“Wakumbukeni Wale Wanaoongoza Kati Yenu”
“Wakumbukeni wale wanaoongoza kati yenu, ambao wamewaambia neno la Mungu, nanyi mnapotazama sana namna mwenendo wao utakavyokuwa iigeni imani yao.”—WAEBRANIA 13:7, NW.
1. Ni mabadiliko gani yaliyotokea kuhusu ibada ya kweli katika miaka ya mwisho-mwisho ya karne ya 19, lakini wazee Wakristo walichaguliwa namna gani?
KATIKA robo ya mwisho ya karne ya 19 ibada ya kweli ilianza kurudishwa kupitia kikundi kidogo cha wanafunzi wa Biblia waliojitoa kwa bidii wakishirikiana na Charles Taze Russell katika Pittsburgh, Pennsylvania. Kwanza walijaribu kurudisha mafundisho ya kweli ya Biblia, yawe safi bila kutiwa uchafu na mapokeo na falsafa ya Kibabuloni. Lakini, mwendo wa kwanza wa kurudishwa kwa mambo ya tengenezo la kundi ulikuwa wa polepole zaidi. Ingawa Wanafunzi wa Biblia walikuwa na wazee na mashemasi (watumishi wa huduma), bado mawazo ya uongo ya kidini yalidumu katika pande fulani-fulani. Hivyo kuingia moja kwa moja mpaka karne ya 20 wazee walichaguliwa na makundi kwa kufuata utaratibu wa kidemokrasi wa kupiga kura za kuinua mikono juu.
2. Hata hivyo, ni kiwango gani cha hali ya juu walichowekewa wazee kati ya watu wa Yehova?
2 Hata hivyo, kiwango cha hali ya juu kilidaiwa kitimizwe, kwa maana gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Novemba 1, 1909, lilisema hivi katika ukurasa wa 325: “Katika kuchagua Wazee, wale waliotakaswa wanapaswa kukumbuka kwamba daraka hilo linawakalia wao; na hakuna kura inayopasa kutupwa bila kuyachunguza kwa makini sana mapenzi ya Kimungu, na kutoa sala ya kuomba uongozi wa Kimungu.” Makala hiyo iliendelea kukazia tabia tatu za mzee mwema: (1) Alipaswa kuwa stadi wa kufundisha; (2) alipaswa kufundisha kweli wala si makosa; na (3) unyenyekevu na utawa wa kumcha Mungu zilikuwa ndizo “sifa kuu zaidi na za msingi za kufanya mtu apate uzee.”
Utaratibu wa Kitheokrasi Unarudishwa
3, 4. Ni mabadiliko gani makubwa yaliyotokea kuhusu kuwekwa kwa watu wachukue madaraka ya kundi katika (a) mwaka wa 1919? (b) mwaka wa 1932? (c) mwaka wa 1938? na (d) mwaka wa 1971?
3 Katika mwaka wa 1919 hatua ya kwanza ilichukuliwa ili kurudisha uongozi wa kitheokrasi katika kuweka watu kwenye vyeo. Makundi yalikaribishwa kupendekeza ndugu mwenye juhudi awe “mkurugenzi” wa utumishi, aongoze katika kuhubiri. Yeye hangepaswa kuchaguliwa na washiriki wa eneo lake kila mwaka bali angewekwa moja kwa moja na Sosaiti, Sosaiti hiyo iliyoandikishwa kisheria ikiwa ndiyo yenye kuliwakilisha kundi la wapakwa mafuta. Halafu mwaka wa 1932 wazee wa kuchaguliwa waliokuwa wamepaswa kufanya ushirikiano na “mkurugenzi” wa utumishi walibadilishwa na nafasi yao ikachukuliwa na halmashauri ya utumishi ya ndugu waliokomaa, wakajaza vyeo mbalimbali vya utumishi katika kundi lakini bado wakawa wanachaguliwa kupitia kura ya kundi. Neno “mzee” liliondolewa kisha maneno “mtumishi wa kampuni,” “mtumishi wa mafunzo ya Biblia,” na hivyo hivyo, yakawekwa mahali palo.
