Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
“Tukinena kweli, acheni kwa upendo tukue katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo.”—Efe. 4:15, NW.
1. Maandiko yanaelezaje habari ya kundi la Kikristo na waangalizi wake?
TUNAPOKARIBIA “dhiki kubwa,” tunazidi kulithamini kundi la Kikristo. Mtume Paulo alilieleza kundi hili la Mungu aliye hai kama “nguzo na msingi wa kweli.” Alisema pia juu ya “nguzo” akimaanisha waangalizi fulani wa kundi waliowekwa na roho takatifu ‘walichunge kundi la Mungu.’ Vivyo hivyo, katika kundi la Kikristo leo, waangalizi huwekwa kitheokrasi walijenge katika upendo.—1 Tim. 3:15; Gal. 2:9; Matendo 20:28.
2, 3. (a) Kristo alilipa kundi “zawadi” gani, na kwa kusudi gani? (b) Yawapasa waangalizi wajaribu kufuata mfano gani mwema?
2 “Na [Kristo] aliwapa wengine kama mitume, wengine kama manabii, wengine kama wahubiri wa injili, wengine kama wachungaji na waalimu, kwa kusudi la kutengenezwa upya kwa watakatifu, kwa kazi ya huduma, kwa kujengwa kwa mwili wa Kristo, hata sote tuufikie umoja katika imani na katika maarifa sahihi ya Mwana wa Mungu, tuwe mtu mzima, tufikie kimo cha ukamili wa Kristo; ili tusiwe vitoto tena, tukitupwa-tupwa kama kwamba na mawimbi na kuchukuliwa huku na huko na kila upepo wa kufundisha kwa hila ya wanadamu, kwa ujanja katika kutunga makosa.”—Efe. 4:11-14, NW.
3 Ingawa hatuna “mitume” na “manabii” waliokuwa na mgawo wa pekee katika kundi la kwanza, bado ‘wahubiri wa injili, wachungaji na waalimu’ wanawekwa na roho takatifu waongoze katika utumishi wa Mungu. Lo! Yehova, “mchungaji na mwangalizi wa nafsi” zetu, aliwawekea mfano mwema namna gani! (1 Pet. 2:25, NW) Lo! yeye huongoza kondoo kwa uanana namna gani “katika njia za haki kwa ajili ya jina lake!” (Zab. 23:1-6) Yeye huangalia kondoo kwa fadhili na ufahamu namna gani! “Bwana [Yehova] asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. . . . Nami nitawalisha malisho mema. . . . Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa.” (Eze. 34:11-16) Yehova huhakikisha kwamba “kondoo” wote wanafundishwa kupitia kwa tengenezo lake lililo kama mke, “mama” yao, ili wawe na amani tele na kuimarishwa sana katika haki.—Isa. 54:13, 14; Gal. 4:26.
4. Kumekuwa na matokeo gani kutokana na “kutengenezwa upya kwa watakatifu”?
4 ‘Watakatifu wameendelea kutengenezwa upya’ miaka iliyopita. Kadiri nuru ya ufahamu inavyoangaza zaidi, mawazo mapya yameondoa ya zamani. Sasa, katika miaka hii ya 1970, yaweza kusemwa kweli kweli kwamba ni “mchana mkamilifu” kati ya watu wa Yehova na kwamba kundi limekua kabisa. Kundi la Mungu ulimwenguni pote limeungana katika “umoja katika imani” unaotofautiana sana na migawanyiko iliyomo katika dini za kilimwengu za Kibabeli, hasa zile za Jumuiya ya Wakristo. Umoja kama huo unaoonekana sasa katika kila nchi kati ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova haujapata kuonekana tena usoni pa dunia. Wakiwa wameungana kusema kweli ya Biblia na katika kifungo cha upendo, hawapigwi na ‘pepo za kufundisha’ zenye dhoruba zinazopiga Jumuiya ya Wakristo sasa. Wamekuwa wenye bidii kufuata onyo la upole la Paulo: “Tukinena kweli, acheni kwa upendo tukue katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo.”—Efe. 4:15, NW; Mit. 4:18.
5, 6. (a) Ni maulizo gani yanafaa kuulizwa juu ya mpango wa wazee? (b) Yatupasa kuuonaje mpango huu?
