Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 6/15 kur. 10-13
  • Je, Yakupasa Kupanua Maoni Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Yakupasa Kupanua Maoni Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pata Kuelewa Mambo Yote
  • Jinsi Unavyowaona Wengine
  • Unapotoa Vitu vya Kimwili
  • Unapotoa Shauri
  • Jitahidi Kupanuka
  • Je, Unawaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Je! Wewe Umepata Kumjua Mungu Kweli Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Shiriki Shangwe ya Kutoa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Usiruhusu Makosa ya Wengine Yakukwaze
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 6/15 kur. 10-13

Je, Yakupasa Kupanua Maoni Yako?

TETEMEKO la dunia lenye kuangamiza lilikumba Kobe City, magharibi mwa Japani, na wajitoleaji wenye kujitoa mhanga wakaja upesi kuwasaidia wakazi walioathiriwa. Hata hivyo, ombi la kikundi cha madaktari wenye kuzuru la kupata vifaa vya tiba lilikataliwa na mtu fulani kwenye Ofisi ya Afya ya jiji hilo. Ofisa huyo, ambaye pia alikuwa mkurugenzi wa hospitali kubwa ya manispaa, alitaka wahasiriwa waende kwenye hospitali za Kobe badala ya kutibiwa kwenye vituo vya kutoa misaada ambako madaktari waliwadunga sindano na kuwatia maji mwilini, shughuli iliyokuwa ghali sana. Hatimaye, ombi la madaktari hao lilikubaliwa, lakini mtazamo mgumu ambao ofisa huyo alionyesha hapo awali na kule kuonekana kuwa bila huruma kulifanya ashutumiwe sana.

Labda wewe umetendewa vivyo hivyo na mtu fulani mwenye mamlaka. Huenda hata wewe umewatendea wengine vivyo hivyo. Je, ungeweza kunufaika kwa kusitawisha maoni yaliyopanuka zaidi?

Pata Kuelewa Mambo Yote

Ni jambo la kawaida kwa watu kutazama mambo kwa upande mmoja tu, hivyo wakipunguza uwezo wao wa kutambua na kuelewa mambo. Hilo mara nyingi husababishwa na mambo kama elimu, mambo yaliyompata mtu maishani, na malezi. Mtu anaweza kufanya maamuzi ya hekima zaidi akijaribu kuelewa mambo yote. Kwa mfano, ikiwa unavuka njia panda, ambapo hapana taa za kuongoza magari, je, lingekuwa jambo la hekima kuangalia mbele tu? La hasha! Vivyo hivyo, kupanua maoni yako ili uelewe mambo yote kwaweza kukusaidia sana ufanye maamuzi na kutenda kwa njia inayofaa. Kufanya hivyo hata kunaweza kuokoa uhai.

Yaelekea kwamba sote twaweza kufanya maendeleo kuhusiana na jambo hilo. Jiulize, ‘Ni katika maeneo yapi naweza kunufaika kwa kupanua maoni yangu?’

Jinsi Unavyowaona Wengine

Je, wewe huona nini unapowatazama wengine? Je, una mwelekeo wa kuona yale wasemayo au wafanyayo kuwa ama mabaya ama mazuri, kana kwamba hakuna maoni tofauti? Je, wewe huyaona maelezo atoayo mtu kuwa ama sifa ama tukano? Je, mtu anakuwa ama ametenda sawa kabisa au amekosea kabisa? Kuwa na maoni kama hayo ni sawa na mpiga-picha ambaye hupuuza rangi mbalimbali zilizo nyangavu katika mandhari wakati wa vuli, kana kwamba rangi nyeusi na nyeupe ndizo zenye kuonekana kwenye mandhari hiyo. Au je, una mwelekeo wa kukazia fikira zile sifa zisizofaa za utu wa mtu, kama vile msafiri anayekosa kufurahia mandhari maridadi sana eti kwa sababu mgeni mwingine asiyejali ameacha takataka kidogo hapo?—Linganisha Mhubiri 7:16.

