Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” Yetu
“Kila kitu kitaishi po pote utakapofikilia mto huo.”—EZEKIELI 47:9.
1, 2. (a) Maji yana umuhimu gani? (b) Maji kwenye mto wa kimaono wa Ezekieli hufananisha nini?
MAJI ni kitu cha ajabu. Uhai wote duniani huyategemea. Hakuna yeyote kati yetu awezaye kuishi kwa muda mrefu bila maji. Pia twayatumia kwa kusafisha, kwa kuwa maji yaweza kufyonza na kuondolea mbali uchafu. Hivyo, sisi hutumia maji kuogea, kufulia nguo, na hata kuoshea vyakula. Kufanya hivyo kwaweza kuokoa uhai wetu.
2 Biblia hutumia maji kufananisha maandalizi ya Yehova ya kiroho kwa ajili ya uhai. (Yeremia 2:13; Yohana 4:7-15) Maandalizi haya yatia ndani kusafishwa kwa watu wake kupitia fidia ya dhabihu ya Kristo na ujuzi juu ya Mungu ulio katika Neno lake. (Waefeso 5:25-27) Katika ono la Ezekieli la hekalu, mto wa kimwujiza unaotiririka kutoka kwenye hekalu hufananisha baraka hizo zinazotokeza uhai. Lakini mto huo hutiririka lini, nao wamaanisha nini kwetu leo?
Mto Watiririka Katika Nchi Iliyorudishwa
3. Ezekieli aliona nini, kama ilivyoripotiwa kwenye Ezekieli 47:2-12?
3 Wakiwa mateka huko Babiloni, watu wa Ezekieli walihitaji sana maandalizi ya Yehova. Basi ilimtia Ezekieli moyo kama nini kuona mchuruziko wa maji ukitokea mahali patakatifu na kutiririka kutoka ndani ya hekalu la kimaono! Malaika fulani akipima kijito hicho baada ya kila dhiraa 1,000. Kina chake chaongezeka kutoka kifundo cha mguu hadi kufikia magotini, kutoka magotini hadi kiunoni, halafu unakuwa mto ambao mtu ahitaji kuogelea. Mto huo hutokeza uhai na mazao. (Ezekieli 47:2-11) Ezekieli aambiwa: “Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula.” (Ezekieli 47:12a) Mto huo unapoingia Bahari ya Chumvi—maji yasiyo na uhai—uhai waanza! Samaki watokea kwa wingi. Biashara ya uvuvi yasitawi.
4, 5. Ni jinsi gani unabii wa Yoeli unaohusu mto unafanana na ule wa Ezekieli, na kwa nini hilo ni muhimu?
4 Huenda unabii huo mzuri uliwakumbusha Wayahudi wahamishwa unabii mwingine uliorekodiwa zaidi ya karne mbili mapema: “Chemchemi itatokea katika nyumba ya BWANA, na kulinywesha bonde la Shitimu.”a (Yoeli 3:18) Unabii wa Yoeli, kama ulivyo wa Ezekieli, unatabiri kwamba mto ungetiririka kutoka kwenye nyumba ya Mungu, lile hekalu, na kutokeza uhai katika eneo la ukame.
5 Kwa muda mrefu gazeti Mnara wa Mlinzi limeeleza kwamba unabii wa Yoeli unatimizwa siku zetu.b Kwa hakika basi, iko vivyo hivyo kwa habari ya ono la Ezekieli linalofanana na unabii huo. Katika nchi iliyorudishwa ya watu wa Mungu leo, kama tu katika Israeli la kale, baraka za Yehova zimetiririka kwelikweli.
