Je! Wewe Umepata Kumjua Mungu Kweli Kweli?
“Kwa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile.”—2 Tim. 1:12.
1. Ni hali gani Iliyokuwamo katika Israeli wa kale inayotufanya tujiulize kama twamjua Mungu kweli kweli?
JE! WEWE unamjua Mungu? ‘Eeh, ndiyo,’ wajibu, ‘kila mtu amjua Mungu, sivyo?’ Kwa nje huenda ikaonekana hivyo, lakini miaka 2,700 iliyopita nabii mmoja aliyeitwa Hosea alisema jambo ambalo huenda likatufanya tutue na kujiuliza wenyewe, ‘Je! kweli mimi namjua Mungu?’ Hosea aliishi katika Israeli wakati ambao taifa hilo lilikuwa katika uhusiano wa pekee wa agano na Yehova Mungu. Bila shaka Waisraeli wengi walijua kwamba jina la Mungu Yehova lilimaanisha kwa halisi “Yeye Hufanya Iwe.” Bila shaka walijua namna Mungu alivyokuwa ameshiriki kuleta maendeleo yao ya kitaifa nao walizijua sheria zake hasa. Ijapokuwa kufahamiana huku na Muumba wao nabii Hosea alilazimika kuwaambia hivi: “Lisikieni neno la [Yehova], enyi wana wa Israeli; kwa maana [Yehova] ana mateto nao wakaao katika nchi, kwa sababu hapana kweli, wala fadhili, wala kumjua Mungu katika nchi.”—Hos. 4:1; linganisha Yohana 7:28.
2, 3. (a) Ni mambo gani yanayohusika katika kumjua mtu fulani kweli kweli? (b) Kwa sababu gani ni jambo la maana hasa kumjua Mungu?
2 Kwa hiyo, basi, Waisraeli hawa hawakumjua Mungu kweli kweli. Kwa hiyo, mengi yanahusika katika kumjua mtu kuliko tu kulijua jina lake na pengine kuwa na habari fulani juu ya maisha ya mtu huyo, au mambo ayapendayo na asiyoyapenda.
3 Je! kwa kweli wewe unamjua Mungu kwa kadiri gani? Je! una nia ya kuhatirisha maisha yako kwa sababu ya uyajuayo? Itakupasa ufanye hivyo. Taifa la Israeli lilikataliwa kwa kukosa maarifa, naye Mungu anaona namna ile ile juu ya wale wanaokataa maarifa yake ya kweli. Wakati unakaribia sana ambapo ‘atawalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu.’—2 The. 1:8; Yohana 17:3.
4. Kukosa kumjua Mungu kunaonekanaje wazi?
4 Inaonekana wazi kwamba leo watu wengi wanakataa kumjua Mungu, kama taifa la Israeli lilivyofanya siku za Hosea. Baada ya kuulaumu ukosefu wa maarifa wenye kusikitisha kati ya Waisraeli wenzake, Hosea aliendelea kuonyesha namna ukosefu wao wa maarifa ulivyokuwa wazi. Alisema hivi: “Hapana neno ila kuapa kwa uongo, na kuvunja ahadi, na kuua, na kuiba, na kuzini; huruka mpaka, na damu hugusana na damu.” (Hos. 4:2) Ndiyo, matendo ya mtu yanaonyesha wazi ni kwa kadiri gani amjuavyo Mungu. Mwandikaji wa Kikristo alitoa maelezo juu ya hili aliposema: “Na katika hili twajua ya kuwa tumemjua yeye [yaani, Mungu, kama anavyotajwa katika 1 Yohana 1:5], ikiwa tunashika amri zake. Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake.” (1 Yohana 2:3, 4) Kwa hiyo, ili mtu amjue Mungu mengi zaidi yanahusika kuliko kuwa mwenda kanisani tu anayefuata dini. Ingempasa awe mtiifu kwa mapenzi ya Mungu. Je! wewe wasimama wapi katika habari hii?