5 Katika miaka ya karibuni tumeuthamini zaidi mpango wa kimungu wa kuweka wazee katika kila kundi. Hiyo yatuletea baraka. Walakini, je! wote wanajua hivyo kweli kweli? Je! wengine bado wanawaona wazee kwa maoni ya kibinadamu tu, maoni ya kimwili? Je! wengine hawataki kuzungumza matatizo ya kipekee yenye kuwasumbua na mzee? Je! wengine wanatia shaka wakiona mzee katika kundi lao wenyewe hana uwezo wa kufahamu tatizo lao na kutoa shauri la Maandiko lifaalo? Je! wanadhani kwamba utatuzi wa pekee ni kuandikia Watch Tower Society? Bila shaka, Sosaiti na Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova inafurahi kusaidia inapoweza. Lakini kumbuka kwamba wazee, waliowekwa na roho takatifu, ndio wajumbe wa Baraza Inayoongoza hapo, na wamo katika cheo cha kuangalia mambo yote.
6 Hatupaswi kamwe kudharau mpango wa wazee. Ni mpango wa Yehova wenye upendo kwamba wazee ‘wakeshe wakiangalia nafsi zetu.’—Ebr. 13:17, NW; 19:7-9.
7. (a) Ni “mizigo” gani tunayoweza kuchukuliana? (b) “Furushi” ambalo lazima kila mtu ajichukulie mwenyewe ni nini?
7 Katika habari hii, itatufaidi tukiangalia maneno ya Paulo katika Wagalatia 6:2, 5: “Mchukuliane mizigo,” na, “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” Je! maneno hayo yanapingana? Sivyo, kwa maana pana tofauti kati ya “mzigo” na “furushi.” Neno la Kigiriki la “mzigo” ni baʹros, nalo sikuzote lina maana ya kitu kizito chenye kulemeza. Hivyo, Mkristo akiingia katika ugumu fulani wa kiroho asioweza kuvumilia, waamini wenzake wenye upendo wamepaswa ‘kuitimiza sheria ya Kristo’ kwa kumsaidia. Wazee, hasa, wamepaswa kusaidia. ‘Mwenye mzigo’ asisite kutafuta msaada wao. Lakini wakati ule ule lazima ‘achukue furushi lake mwenyewe.’ Hapa Paulo atumia neno la Kigiriki phor·tiʹon, akimaanisha kitu cha kuchukuliwa, bila kutaja uzito wake. Sote twapaswa kuchukua “furushi,” hata hali ziweje—furushi letu wenyewe la daraka la kuwa waaminifu kama watumwa walio wakf wa Yehova Mungu.—Gal. 6:4; 2 Kor. 10:12.
8, 9. Ni kwa kadiri gani wazee wanaweza kusaidia ‘kuchukua mizigo yenu’?
8 Ikiwa unahitaji msaada wa ‘kuchukua mizigo yako’ usisite kutafuta msaada na mashauri kutoka kwa wazee. Watafurahi kukusaidia kadiri wawezavyo. Walakini, usitazamie wazee wakufanyie maamuzi. Maamuzi ni “furushi” lako mwenyewe, daraka lako. Si sawa wala haifai kuuliza mzee hivi: Wewe ungefanyaje kama ungekuwa katika hali yangu? Yeye hayumo katika hali yako. Lakini atafurahi kuangalia maandiko pamoja nawe na kukusaidia ufikirie mambo kwa msaada wa kanuni za Biblia. (Mit. 11:14) Mara nyingi jibu la ulizo au tatizo hueleweka kwa kuzungumza na mtu mwenye msingi mzuri wa maarifa ya Biblia na ujuzi ufaao. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia ufanye uamuzi wako mwenyewe.—Mit. 15:22.
9 Wazee wanaweza kusaidia kwa njia nyingi. Jinsi gani?
WAKATI MATATIZO YA KIPEKEE NA YA JAMAA YATOKEAPO
10. (a) Mwendo wa hekima kufuata ni nini ikiwa huwezi kuondoa udhaifu fulani unaoendelea kuwapo? (b) Ni nini kinachoonyeshwa na ‘kupaka mafuta,’ na nini nani awezaye kusaidia zaidi sana katika jambo hilo?