Mtiririko Mkubwa wa Baraka
6. Kunyunyizwa kwa damu katika madhabahu ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha Wayahudi juu ya nini?
6 Ni nini chanzo cha baraka ambazo watu wa Mungu waliorudishwa wanazo? Naam, ona kwamba maji hayo hutiririka kutoka hekalu la Mungu. Vivyo hivyo leo, baraka hizo huja kutoka kwa Yehova kupitia hekalu lake kubwa la kiroho—mpango kwa ajili ya ibada safi. Ono la Ezekieli laongezea jambo fulani muhimu. Katika ua wa ndani, kijito hicho chatiririka kupitia kusini mwa madhabahu. (Ezekieli 47:1) Madhabahu imo katikati hasa mwa hekalu hilo la kimaono. Yehova amfafanulia Ezekieli kwa makini kuihusu na aamuru kwamba damu ya dhabihu inyunyizwe juu yake. (Ezekieli 43:13-18, 20) Madhabahu hiyo ilikuwa na maana kubwa sana kwa Waisraeli wote. Agano lao na Yehova lilikuwa limehalalishwa muda mrefu mapema wakati Musa aliponyunyiza damu juu ya madhabahu iliyokuwa chini ya Mlima Sinai. (Kutoka 24:4-8) Kunyunyizwa kwa damu juu ya madhabahu hiyo ya kimaono kulipaswa kuwakumbusha kwamba mara warudipo kwenye nchi yao iliyorudishwa, baraka za Yehova zingetiririka maadamu wangeishi kulingana na agano lao naye.—Kumbukumbu la Torati 28:1-14.
7. Wakristo leo wanapata maana gani katika madhabahu ya ufananisho?
7 Hali kadhalika, watu wa Mungu leo wanabarikiwa kupitia agano—lililo bora, agano jipya. (Yeremia 31:31-34) Hilo pia lilihalalishwa muda mrefu uliopita kwa damu ya Yesu Kristo. (Waebrania 9:15-20) Leo, tuwe miongoni mwa watiwa-mafuta, ambao ni washiriki wa agano hilo, au miongoni mwa “kondoo wengine,” ambao wanafaidika kutokana nalo, twapata maana kubwa katika madhabahu hiyo ya mfano. Hiyo hufananisha mapenzi ya Mungu kuhusiana na dhabihu ya Kristo. (Yohana 10:16; Waebrania 10:10) Kama tu vile madhabahu hiyo ya ufananisho imo katikati hasa mwa hekalu la kiroho, dhabihu ya fidia ya Kristo ni ya umuhimu mkubwa katika ibada safi. Hiyo ndiyo msingi wa msamaha wa dhambi zetu na kwa sababu hiyo, dhabihu hiyo inakuwa pia msingi wa matumaini yetu yote ya wakati ujao. (1 Yohana 2:2) Hivyo, twajitahidi kuishi kulingana na sheria inayohusishwa na hilo agano jipya, “sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Maadamu twafanya hivyo, tutafaidika kutokana na maandalizi ya Yehova ya uhai.
8. (a) Ni nini ambacho ua wa ndani wa hekalu la kimaono ulikosa? (b) Makuhani kwenye hekalu la kimaono wangejisafisha kwa njia gani?
8 Faida moja ya aina hiyo ni msimamo safi mbele za Yehova. Katika hekalu hilo la kimaono, ua wa ndani unakosa kitu fulani ambacho kilitokeza sana katika ua wa tabenakulo na katika hekalu la Solomoni—beseni kubwa, ambayo baadaye iliitwa bahari, kwa ajili ya makuhani kuogea ndani. (Kutoka 30:18-21; 2 Mambo ya Nyakati 4:2-6) Je, makuhani katika hekalu la kimaono la Ezekieli wangetumia nini kusafishia? Naam, kijito kile cha kimwujiza kinachotiririka kupitia ua wa ndani! Ndiyo, Yehova angewabariki kwa kuwawezesha kufurahia msimamo safi, au mtakatifu.