5. Ni kwa njia gani maarifa yanavyokuza matumaini kwa Muumba wetu?
5 Maarifa yaliyo sahihi juu ya Mungu yanaonyeshwa kwa kumtumaini yeye kabisa. Mtunga zaburi Daudi asema: “Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, maana Wewe, [Yehova], hukuwaacha wakutafutao.” (Zab. 9:10) Wale walijuao “jina” la Mungu, yaani, hali na sifa yake, hawataamini mambo ya uongo yakisemwa juu ya Baba yao wa kimbinguni. Yeye akifanya au kusema jambo wasilolifahamu vizuri, hawatamdhania amefanya hivyo kwa nia mbaya. Wao wanajua kuna sababu nzuri kwa yote ambayo Yeye anayafanya hata ikiwa hawaifahamu wakati huo. Na ikiwa Yeye anaelekea kukawia kidogo kwako, bila shaka kuna sababu nzuri. Katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wengine waliona hivi, wakimfanya mtume Petro aandike: “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Pet. 3:9) Mungu ni mvumilivu sasa kama alivyokuwa wakati huo, nao watu ni wenye harara sasa kama walivyokuwa wakati huo.
WAZEE, JE! MWAMJUA MUNGU KWELI KWELI?
6. Wazee wanawezaje kuonyesha maoni ya Yehova juu ya kutokamilika?
6 Wazee au waangalizi katika kundi la Kikristo wanaweza kuonyesha ni kwa kadiri gani wanavyomjua Mungu kwa kushughulika na wengine kama ambavyo Mungu angefanya. Kwa mfano, chukua namna ambavyo wazee wanawaona ndugu zao. Je! nia yao yaonyesha maoni ya Yehova? Angalia yaliyoandikwa katika Zaburi: “[Yehova], kama Wewe ungehesabu maovu, Ee [Yehova], nani angesimama?” (Zab. 130:3) Kwa hiyo Muumba hazunguki-zunguki akitafuta makosa, wala yeye si mwenye kulaumu-laumu mno kwa sababu ya makosa madogo madogo. Maelekeo ya kawaida ya maoni ya Yehova juu ya wanadamu yanaonyeshwa zaidi katika Zaburi: “[Yehova] amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Yeye hatateta sikuzote, wala hatashika hasira yake milele. Hakututenda sawasawa na hatia zetu, wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao. Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo [Yehova] anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zab. 103:8-14) Je! shughuli zetu na akina ndugu zinaonyesha kwamba tunayajua mambo haya kweli juu ya Mungu?
7, 8. Maarifa ya wazee yanalifaidije kundi?
7 Ikiwa ndivyo, wazee hawawezi kuwa wasahaulifu juu ya kundi linavyoendelea. Huenda wakayatumia maneno haya juu yao wenyewe kama wachungaji wa kiroho: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako; na kuwaangalia sana ng’ombe zako.” (Mit. 27:23) Lakini je! wazee wanafanya nini na maarifa waliyo nayo juu ya kundi? Kama vile Yehova, wanauona wema katika watu. Wao wanashukuru kwa wema unaofanywa na wengine, na kwa hiyo wanajitahidi kuwajenga wale walio karibu yao. Je! hii haipatani na mfano wa Yehova na mashauri anayotupa katika neno lake? “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia. Tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”—Efe. 4:29, 32; Gal. 5:22, 23; Ebr. 10:24, 25; 1 The. 5:14, 15.
8 Pia, wao wanajua ni akina nani wanaohitaji msaada kundini. Pengine walio wazee zaidi wana magumu yanayohusu utumishi wao kwa Mungu. Pengine wana huzuni na hivyo wanahitaji faraja. Je! wengine wanakosa mikutano au kwa njia nyingine kulegea katika utumishi wao kwa Mungu? Je! wengine wanasafiri peke yao kwenye mikutano na utumishi wa shambani wakipita katika mitaa yenye hatari? Je! vijana wangeweza kutumiwa wasaidie vijana wengine katika utumishi wa shambani na kutayarisha hotuba za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Je! wangeweza kupewa madaraka katika Jumba la Ufalme? Wazee wako macho kuyaona yote yanayoyapata maisha ya kiroho ya akina ndugu nao wanafanya yote wawezayo wawasaidie. Haya ndiyo mambo wanayoyazungumza wanapokutana pamoja.
