendaji katika mojawapo ya makutaniko yaliyoko mjini Zug, Uswisi.