9. Ni jinsi gani watiwa-mafuta na umati mkubwa waweza kuwa na msimamo safi leo?
9 Vivyo hivyo leo, watiwa-mafuta wamebarikiwa kwa kupewa msimamo safi mbele za Yehova. Yehova huwaona kuwa watakatifu, akiwatangaza kuwa waadilifu. (Waroma 5:1, 2) Vipi juu ya “umati mkubwa,” unaofananishwa na yale makabila yasiyo ya kikuhani? Wao wanaabudia katika ua wa nje, na kijito kile kile hupitia ndani ya sehemu hiyo ya hekalu la kimaono. Basi, yafaa kama nini, kwamba mtume Yohana aliona umati mkubwa ukiwa umevaa kanzu safi nyeupe wanapoabudia katika ua wa hekalu la kiroho! (Ufunuo 7:9-14) Haidhuru wametendewa vipi katika ulimwengu huu ulioshuka kiadili, wanaweza kuwa na uhakika kwamba maadamu wanazoea imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo, Yehova awaona kuwa safi na wenye kutakata. Wanajizoezaje imani? Kwa kufuata hatua za Yesu, wakiwa na uhakika kamili katika dhabihu ya fidia.—1 Petro 2:21.
10, 11. Ni ipi iliyo sehemu moja muhimu ya maji ya ufananisho, na hiyo yahusuje mpanuko wa ajabu wa mto huo?
10 Kama ilivyotangulia kutajwa, kuna sehemu nyingine muhimu ya maji haya ya ufananisho—ujuzi. Katika Israeli lililorudishwa, Yehova aliwabariki watu wake kwa mafundisho ya Kimaandiko kupitia ukuhani. (Ezekieli 44:23) Kwa njia kama hiyo, Yehova amewabariki watu wake leo kwa mafundisho tele juu ya Neno lake la kweli, kupitia ule “ukuhani wa kifalme.” (1 Petro 2:9) Ujuzi juu ya Yehova Mungu, juu ya makusudi yake kwa wanadamu, na hasa juu ya Yesu Kristo na Ufalme wa Kimesiya umetiririka kwa wingi unaozidi kuongezeka daima wakati huu wa siku za mwisho. Burudisho la mbubujiko wa kiroho tunaopata na ambao unazidi kuongezeka ni tukufu jinsi gani!—Danieli 12:4.
11 Kama vile ule mto ambao malaika aliupima ulivyoendelea kuongezeka kina hatua kwa hatua, ndivyo mtiririko wa baraka zinazotokeza uhai kutoka kwa Yehova umeongezeka sana ili kutosheleza mmiminiko wa watu wanaoingia katika nchi yetu ya kiroho iliyobarikiwa. Unabii mwingine wa urudisho ulitabiri hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Maneno hayo yametimia—mamilioni ya watu wamemiminika makundi makundi na kujiunga nasi katika ibada safi! Yehova amefanya “maji” mengi sana yapatikane kwa wote wanaomjia. (Ufunuo 22:17) Yeye huhakikisha kwamba tengenezo lake la kidunia hugawa Biblia na fasihi za Biblia ulimwenguni pote, katika mamia ya lugha. Vivyo hivyo, mikutano ya Kikristo na mikusanyiko imepangwa ulimwenguni pote ili wote waweze kupewa maji safi kabisa ya kweli. Maandalizi hayo huwaathirije watu?
Maji Yatokeza Uhai!
12. (a) Ni kwa nini miti iliyo katika ono la Ezekieli yaweza kuzaa kama ifanyavyo? (b) Miti hiyo yenye kuzaa sana huwakilisha nini katika siku za mwisho?