4 Kikomo kamili cha uchaguzi uliokuwa ukifanywa kilifika mwaka wa 1938. Wakati huo ilionyeshwa kwamba mamlaka ya kuweka watu kwenye vyeo ilikuwa ya Baraza Linaloongoza la kundi la Kikristo la ulimwenguni pote. Tangu wakati huo na kuendelea mbele, wanaume wenye kustahili waliwekwa moja kwa moja na Sosaiti wakawa “watumishi” wa kuangalia wajibu mbalimbali katika kundi. Lakini, katika matoleo ya Machi 15 na Mei 1,1972 ya Mnara wa Mlinzi, ufahamu ulio wazi zaidi wa madaraka ya wazee na waangalizi ulielezwa. Sababu halali zilitolewa juu ya kurudishwa kwa maneno yenye kusema mwanamume mzee, au mzee (presbýteros), na mwangalizi (epískopos).
5. (a) Kwa sababu gani ni lazima uangalifu wa pekee ufanywe katika kupendekeza wazee? (b) Ni mambo gani yanayopasa kukumbukwa?
5 Kwa mara nyingine tena vile viwango vya hali ya juu vilivyowekwa na roho takatifu na kutajwa katika Neno la Mungu vilitiliwa mkazo. Kwa sababu gani? Kwa sababu ili mzee astahili kupewa heshima ni lazima ‘awe anaongoza’ katika mwenendo na huduma ya Kikristo kabla ya kupendekezwa na kuwekwa kwake. (Waebrania 13:7, 17, NW) Basi, mabaraza ya wazee hayapaswi kufanya haraka-haraka ya kufanya mapendekezo ya wazee wapya.(1 Timotheo 3:6; 5:22) Kumbuka kwamba mara nyingi inakuwa kwamba, wakati mwingi zaidi unatumiwa na mazungumzo mengi yanafanywa katika kuondoa mzee asiyestahili kuliko vile inavyokuwa katika kupendekeza awekwe. Kwa kweli, mwongozo wa ziada unaopasa kufuatwa ni kuona kama kundi tayari linamchukua ndugu huyo kama kwamba ni mzee kabla ya kuwekwa kwake. Je! yeye amejipatia heshima yao kwa kutimiza matakwa ya Biblia hivi kwamba hakuna shaka juu ya pendekezo lake?
“Mwenye Kusimamia Nyumba Yake Mwenyewe Katika Adabu Nzuri”
6. Ni nini nyingine za sifa zinazostahilisha mzee kuhusiana na jamaa yake?
6 Acha turudie kujikumbusha kwa ufupi nyingine za sifa zinazopasa kutimizwa na mzee kama zinavyotajwa na mtume Paulo, halafu na tuone zina maana gani leo katika matumizi. Paulo aliandika hivi:
“Ikiwa kuna mwanamume ye yote asiye na shtaka, mume wa mke mmoja, mwenye watoto wanaoamini ambao hawakushtakiwa kuwa na ufisadi wala utundu.”—Tito 1:6, NW.
“Kwa hiyo imempasa mwangalizi awe . . . mwanamume mwenye kusimamia nyumba yake mwenyewe katika adabu nzuri, mwenye kutiisha watoto kwa uzito wote; (ikiwa kweli mwanamume ye yote hajui jinsi ya kusimamia nyumba yake mwenyewe, yeye ataliangaliaje kundi la Mungu?).”—1 Timotheo 3:2, 4, 5, NW.
7. Ni usawaziko gani unaopasa kutunzwa kwa uangalifu mwingi sana kati ya daraka la mzee kwa jamaa yake na kwa kundi?
7 Takwa la kuangalia jamaa ya mtu linatokeza mwito wa ushindani kwa wazee wengi. Mzee anaweza kuongozaje katika kundi na bado asikose kujali mahitaji ya kiroho na ya moyoni ya mke wake na watoto? Si jambo jepesi. Kwa uhakika, ukomavu wa kiroho unatakwa ili kuendeleza usawaziko mzuri kati ya madaraka hayo. Nyakati nyingine washiriki wa kundi wanahitaji wakati na fikira ambazo mzee kwa haki anapaswa kuelekeza kwa jamaa yake. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana ahangaikie jamaa yake? Kwa sababu akikosa kujali uhusiano wa namna mbalimbali alio nao na watu wa jamaa yake au watoto wadogo wanaomtegemea yeye wakigeuka wawe wasiotii mambo ya kiroho, hapo yeye hastahili tena kuwa mzee hata kama ana majaliwa mangapi na juhudi nyingi. Basi, inatupasa tukumbuke kwamba uchungaji unaanzia nyumbani! Ndiyo, ni lazima usawaziko uliopangwa kwa uangalifu udhihirishwe wazi, na mzee mwenyewe na jamaa yake, na pia na kundi wakati linapofanya madai ya mahitaji linalopasa kutimiziwa.—Waefeso 5:28-33; 6:4; 1 Timotheo 5:8; 1 Petro 3:7.
‘Si Mwenye Kutaka Yake Bali Mwepesi Kukubali Maoni ya Wengine’
8, 9. Ni sifa gani ambazo mzee anapaswa kudhihirisha wazi katika uhusiano wake na wengine?
8 Mfululizo mwingine wa matakwa unahusu sana namna mzee anavyotendea wazee wenzake na kundi kwa ujumla. Ni kama vile Paulo anavyoeleza jambo hilo katika barua alizowaandikia Tito na Timotheo:
“Kwa maana yampasa mwangalizi awe bila shtaka kama mtumishi wa nyumba ya Mungu, si mwenye kutaka yake, si mwenye kuhamaki, . . . si mpigaji, . . . mwenye kujiweza.”—Tito 1:7, 8, NW.
“Si mpigaji, bali mwepesi kukubali maoni ya wengine, si mtaka vita.”—1 Timotheo 3:3, NW.
9 Matakwa hayo yanaonyesha kwamba ni lazima mzee awe kama Kristo katika utu wake. Hakika hicho ni kiwango cha hali ya juu. Lakini kiwango hicho kinabaki ivyo hivyo kwa kila Mkristo! Ni lazima sisi sote tuwe waigaji wa Kristo, na hiyo maana yake ni kwamba lazima tuwe watu wenye kuamanika (kutafuta amani). (1 Wakorintho 11:1) Ni kama vile Yakobo mwandikaji wa Biblia alivyoeleza jambo hilo: “Hekima ya kutoka juu kwanza ni safi kwa tabia, halafu inaamanika, ni nyepesi kukubali maoni ya wengine, tayari kutii, imejawa na rehema na matunda mema . . . Zaidi ya hilo, tunda la uadilifu linapandwa mbegu yalo chini ya hali zenye amani kwa ajili ya wale ambao wanafanya amani.”—Yakobo 3:17, 18, NW.
10, 11. (a) Nia ya mzee ingeweza kulihusu kundi kwa njia gani? (b) Hata wakati kunapokuwako visa vya kutofautiana maoni, ni nia gani zinazopasa kudumishwa?
10 Je! sisi tulio wazee ‘tunafanya amani’? Hakuna mzee ambaye angetaka kutokeza ugomvi na ushindani. Baraza la wazee linapasa kuweka mfano mwema katika jambo hilo. Hivyo kundi halitaudhika kwa sababu ya mabishano kati ya wazee. Acheni sisi sote tuyakumbuke maneno ya Paulo: “Mimi nataka kwamba katika kila mahali wanaume ndio waendeleze sala, wakiinua mikono yenye ushikamanifu, bila ghadhabu na majadiliano.”—1 Timotheo 2:8, NW.
11 Mara kwa mara, kutakuwako hali za kutofautiana maoni. Hata kama ana utu wa umashuhuri, mwanamume aliye mwepesi kukubali maoni ya wengine hatakuwa mtu wa kujitakia yake wala hatakuwa na shingo ngumu. Atakuwa na nia ya kufuata maoni ya wengine wakati kanuni za Kimaandiko hazihusiki. Na wakati zinapohusika yeye ataiona hekima ya kudumisha hali ya kujiweza. Ataikumbuka kanuni inayotajwa kwenye 1 Wakorintho 13:4, 5 kwamba upendo “hauoni uchungu.”—Wakolosai 3:12-14.
‘Kushikamana kwa Imara na Neno la Uaminifu’
12. Ni takwa gani jingine linalokaziwa na Paulo?
12 Ni jambo gani litakalosaidia mzee aendelee kukuza zaidi sifa zilizo za maana sana? Na kwa kweli, katika visa fulani tunaweza kufanya nini tubaki tukiwa na sifa hizo? Maneno ya Paulo yanatutolea jibu:
“Mwenye kushikamana kwa imara na neno la uaminifu kwa habari ya ustadi wake wa kufundisha, apate kuweza kutia moyo kwa fundisho ambalo ni lenye afya na kukaripia wale wanaopinga.”—Tito 1:9, NW.
“Mwenye kustahili kufundisha.”—1 Timotheo 3:2, NW.
13. Ni kwa njia gani inampasa mzee aangalie kwa njia ya pekee afya yake ya kiroho?
13 Mzee anaweza kufanya nini ili ‘ashikamane kwa imara na neno la uaminifu’ na awe “mwenye kustahili kufundisha”? Kwanza, ni lazima aweke kando wakati wa kujifunza Biblia kibinafsi kwa ukawaida. Hiyo inatia ndani kujitayarishia mikutano ya Kikristo na migawo ya kuhutubu. Kwa ajili ya afya yake mwenyewe ya kiroho, asifanye matayarisho hayo kijuu-juu tu. Kwa mfano, huenda yeye akawa anaweza kupiga mistari chini ya majibu ya makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi kwa muda mfupi, lakini je! hiyo inamaanisha kwamba amejifunza habari hizo? Je! anaelewa kabisa kabisa namna kichwa cha habari hizo kimeendelea kukuzwa hatua kwa hatua? Je! ameangalia maandiko ya Biblia ambayo maneno yake hayakuandikwa katika fungu ili aamue yatatumikaje? Ni wazi kwamba haiwezekani kufanya hivyo akichora-chora mistari chini ya majibu kwa muda mfupi. Funzo la kibinafsi na la jamaa litahitaji wakati utumiwe.—Yoshua 1:8; Zaburi 1:2; 77:6, 12.
14. Mzee anaweza kufanya nini ili aangalie ustadi wake wa kufundisha?
14 Pili, kwa kuwa orodha yenye shughuli nyingi haimpi mzee wakati wa kufanya kila jambo, ni lazima yeye avichunguze kwa njia ya pekee vichapo na makala za Kikristo zinazohusiana moja kwa moja na ‘ustadi wake wa kufundisha, kutia moyo na kutoa karipio.’ Msaada ambao si mzigo mzito katika kufanya hivyo ni kuwa na maktaba ya kibinafsi iliyopangwa kwa njia safi na ya kupendeza. Inampasa hasa mzee aweze kutafuta upesi habari sahihi za Kimaandiko, na basi anahitajiwa kuzitumia kwa ukawaida fahirisi (index) za vichapo vya Sosaiti. Kwa sababu gani kazi yote hiyo ni ya maana? Mtume Paulo aliandika hivi: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.”—1 Timotheo 4:16.
15. Kwa sababu gani shauri lisilopatana na Maandiko ni hatari?
15 Ndiyo, uhai na wokovu wa watu unaweza kuhusika katika mashauri ya mzee. Kwa mfano, katika mambo yanayohusu kutoa mimba, utiaji wa damu mishipani na kutokuwamo kwa Kikristo, mzee anaweza kuleta matokeo mazito yenye kufaidi au kuumiza dhamiri yake mwenyewe na ile ya wengine, na pia uhusiano wa watu na Yehova. Basi, tunaweza kuona si jambo la hekima kujaribu kujibu maulizo wakati tusipokuwa na uhakika kabisa juu ya kanuni za Biblia zinazohusika. Shauri lisilo na msingi unaofaa wa Kimaandiko linaweza kuleta madhara yasiyoweza kurekebishwa.—Wafilipi 1:9, 10.
16. Kwa sababu gani wazee wengine wametumbukia katika dhambi nzito, na je! hilo ni jambo la kuchukuliwa hivi hivi tu?
16 Sababu nyingine ya kujiangalia mwenyewe ukiwa mzee ni uhitaji wa kusitawisha na kudumisha uhusiano wa kindani pamoja na Yehova. Jambo la kusikitisha ni kwamba wazee wengine wamekosa kujali uhusiano huo mpaka wakafikia hatua ya kutumbukia katika dhambi kama uzinzi. Jambo hilo lingewezekanaje? Ni kwa sababu tu wameacha Yehova na ahadi zake zififie. Maono yao ya kiroho yametiwa utusitusi, kisha tamaa za mwili za kichoyo zimechukua nafasi ya pengo hilo lililoachwa. Kwa sababu ya wazee fulani kuwa baridi wasijali suto linaloweza kuletwa juu ya jina takatifu la Yehova na pia kutokujali maumivu watakayoletea wapendwa wao, wachache kati yao wamekosa ushikamanifu kwa nadhiri zao za ndoa. Kwa uhakika, wanaume wa namna hiyo wamekuwa vikwazo. Dhambi yao haiwezi kufanyiwa visababu-visababu wala kuondolewa fikirani kama jambo lisilo kubwa sana, ati kwa sababu tu sisi tunaishi katika kizazi chenye wendekevu wa mambo ya ngono.—Mathayo 13:41; 18:7-9; Waebrania 13:4.
Wazee Waaminifu na Wake Zao
17. Walio wengi kati ya wazee wanaweka mfano gani mwema?
17 Kwa upande mwingine, ni lazima pia isemwe kwamba wazee ulimwenguni pote, isipokuwa wachache, wamefuata ukamilifu na kweli kwa imara. Mfano mwema wao katika makundi zaidi ya 45,000 ni chanzo cha kuwatia moyo watu wa Mungu. Katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” waangalizi wenye bidii wamekuwa wenye shughuli nyingi mchana na usiku, kama mtume Paulo. (2 Timotheo 3:1, NW; Matendo 20:31) Wazee hao wana nia ya kutembelea mgonjwa wa kiroho nyumbani kwake, bila kujali mambo kama umbali au hali ya hewa. Tena ni vizuri kama nini kuwaona ‘wanaume wazee’ hao wakiongoza katika utumishi wa shambani kwa ukawaida!
18. Ni daraka gani jema linalotimizwa na wake za wazee kundini?
18 Pia tunathamini kwa njia kubwa namna wake za wazee wanavyolazimika kujinyima mambo nyakati nyingine! Nyakati fulani, wanawake wa namna hiyo wanaachwa nyumbani huku waume zao wakihudhuria mikutano ya pekee au wakifanya ziara za uchungaji. Nyakati nyingine mipango iliyokuwa imefanywa kwa uangalifu imewekwa kando kwa sababu ya tatizo fulani la haraka lililotokea katika kundi. Ndiyo, sisi tunawasifu pia dada hao walio wema wanaofanya busara wasijaribu kuuliza-uliza waume zao maulizo ya mambo ya siri ili wawaambie. Wao wanawaonyesha wazee heshima nao ni msaada mkubwa kwenye kundi.—Linganisha Warumi 16:12; Tito 2:3-5.