Kwa kuzingatia maoni ya Yehova kuhusu makosa ya kibinadamu tunaweza kujifunza mengi. Ingawa anafahamu udhaifu na kasoro mbalimbali za mwanadamu, yeye huamua kuyapuuza au kutoyakazia fikira sana. Mtunga-zaburi mwenye shukrani alisema hivi: “Kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Yehova yu tayari kusamehe kabisa makosa ya watenda-dhambi wenye kutubu, naam, akiyafutilia mbali kwa huruma, hivi kwamba hayaharibu uhusiano wetu pamoja naye. (Zaburi 51:1; 103:12) Kumhusu Mfalme Daudi ambaye wakati mmoja alifanya dhambi nzito na Bath-sheba, Yehova angeweza kusema kwamba yeye alikuwa mwanamume “aliyezishika amri zangu, na kunifuata kwa moyo wake wote, asifanye lo lote ila yaliyo mema machoni pangu.” (1 Wafalme 14:8) Kwa nini Mungu angeweza kusema hivyo kumhusu Daudi? Kwa sababu alikazia fikira sifa za Daudi zilizokuwa nzuri zaidi. Alizingatia mambo yote yaliyohusika, akaamua kuendelea kumwonyesha rehema mtumishi wake.

Kristo Yesu alidhihirisha kikamili maoni hayo yaliyopanuka kuelekea kasoro za wengine. (Yohana 5:19) Alipokabiliwa na kasoro za mitume wake, Yesu alionyesha rehema na uelewevu. Yeye alitambua kuhusu wanadamu wasiokamilika kwamba hata wakati ambapo ‘roho ni yenye hamu, mwili ni dhaifu.’ (Mathayo 26:41) Kwa kuzingatia hayo, Yesu angeweza kushughulika na udhaifu na kasoro mbalimbali za mitume wake kwa subira na uelewevu. Yeye hakukazia fikira kasoro zao, bali sifa zao nzuri.

Pindi moja baada ya kuwasahihisha mitume kwa kubishana juu ya ni yupi aliyeonekana kuwa mkubwa zaidi, Yesu aliendelea kusema hivi: “Hata hivyo, nyinyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu amefanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa kwenye meza yangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.” (Luka 22:24-30) Naam, licha ya kasoro nyingi za mitume, Yesu alikumbuka uaminifu na upendo wao kwake. (Mithali 17:17) Yesu alikuwa na uhakika katika yale ambayo walikuwa na uwezo wa kufanya na yale ambayo wangefanya, kwa hiyo akafanya agano pamoja nao kwa ajili ya Ufalme. Naam, ‘Yesu aliwapenda wanafunzi wake hadi mwisho.’—Yohana 13:1.

Kwa hiyo, uwe kama Yehova na Yesu ikiwa tabia au kasoro za utu wa mtu zaelekea kukuudhi. Panua maoni yako, na jaribu kuzingatia mambo yote. Kwa kuona mambo ifaavyo, itakuwa rahisi kwako kuwapenda na kuwathamini ndugu zako.

Unapotoa Vitu vya Kimwili

Pendeleo la kutoa ni mojawapo ya mambo yenye kufurahisha ambayo Wakristo wamepewa. Lakini je, twahitaji tu kufanya jambo moja katika kutoa, kwa mfano, kushiriki katika huduma ya shambani? (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Au maoni yako yaweza kupanuliwa yatie ndani mahitaji ya kimwili na hali njema ya wengine? Bila shaka, Wakristo wote wanafahamu kwamba kutoa kwa njia ya kiroho ni muhimu sana. (Yohana 6:26, 27; Matendo 1:8) Hata hivyo, kama vile kutoa kwa njia ya kiroho ni muhimu, kutoa kwa njia ya kimwili pia kusipuuzwe.— Yakobo 2:15, 16.

Tufikiriapo kwa makini mahitaji muhimu ya ndugu zetu wa kiroho katika kutaniko letu na ulimwenguni pote, twaweza kuelewa kikamili yale tuwezayo kufanya ili kuwasaidia. Usawaziko unakuwepo wakati ambapo wale walio na uwezo zaidi kifedha wanashiriki na wengine kwa ukarimu. Kwa njia hiyo, mahitaji ya ndugu zetu wote yanashughulikiwa. Mzee mmoja Mkristo alieleza jambo hilo hivi: “Kukiwa na uhitaji katika sehemu moja ya ulimwengu, ndugu katika sehemu nyingi ya ulimwengu watasaidia. Ikiwa hawawezi kusaidia, basi ndugu zao mahali pengine watafanya hivyo. Hivyo, mahitaji ya ndugu zetu ulimwenguni pote yanashughulikiwa. Kwa kweli, udugu huu wa ulimwenguni pote ni wa kustaajabisha.”—2 Wakorintho 8:13-15; 1 Petro 2:17.