12 Mto katika ono la Ezekieli watokeza uhai na afya. Ezekieli anapopata kujua juu ya miti ambayo ingekua kando-kando ya mto huo, aambiwa: “Majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; . . . na matunda yake yatakuwa chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.” Kwa nini miti hiyo huzaa kwa njia hii yenye kustaajabisha? “Kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu.” (Ezekieli 47:12b) Miti hiyo ya mfano hufananisha kimbele maandalizi yote ya Mungu kwa ajili ya kurudisha wanadamu kwenye ukamilifu kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. Hapa duniani wakati huu, baki la watiwa-mafuta huongoza katika kuandaa lishe na ponyo la kiroho. Baada ya wale 144,000 wote kupokea thawabu yao ya kimbingu, faida zinazotokana na utumishi wao wa kikuhani wakiwa watawala-wenzi pamoja na Kristo zitaenea hadi wakati ujao, hatimaye zikiongoza kwenye kushindwa kabisa kwa kifo cha Kiadamu.—Ufunuo 5:9, 10; 21:2-4.
13. Ni ponyo gani limetimizwa wakati wetu?
13 Mto huo wa kimaono unaingia katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai na kuponya chochote ambacho hukifikia. Bahari hiyo hufananisha mazingira yaliyokufa kiroho. Lakini uhai watokea kwa wingi ‘kila mahali ufikapo mto huo.’ (Ezekieli 47:9) Vivyo hivyo, katika siku za mwisho, watu wamefanywa hai kiroho kokote ambako maji ya uhai yamepenyeza. Watu wa kwanza kutiwa uhai mpya jinsi hiyo ni baki la watiwa-mafuta mwaka wa 1919. Walirudishwa kighafula kwenye uhai wa kiroho kutoka hali iliyo kama kifo, ya kutotenda. (Ezekieli 37:1-14; Ufunuo 11:3, 7-12) Tangu wakati huo maji hayo ya uhai yamewafikia watu wengine walio wafu kiroho, nao wamekuwa hai na kufanyiza umati mkubwa wa kondoo wengine unaozidi kuongezeka daima, wanaompenda na kumtumikia Yehova. Hivi karibuni, uandalizi huu utafikia halaiki ya watu watakaofufuliwa.
14. Biashara ya uvuvi inayositawi sehemu fulani ya ufuo wa Bahari ya Chumvi yaonyesha vizuri jambo gani leo?
14 Uhai wa kiroho hutokeza uzalishaji. Hilo laonyeshwa kwa biashara ya uvuvi inayositawi kwenye fuo za bahari ambayo hapo kwanza ilikuwa imekufa. Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Katika siku za mwisho, kazi ya uvuvi ilianza kwa kukusanywa kwa mabaki ya watiwa-mafuta, lakini haijakomea hapo. Maji yenye kutokeza uhai yatokayo katika hekalu la kiroho la Yehova, kutia ndani baraka ya ujuzi sahihi, yaathiri watu wa mataifa yote. Kokote ambako mto huo umefikia, uhai wa kiroho umetokezwa.
15. Ni nini kionyeshacho kwamba si kila mtu atakayekubali maandalizi ya Mungu ya uhai, nalo tokeo la mwisho ni nini kwa watu kama hao?
15 Bila shaka, si wote huitikia ujumbe wa uhai ifaavyo sasa; wala si wote watakaofufuliwa wakati wa Utawala wa Milenia wa Kristo wataitikia ifaavyo. (Isaya 65:20; Ufunuo 21:8) Malaika atangaza kwamba sehemu fulani za bahari haziponywi. Sehemu hizo zenye matope, zisizo na uhai ‘zaachwa ziwe za chumvi.’ (Ezekieli 47:11) Kwa habari ya watu wa siku yetu, si wote huyakubali maji ya Yehova yenye kutokeza uhai wanayopewa. (Isaya 6:10) Kwenye Har–Magedoni, wale wote ambao wamechagua kubaki katika hali isiyo na uhai na yenye ugonjwa kiroho wataachiwa chumvi, yaani, wataharibiwa milele. (Ufunuo 19:11-21) Hata hivyo, wale ambao wamekuwa wakinywa maji hayo kwa uaminifu wanaweza kutumaini kuokoka na kuona utimizo wa mwisho wa unabii huu.