19. (a) Kuwa mzee kuna maana gani? (b) Wanaume walio wakf ambao si wazee wanaweza kujiuliza ulizo gani?
19 Tunaporudia kujikumbusha daraka la wazee katika kundi la Kikristo leo na kuona namna walio wengi kati yao wanavyoongoza kwa njia nzuri, mioyo yetu inafunguka kumtolea Yehova shukrani kwa sababu aliuanzisha mpango huu wenye upendo. Lo! hao ni wanaume hodari katika kazi, wanaothamini mambo ya kiroho na kujitolea wafanye utumishi kundini! Hiyo ndiyo sababu Paulo angeweza kumwambia Timotheo hivi: “Ikiwa mwanamume ye yote anafikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.” Hiyo “kazi nzuri” haimaanishi cheo, mamlaka na heshima kubwa, kama ilivyo katika Jumuiya ya Wakristo. Inahitaji mtu afanye utumishi wa kutokujifikiria mwenyewe na wa kujinyima. Ikiwa wewe ni mwanamume uliye wakf na uliyebatizwa, je! wewe una nia ya kujinyosha ukafikie daraka hilo ukiwa na kusudi safi?—1 Timotheo 3:1, NW; Luka 17:10.
20, 21. (a) Inatupasa tuwaoneje wazee waaminifu kundini? (b) Kwa kufanya hivyo, tunadhihirisha wazi Jambo gani jingine?
20 Wale wanaoongoza kwa uaminifu wanaheshimiwa katika kundi. Washikamanifu walio katika kundi wanauitikia kwa nia mfano wao wenye upendo na kufuata shauri la Paulo: “Wakumbukeni wale wanaoongoza kati yenu, ambao wamewaambia neno la Mungu, nanyi mnapotazama sana namna mwenendo wao utakavyokuwa iigeni imani yao. Iweni wenye kutii wale wanaoongoza kati yenu na kuwa wenye kunyenyekea, maana wanalinda nafsi zenu kama wale watakaotoa sababu; kwamba wapate kufanya hivyo kwa furaha na si kwa kusikitika, maana hilo lingekuwa lenye kuleta hasara kwenu ninyi.”—Waebrania 13:7, 17, NW.
21 Acheni sisi sote tuonyeshe unyenyekevu kwa mpango wa kitheokrasi na kuwaheshimu wazee wanaoongoza kikweli, ili waweze kufanya hivyo kwa furaha wala si kwa kupumua kwa maumivu. Tukifanya hivyo, tunaonyesha kwamba sisi tunamheshimu pia yule Mwangalizi Mkubwa wa Wote, Yehova, na yule aliye Mwangalizi Makamu wake, Yesu Kristo.—1 Petro 2:25; Ufunuo 1:1; 2:1-3:22.—Kutoka W9/1/83.
Wewe Unakumbuka?
◻ Ni kiwango gani cha hali ya juu kilichopasa kufikiwa na “wazee wa kuchaguliwa”?
◻ Kuanzia mwaka wa 1919 na wa 1938, ni hatua gani zilizochukuliwa ili kurudisha utaratibu wa kitheokrasi ndani ya tengenezo la Kikristo?
◻ Ili mzee atimize madaraka yake kwa jamaa yake na kundi, ni lazima adumishe usawaziko gani?
◻ Inawapasa wazee wadhihirishe wazi sifa gani za kutokeza katika uhusiano wao na wengine?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la maana sana mzee ‘ashikamane kwa imara na neno la uaminifu’?
◻ Kwa sababu gani inatupasa tushukuru kwa ajili ya mpango wa wazee ulio katika kundi?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Mzee anatumia wakati kwa hekima pamoja na jamaa yake na katika huduma ya shambani
[Picha katika ukurasa wa 16]
Yeye anapanga pia wakati wa kufurahia tafrija inayofaa pamoja na wapendwa wake