9. Je! Waisraeli walilikubali onyo la Yehova Juu ya kuwa na mfalme wa kibinadamu, naye Mungu alitendaje kwa sababu ya nia yao?
9 Walakini, namna gani ikiwa mshiriki wa kundi anaanza kuwa na maelekeo ambayo wazee wanaona yataleta ugumu wa kiroho? Je! ni wonyesho wa fadhili kuiachilia hali hiyo? Kushughulika kwa Yehova na Israeli wakati walipoomba wawe na mfalme wa kibinadamu kwaonyesha namna ya kushughulika na hali kama hiyo. Yehova aliwaonya Waisraeli waziwazi juu ya ambayo yangewapata kwa kuwa na mfalme wa kibinadamu; hata hivyo, yeye hakuwakataza walichotaka. Ombi lao lilikuwa kumkataa Yehova, na ingawa waliendelea kuyakataa maonyo yake wakati huu yeye hakuwapa kisogo, bali aliendelea kulisihi taifa mpaka kuharibiwa kwao. Kwa kuwa wanamjua Mungu, wazee wanatenda vivyo hivyo kwa uvumilivu hata kwa wale wanaopuza maonyo. 1 Sam. 8:4-22.
10. Eleza maoni yafaayo ya waangalizi kwa mtu anayekataa maonyo.
10 Mshiriki asiyeoa au kuolewa wa kundi huenda akawa anashirikiana sana na mtu asiyeamini. Wazee watatoa maonyo yafaayo ya Maandiko wakieleza namna Mungu anavyoona, wakionyesha kwamba ni kinyume kabisa cha sheria ya Yehova kuoa au kuolewa na mtu asiyeamini. Hata ikiwa maonyo hayo yanapuzwa, wazee watajaribu kwa upendo kumsaidia mtu huyo maadamu mtu huyo ni sehemu ya kundi la Kikristo. Haiwapasi wazee kuvunjika moyo mashauri yao yakipuzwa, bali wakumbuke kwamba ni daraka lao “kutia moyo . . . na kukaripia wale wanaopinganisha,” na ni kweli pia kwamba mwishowe “kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.”—Tito 1:9, NW; Gal. 6:5.
11. Ni sifa gani ya maana sana ili maonyo yapate kuwa na matokeo mema? Toa mfano.
11 Kwa habari ya kutoa maonyo, jambo la maana lapasa lijulikane kutokana na mfano wa Yehova: Uwe mpole, mwenye busara, sema waziwazi. Hakikisha kwamba anayeshauriwa anaelewa maana. Kwa mfano, hali zinatokea ambapo shauri lazima litolewe kwa watu waliooana. Pengine hawapatani na hivyo wanatafuta msaada wa mzee. Jambo la kwanza awezalo kufanya mtu ni kusikiliza pande zote mbili za kisa chenyewe, mume na mke wakiwapo. Sikuzote Yehova Mungu alilisikiliza taifa la Israeli walipoomba msaada. Mara nyingi mzee ataona kwamba dalili za ugumu tu ndizo anazoelezwa na kwamba penye shina la jambo lenyewe pana jambo linalosababisha zaidi, kama vile maoni yao juu ya ngono. Yawezekana kwamba mke anaongozwa na maoni ya kwamba ngono ni ubaya unaofanywa kwa sababu ni wa lazima tu na hivyo anakataa kufanya ngono na mumewe. Au, kwa upande mwingine, pengine mume haifikirii hali ya moyoni ya mkewe naye anadai ngono kupita kiasi.