Mto Huo Watiririka Katika Paradiso
16. Ni lini na jinsi gani ono la Ezekieli la hekalu litakuwa na utimizo wake wa mwisho?
16 Kama ulivyo unabii mwingine mbalimbali wa urudisho, ono la Ezekieli la hekalu hupata utimizo wake wa mwisho wakati wa ile Milenia. Wakati huo jamii ya kikuhani haitakuwa tena hapa duniani. “Watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye [mbinguni] kwa miaka elfu.” (Ufunuo 20:6) Makuhani hawa wa kimbingu watashirikiana na Kristo katika kutoa manufaa kamili ya fidia ya dhabihu ya Kristo. Hivyo, wanadamu waadilifu wataokolewa, wakiwa wamerudishwa kwenye ukamilifu!—Yohana 3:17.
17, 18. (a) Mto unaotokeza uhai unafafanuliwaje kwenye Ufunuo 22:1, 2, na wakati muhimu wa utimizo wa ono hilo ni lini? (b) Ni kwa nini mto huo wa maji ya uhai utaingia kipindi cha mpanuko ulio mkubwa zaidi katika Paradiso?
17 Kwa kweli, ndipo mto ambao Ezekieli aliona utatiririka kwa maji ya uhai yenye nguvu nyingi. Huo ndio wakati muhimu wa utimizo wa unabii uliorekodiwa kwenye Ufunuo 22:1, 2: “Akanionyesha mto wa maji ya uhai, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kuteremka katikati ya njia pana yalo. Na upande huu wa mto na upande ule kulikuwa na miti ya uhai yenye kutokeza mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yayo kila mwezi. Na majani ya hiyo miti yalikuwa ya kuponya mataifa.”
18 Wakati wa Milenia, magonjwa yote—ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo—yataponywa. Hilo laonyeshwa vyema kwa ‘kuponywa kwa mataifa’ kupitia miti hiyo ya ufananisho. Kwa sababu ya maandalizi yatakayotolewa na Kristo pamoja na wale 144,000, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Nao mto huo utaingia kipindi cha mpanuko wake ulio mkubwa zaidi. Utalazimika kupanuka na kuongezeka kina ili kuwatosheleza mamilioni, labda mabilioni, ya wanadamu waliofufuliwa ambao watayanywa maji hayo safi ya uhai. Mto wa kimaono uliponya Bahari ya Chumvi, ukitokeza uhai popote maji yake yalipotiririka kuelekea. Katika Paradiso, wanaume na wanawake watakuja kwenye uhai kwa maana iliyo kamili zaidi, wakiponywa kutokana na kifo cha Kiadamu kilichorithiwa ikiwa watajizoeza imani katika manufaa za fidia watakazopewa. Ufunuo 20:12 hutabiri kwamba “hati-kunjo” zitafunguliwa katika siku hizo, zikiandaa nuru zaidi ya uelewevu ambao utawanufaisha wale watakaofufuliwa. Kwa kuhuzunisha, hata katika Paradiso, watu fulani watakataa kuponywa. Waasi hao ndio wale ‘walioachiwa chumvi’ ya uharibifu wa milele.—Ufunuo 20:15.
19. (a) Kugawanywa kwa nchi kutatimizwaje katika Paradiso? (b) Jiji lafananisha kitu gani kikuu katika Paradiso? (c) Ni nini umuhimu wa jiji kuwa umbali fulani kutoka kwenye hekalu?
19 Pia, wakati huo, kugawanywa kwa nchi katika ono la Ezekieli kutakuwa na utimizo wake wa mwisho. Ezekieli aliona nchi ikigawanywa ifaavyo; vivyo hivyo, kila Mkristo mwaminifu aweza kuwa na uhakika kwamba atakuwa na sehemu, yaani urithi, katika Paradiso. Yaonekana, ile tamaa ya mtu kuwa na nyumba yake mwenyewe ya kuishi na kuitunza itatimizwa kwa utaratibu. (Isaya 65:21; 1 Wakorintho 14:33) Lile jiji ambalo Ezekieli aliona hufananisha kwa kufaa mpango wa usimamizi ambao Yehova akusudia kwa ajili ya dunia mpya. Jamii ya kikuhani ya watiwa-mafuta haitakuwapo kimwili tena miongoni mwa wanadamu. Ono hilo ladokeza hilo kwa kulionyesha jiji likiwa katika nchi “chafu” umbali fulani kutoka kwa hekalu. (Ezekieli 48:15, linganisha NW.) Wale 144,000 watakapokuwa wakitawala na Kristo mbinguni, Mfalme hatakosa waakilishi duniani. Raia zake wa kibinadamu watanufaika kwa njia kubwa kutokana na mwongozo na mwelekezo wenye upendo wa ile jamii ya mkuu. Hata hivyo, kitovu halisi cha serikali kitakuwa, si duniani, bali mbinguni. Kila mtu duniani, kutia ndani jamii ya mkuu, atakuwa katika ujitiisho kwa Ufalme wa Kimesiya.—Danieli 2:44; 7:14, 18, 22.
20, 21. (a) Kwa nini jina la jiji hilo lafaa? (b) Kuelewa kwetu ono la Ezekieli kwapaswa kutufanya tujiulize maswali gani?
20 Ona maneno ya kumalizia ya unabii wa Ezekieli: “Jina la mji huo tangu siku hiyo litakuwa Yehova Mwenyewe Yupo Hapo.” (Ezekieli 48:35, NW) Kusudi la jiji hilo halitakuwa kuwapa wanadamu nguvu au mamlaka; wala kusudi halitakuwa kutekeleza mapenzi ya binadamu yeyote. Hilo ni jiji la Yehova, daima likidhihirisha akili zake na njia zake zenye upendo na zenye kiasi. (Yakobo 3:17) Hilo latupa uhakikisho wenye kuchangamsha moyo kwamba Yehova ataibariki, hadi kufikia wakati ujao udumuo kwa muda usio dhahiri, jamii ya kibinadamu iliyopangwa ya “dunia mpya.”—2 Petro 3:13.
21 Je, hatushangilii juu ya tumaini hilo lililo mbele yetu? Kwa kufaa, basi, kila mmoja wetu atafanya vema kuuliza: ‘Je, mimi naitikiaje baraka nzuri ajabu zinazofunuliwa katika ono la Ezekieli? Je, naunga mkono kwa uaminifu kazi inayofanywa na waangalizi wenye upendo, kutia ndani wale mabaki watiwa-mafuta na wale wanaotazamia kuwa washiriki wa jamii ya mkuu? Je, nimeifanya ibada safi kuwa jambo muhimu kabisa katika maisha yangu? Je, ninatumia kwa ukamili maji ya uhai yanayotiririka kwa wingi sana leo?’ Acheni kila mmoja wetu aendelee kufanya hivyo na kupendezwa na maandalizi ya Yehova kwa umilele wote!
[Maelezo ya Chini]
a Bonde hilo la mvo huenda larejezea Bonde la Kidroni, linaloenea kusini-mashariki mwa Yerusalemu na kuishia kwenye Bahari ya Chumvi. Sehemu ya chini ya bonde hilo ni kavu na yenye ukame mwaka mzima.
b Ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1881 (la Kiingereza), na la Julai 15, 1982.
Wewe Ungejibuje?
◻ Maji yatiririkayo kutoka hekaluni yafananisha nini?
◻ Yehova ametimiza uponyaji upi kupitia mto wa ufananisho, na kwa nini mto huo umepanuka?
◻ Miti iliyo kando-kando ya kingo za mto huo hufananisha nini?
◻ Jiji litafananisha nini wakati wa Utawala wa Milenia, na kwa nini jina la jiji hilo lafaa?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mto wa uhai huwakilisha uandalizi wa Mungu kwa wokovu