Dada mmoja Mkristo ambaye alitamani sana kuhudhuria mmojawapo wa mikusanyiko ya kimataifa iliyofanywa Ulaya Mashariki hakuweza kufanya hivyo. Hata hivyo, alisikia kwamba ndugu wa huko walihitaji sana Biblia, kwa hiyo akatoa mchango wa Biblia hizo kupitia mtu fulani aliyehudhuria. Hivyo alifurahia kutoa, kushiriki na ndugu zake katika nchi ya kigeni.—Matendo 20:35.

Labda kwa kuwa na maoni yaliyopanuka unaweza kutoa mchango mkubwa hata zaidi kwa kazi ya ulimwenguni pote ambayo inazidi kupanuka ya kufundisha Biblia, kwa furaha yako na ya wengine vilevile.—Kumbukumbu la Torati 15:7; Mithali 11:24; Wafilipi 4:14-19.

Unapotoa Shauri

Unapohitajika kutoa shauri au sahihisho, kusababu kwa kufikiria wengine na kwa usawaziko kutafanya tustahiwe na ndugu zetu wa kiroho na vilevile kutusaidia kutoa msaada wenye matokeo mazuri. Ni rahisi kukazia fikira mambo machache ya hakika na kwa haraka-haraka kufikia mkataa unaopendelea upande mmoja. Hilo laonyesha kwamba sisi tuna maoni yasiyofikiria upande mwingine, au hata kwamba hatubadili maoni kabisa, kama viongozi wa kidini wa wakati wa Yesu, ambao walikuwa na mwelekeo wa kulemeza wengine kwa kanuni zao nyingi. (Mathayo 23:2-4) Kwa upande mwingine, tukiepuka maoni yenye kupita kiasi na kutoa shauri zuri lenye kutegemea kabisa kanuni za Kimaandiko na kudhihirisha maoni ya Yehova yenye uadilifu na rehema vilevile, itakuwa rahisi zaidi kwa wengine kukubali na kutumia madokezo yetu.

Miaka kadhaa iliyopita, ndugu vijana kutoka makutaniko kadhaa walikutana ili kushiriki katika michezo. Kwa kusikitisha, roho ya mashindano ikasitawi kati yao na kutokeza maneno makali baina yao. Wazee wa kwao walishughulikiaje tatizo hilo? Kwa kutambua uhitaji wa vijana wa kuwa na tafrija, hawakupendekeza waache michezo kabisa. (Waefeso 5:17; 1 Timotheo 4:8) Badala yake, walitoa maonyo thabiti lakini ya busara juu ya kile kiwezacho kusababishwa na roho ya mashindano. Walitoa pia madokezo yafaayo, kama vile kuwa na watu wenye umri mkubwa na wenye kuchukua mambo kwa uzito kwenye michezo hiyo. Vijana hao walithamini hekima na usawaziko wa shauri hilo na kuitikia vizuri. Isitoshe, staha na shauku yao kwa wazee iliongezeka.

Jitahidi Kupanuka

Ingawa huenda usibague kimakusudi au kwa kujua, bado utahitajika kujitahidi kupanua maoni yako. Unapojifunza Neno la Mungu, tafakari juu yake ili uweze kufahamu na kuelewa jinsi Yehova anavyoona mambo. (Zaburi 139:17) Jaribu kuelewa ni kwa nini mambo fulani yametajwa katika Biblia na pia kuelewa kanuni zinazohusika, na kujitahidi kupima mambo jinsi Yehova afanyavyo. Hilo litapatana na sala ya Daudi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha.”—Zaburi 25:4, 5.

Unapopanua maoni yako zaidi, utabarikiwa. Baraka moja ya kuwa na maoni yaliyopanuka itakuwa kusifiwa kwa kuwa mwenye usawaziko na uelewevu. Utaweza kutoa msaada kwa njia ya busara na uelewevu zaidi katika hali mbalimbali. Nalo jambo hilo litachangia muungano na upatano wa kustaajabisha wa udugu wa Kikristo.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kutoa kwa ukarimu husaidia wengine, hufurahisha mwenye kutoa, na humpendeza Baba yetu wa kimbingu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki