Kupenda Wale Ambao ‘Ni Jamaa Katika Imani’
WAKRISTO wa kweli wana muungano ulio kama wa familia miongoni mwao. Naam, tangu karne ya kwanza W.K., wao wameitana “ndugu” na “dada.” (Marko 3:31-35; Filemoni 1, 2) Haya si maneno matupu tu; bali yanafafanua jinsi waabudu wa Mungu wanavyohisi kuelekea wenzao. (Linganisha 1 Yohana 4:7, 8.) Yesu alisema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—Yohana 13:35.
Upendo wa aina hiyo ulidhihirishwa Julai 1997 wakati mvua nyingi yenye mafuriko iliponyesha huko Chile baada ya ukame wa muda mrefu. Kwa ghafula, watu wengi walihitaji chakula, mavazi, na vitu vingine. Wakati wa msiba, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufuata shauri hili la Paulo kwa Wagalatia: “Basi, kwa kweli maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Wagalatia 6:10.
Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova walijiandaa haraka ili kusaidia. Chakula, mavazi, na vitu vingine kama hivyo vilikusanywa, vikapangwa, vikapakiwa, na kusafirishwa kwenye eneo la msiba. Hata watoto walitoa vichezeo! Dada mmoja alishangaa sana alipoona Jumba la Ufalme limejaa misaada. “Nilisimama nimepigwa na butwaa, nisijue nicheke au nilie,” yeye asema. “Misaada hiyo ndiyo tuliyohitaji hasa.”
Kisha, bila kutarajiwa tetemeko la dunia likakumba sehemu fulani ya eneo hilohilo lililokumbwa na mafuriko. Nyumba nyingi zikaharibiwa. Ili kujiandaa kwa ajili ya uhitaji huo, halmashauri zaidi za kutoa misaada zilifanyizwa. Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa, ambazo kwa kawaida hushughulikia ujenzi wa majumba ya kukutania ya Mashahidi wa Yehova, zilijitolea na kusaidia. Matokeo yakawa nini? Wale waliopoteza nyumba zao walijengewa nyumba zenye kiasi ambazo zilibuniwa na kujengwa na akina ndugu. Ingawa nyumba hizi hazikuwa zenye madoido, zilikuwa tofauti kabisa na zile zilizotolewa kwa mkopo na watoaji misaada wa ulimwengu, ambazo hazikuwa na sakafu, madirisha wala rangi.
Ndugu wengine walisafiri kutoka mbali sana ili kuja kusaidia. Mwenyekiti wa Halmashauri moja ya Ujenzi ya Kimkoa alifanya ziara ya ukaguzi kwa siku mbili mfululizo—ijapokuwa alitumia kiti chenye magurudumu. Ndugu mmoja kipofu alifanya kazi kwa bidii, akibeba mihimili kumpelekea seremala aliyeikata kulingana na saizi iliyotakiwa. Ndugu mmoja kiziwi alichukua mihimili hiyo na kuipeleka mahali ilipohitajika.
Watazamaji wengi walivutiwa na msaada uliotolewa na akina ndugu. Katika mji mmoja gari la polisi lilikuwa limeegeshwa karibu na nyumba ya dada iliyokuwa ikirekebishwa. Polisi hao wakataka kujua kilichokuwa kikiendelea. Mmoja wao akauliza ndugu mmoja hivi: “Wafanyakazi hawa wanaoonekana kuwa na furaha hivyo ni nani, nao wanalipwa pesa ngapi?” Ndugu huyo aliwaeleza kwamba hao wote walikuwa wajitoleaji. Mmoja wa maofisa hao akamweleza kwamba alikuwa akitoa sehemu ya kumi kanisani kila mwezi, hata hivyo, pasta wake hakuwa hata amemtembelea tangu tetemeko hilo la dunia litokee! Siku iliyofuata dada huyo alipokea simu kutoka kwa ofisa mmoja wa polisi. Yeye pia alikuwa amewaona wafanyakazi hao. Alisema kwamba alivutiwa sana na shauku na moyo wa bidii wa wafanyakazi hao hivi kwamba karibu ajiunge nao!
Kwa kweli, kazi ya kutoa misaada Chile ilifurahisha wale waliojitolea na kutoa ushuhuda mzuri kwa watazamaji.