12. Mashauri ya Maandiko yanayoonyeshwa wazi yawezaje kutumiwa kusaidia mume na mke wawe na uhusiano uliosawazika zaidi?
12 Ikiwa, sasa, mzee anawaambia tu watu hawa wawili wasali kwa Yehova na kwamba mambo yatakuwa mazuri, huenda wakajisikia hawana nguvu sawa na hapo kwanza. Inawezekana wamesali kwa Mungu naye Yehova sasa anaijibu sala yao kupitia kwa mashauri ya Neno lake Yeye na msaada wa mzee mwenye upendo. Akijua hili, mzee sasa anaweza kuendelea kutoa mashauri ya Maandiko mara ugumu wenyewe unapotolewa nje. Yeye hafanyi haraka haraka bali anakwenda moja kwa moja kwenye Maandiko yanayoshughulika hasa na ugumu wao. Huenda kwanza akaeleza kwamba haimpasi mtu ajisikie ni mchafu kwa sababu anazo nyege, nako kutoshelezwa kwazo ndani ya mpango wa ndoa kunafaa. Bila shaka, kujiweza na kumhurumia mwenzi ni mambo ya lazima kwa maisha yaliyosawazika ya ngono. Haya yote na zaidi yaweza kuonyeshwa kwa kirefu Maandiko yanaposomwa na kuzungumzwa ili kuimarisha maana.—Mwa. 1:28; Mit. 5:15-19; 1 Kor. 7:3-5; 13:4, 5; Gal. 5:22, 23; 1 Pet. 3:7.
13. Je! Mzee avunjika moyo mashauri aliyoyatoa kwa maandiko yasipofuatwa, na kwa sababu gani?
13 Kama mume na mke wanataka kufuata mashauri ya Maandiko katika maisha yao ya ngono au katika neno jingine lo lote ni juu yao; hata hivyo mzee aweza kufurahi kwamba kwa msaada wa Yehova ameweza kutoa uongozi ufaao na kuonyesha kwamba yeye ‘amjua’ Mungu kweli kweli. Bila shaka, haiwapasi wazee wajaribu kuamuru watu wafanye mambo, bali wanapotoa mashauri imewapasa waeleweke vizuri wanapozieleza kanuni za Maandiko zinazohusika.
14. Ni tendo gani la Yehova Mungu kwa habari ya Mfalme Ahabu linaloonyesha ubora wa kuwasikiliza wengine?
14 Kuna njia nyingi ambavyo wazee wanaweza kuonyesha kwamba wanayo maarifa ya kweli juu ya Mungu, nayo hiyo ni kwa namna wanavyosikiliza maoni yanayotolewa na washiriki wa kundi. Kwa kweli Yehova Mungu anajua sikuzote namna ya kushughulika na hali yo yote naye sikuzote anatatua mambo. Lakini, alipokuwa akishughulika na Mfalme Ahabu asiyeaminika wa Israeli, Yehova aliwaruhusu malaika zake watoe maoni yao juu ya watakavyomtendea Ahabu. Kwa kweli Mungu wa ulimwengu wote hakuhitaji mashauri ya malaika zake, lakini alisikiliza. Nyakati nyingine Mungu aliwasikiliza wanadamu. Hakuna njia iliyo bora kwa mzee kupata maoni ya kundi kuliko kusikiliza wengine wasemavyo na kuyafikiria. Hii itamfanya mzee anayesikiliza awe mwalimu mwenye matokeo mazuri zaidi.—1 Fal. 22:19-22; Mwa. 18:22-33; Mit. 21:13.
YAWAPASA WOTE KUNDINI WAMJUE MUNGU
15. Kwa sababu gani kuona mashaka kwafaa kuepukwe kati ya Wakristo, nako kwaweza kuepukwaje?
15 Tunapouona mwisho wa hii taratibu ukikaribia, itawapasa wote watakaovumilia wamjue Mungu. Tusipofahamu namna yeye anavyoshughulika nasi, twaweza kunaswa kwa vyepesi katika mtego wa kuona mashaka, kama vile ambavyo Wakristo wengine walio wakf na kubatizwa wamefanya. Kuona mashaka kwa kawaida hakuhusu kweli za msingi za Biblia kama vile (1) enzi kuu ya Yehova, (2) Ufalme au (3) ukombozi. Bali, huenda tukahangaikia jambo fulani lililo dogo, na kwa sababu ya kiburi tunayatanguliza maoni yetu wenyewe mbele ya Neno la Mungu na tengenezo la Yehova. Ndugu wa mama-mzazi mmoja na Yesu alituonya juu ya kuona mashaka: “Mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa [Yehova]. Mtu wa nia mbili husitasita katika njia zake zote.” (Yak. 1:6-8) Kujua namna Mungu alivyoshughulika na watu wake zamani na sasa kutatusaidia tuepuke kuona mashaka.
16, 17. Je! Mungu ametumia wanadamu wasiokamilika waliongoze tengenezo lake zamani? Toa mifano.
16 Wale wamjuao Mungu watakumbuka namna Mungu ametumia wanadamu wasiokamilika katika vyeo vyenye madaraka mazito ili watu wake waendelee kuwa waliotengenezwa. Kwa mfano, alikuwako Musa, ambaye kutokamilika kwake kulimpotezea haki yake ya kuingia katika Nchi ya Ahadi. Lakini, Mungu aliendelea kumtumia yeye. Walipokuwa ukingoni mwa Kanaani wakati Musa aliporudia kuitaja na kuieleza sheria ya Mungu kwa taifa la Israeli, ingalikuwa vyepesi kwa Waisraeli kuwaza hivi: ‘Wewe ni nani Musa, hata utupe mashauri? Ala! wewe hata hustahili kuiingia Nchi ya Ahadi.’ Ingalikuwa vyepesi kama nini kumlaumu mtu huyo, kuliko kujifaidi na mashauri yaliyoongozwa na Mungu!—Hes. 20:2-12.
17 Kutumia kwa Mungu wanadamu wasiokamilika kuliendelea kundi la Kikristo lilipoanzishwa. Mfikirie mtume Petro. Siku ya kufa kwa Yesu, Petro alimkana Yesu mara tatu. Hilo lilikuwa kosa zito. Walakini, inapendeza kuangalia kwamba siku 52 tu baadaye Petro alipata kuwa mshiriki wa baraza yenye kuongoza iliyotiwa mafuta ya kundi la Kikristo lililoanzishwa karibuni. Yeye alitumiwa sana siku hiyo ya Pentekoste kama mnenaji kwa ajili ya mitume atoe hotuba yenye kusisimua. Ajapokuwa asiyekamilika, siku hiyo Petro alionyesha kwamba alimjua Mungu sana naye alilifahamu Neno lake sana, kama inavyoonyeshwa na mitajo aliyotumia ya Maandiko ya Kiebrania.—Luka 22:54-62; Matendo 2:1-47.
18. Je! Mkristo aweza kujipa udhuru kwa kukataa mashauri ya waangalizi kundini kwa sababu wao ni wasiokamilika, na kwa sababu gani?
18 Ndivyo ilivyo na leo katika kundi la Kikristo. Wanaume wasiokamilika wamjuao Mungu wanatumiwa waongoze. Pengine mzee katika kundi lako atakupa shauri juu ya nia yako. Je! utalidharau shauri jema la Maandiko atakalokupa na kuwa na maoni haya: ‘Wewe ni nani hata uniambie la kufanya? Wewe hujakamilika kabisa.’ Au, badala yake utaonyesha kwamba ‘wamjua’ Mungu, kwamba unajua yeye anatumia wanadamu wasiokamilika watoe mashauri, watengeneze na kuwaongoza watu wake duniani? Kwa kweli, ikiwa Yehova anaridhika na kufanya kazi pamoja na wanadamu wasiokamilika, sisi ni akina nani hata tuulaumu mpango huu? Jambo la maana ni kwamba imetupasa tujifaidi na mashauri ya Maandiko yanayotolewa.
19. Ni njia gani ya kutenda tusikiapo maneno mabaya yakisemwa juu ya ndugu katika kundi la Kikristo?
19 Kwa upande mwingine, pengine unasikia jambo fulani juu ya mmoja wa ndugu zako linaloelekea kuonyesha ubaya wake. Je! unapendezwa na kuyasikia mambo hayo na mara hiyo kuyaamini? Pengine ndugu huyo ni mzee kundini. Je! sasa unaanza si kumwonea mashaka tu ndugu huyo, bali pengine kuanza kuona mashaka mazito juu ya baraza yote ya wazee? Mtu amjuaye Yehova atatenda kwa haraka kuyaondolea mbali mashaka hayo. Atajiuliza hivi: ‘Je! nina mambo yote ya hakika kweli, au ni uvumi tu? Hainipasi nimhukumu ndugu yangu kwa sababu ya maneno ya Paulo: “Wewe u nani unayemhukumu mtumishi wa mwingine? Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka.”’—Rum. 14:4.
20. Ni kukumbuka mambo gani kutakakotusaidia sikuzote tupatane na ndugu na dada zetu wa Kikristo?
20 Pengine hukubaliani na namna mambo yamefanywa kurekebisha au kujenga Jumba la Ufalme. Pengine unajisikia ingalikuwa wewe ungalichagua mtindo tofauti, namna nyingine ya mkeka au rangi tofauti ya vitambaa. Lakini je! mitindo si mingi iwezayo kutumiwa, namna nyingine za mikeka na rangi nyingi za vitambaa? Je! mapambo tofauti ya ndani yataugeuza uhusiano wetu na Yehova? Kwa sababu gani usilifuate shauri la Paulo: “Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi, kusudi mpate kuwa wasio na mawaa msiwakwaze wengine mpaka siku ya Kristo”? (Flp. 1:10, NW) Je! tusimshukuru Yehova kwamba ametoa wanaume waongoze na kuhakikisha kwamba tuna mahali pa kukutania kwa ibada safi?
21. Kwa sababu gani mtu mwenye maarifa ya kweli juu ya Mungu haoni mashaka anapopokea rekebisho juu ya ufahamu wake wa shauri la Maandiko?
21 Pengine jambo fulani lasemwa katika kimojawapo cha vitabu vya Watch Tower usilolielewa au linalorekebisha ufahamu tuliokuwa nao siku zilizopita juu ya mambo. Je! wewe walionaje hili? Je! unaacha mashaka yapenye? Je! badala ya shuku utakuwa na matumaini? Jiulize hivi: ‘Niliyapata wapi maarifa ya Maandiko niliyo nayo? Je! chakula cha kiroho kinachotolewa kupitia kwa vitabu vya Watch Tower hakikunisaidia nibadili maisha yangu na kupata uradhi? Nitakwenda wapi pengine?’ Haya ndiyo maono waliyokuwa nayo wanafunzi juu ya Yesu kwa habari mipango ya Yehova: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:68.
22. Maarifa yaliyo sahihi juu ya Mungu katika hizi “siku za mwisho” yatatufaidije kila mmoja wetu?
22 Leo ni kweli juu ya mamilioni ya watu kwamba: “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana; ni wenye machukizo, waasi, wala kwa kila tendo jema hawafai.” (Tito 1:16) Mashaka, shuku, wasiwasi zote ni dalili za kizazi kisichomjua Mungu. Tofauti na hivyo, Wakristo wanajisikia kama mtume Paulo: “Kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile.” (2 Tim. 1:12) Wale wamjuao Mungu kweli kweli ni wenye matumaini, ni wenye imara na ujasiri katika hizi siku zenye maana sana.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Je! kweli kanisa lako limekusaidia ujifunze mapenzi ya Mungu? Je! kweli wewe unapatanisha maisha yako na matakwa ya Mungu yanayoonyeshwa katika Biblia?