10 Je! unajitahidi sana kuondoa udhaifu unaoendelea kuwapo ijapokuwa umejitahidi kwa uaminifu kuuondoa? Yakobo 5:13-15 yashauri hivi: “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? na aombe. . . . Mtu wa kwenu amekuwa [mgonjwa kiroho]? na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la [Yehova]. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na [Yehova] atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” Kama vile kupaka mafuta kichwani kunavyotuliza na kuburudisha, ndivyo matumizi ya Neno la Mungu kwa mgonjwa wa kiroho yanavyomtuliza, kumsahihisha, kumfariji na kumpoza. (Zab. 141:5; Isa. 1:6) Hasa mzee mwenye ufahamu aweza kusaidia sana katika jambo hili.
11. Wengine wanawezaje kupata msaada wa kuwa na dhamiri safi?
11 Je! kuna kosa lo lote la zamani linalokuhuzunisha, kukuaibisha na kukutia mashaka juu ya kama Yehova amekusamehe? Mzee aweza kukusaidia uchunguze mwendo na nia yako iliyobadilika uone kama kuna sababu yo yote halisi ya kuamini kwamba Yehova hakukusamehe. Kumbuka vile Nathani, aliyekuwa nabii na bila shaka mzee katika Israeli, alivyotumiwa na Yehova kufanyiza katika Mfalme Daudi ‘moyo safi na roho mpya.’ (2 Sam. 12:1-13; Zaburi 51) Kama katika habari ya Daudi, wewe waweza kuwa na hakika kwamba sala za unyofu za kutubu zitasikiwa na Yehova. Ukiisha kutubu na kugeuka, unaweza kusonga mbele ukiwa na dhamiri safi, ukithamini rehema ya Yehova.—Zab. 86:15-17; Matendo 3:19, 20.
12. Ni kwa njia gani huenda wazee wakasaidia juu ya matatizo ya afya?
12 Je! umevunjwa moyo na tatizo la afya? Mzee hawezi kukuponya kwa mwujiza, lakini aweza kukutia moyo kwa uchangamfu na pengine kukupa mawaidha yanayofaa akusaidie uvumilie na kuendeleza Furaha yako. Sema naye. Wale ‘wanaosimamia katika Bwana’ ndio wanaopaswa kuongoza kusema “kwa kufariji nafsi zenye huzuni.” Wazee ndio wanaoweza kusaidia ‘kutia nguvu mikono dhaifu na kuimarisha magoti yanayotikisika,’ na ndio wanaoweza “kuwaambia wale walio na hangaiko moyoni: ‘Iweni wenye nguvu. Msiogope.’” Bila shaka wazee wanaweza kukufariji kiroho.—1 The. 5:12, 14; Isa. 35:3, 4, NW.
13-15. Wazee wanaweza kutoa msaada gani ufaao juu ya (a) matatizo ya kinyumbani, (b) kukosana kwa watu?
13 Je! wewe una tatizo la kinyumbani, pengine una mwenzi asiyeamini? Bila shaka unalifahamu sana shauri la Maandiko, kama 1 Wakorintho 7:10-16 na 1 Petro 3:1-9. Lakini washangaa, Nawezaje kutumia Maandiko hayo nifaulu zaidi? Mzee aweza kukupa mawaidha yafaayo unayohitaji. Aweza kukutembelea mnapokuwa nyumbani nyote pamoja, na kusaidia kumaliza wasiwasi, akikupa mawaidha yanayofaa ya kuendeleza uhusiano wenu.
14 Mara nyingi, mwenzi asiyeamini anakuwa amezuiwa na maongezi mabaya juu ya Mashahidi wa Yehova ya wafanya kazi wenzake au watu wa ukoo—kuhusu kutokuwamo, damu, masuala ya “sikukuu” au ibada ya sanamu. Kwa njia ya ufahamu, mzee aweza kueleza jinsi kila jambo linavyoungana na suala kuu la Ufalme lenye kuelekea upande ufaao, unaoleta furaha na amani ya kudumu, na ‘kushibisha kila kilicho hai matakwa yake.’—Zab. 145:9-16.
15 Je! umekosana na mtu fulani, na hiyo yakuchukiza, hata imekuwa vigumu kupatana naye? Pengine umetatizwa katika kujaribu kutumia shauri jema la Waefeso 4:26, 32. Ukisema na mzee, huenda akaweza kukusaidia usahau kosa hilo. Ikifaa, aweza kupanga kuzungumza nanyi wawili, akiwasaidia mpate utatuzi kwa kutumia kanuni za Biblia.—Zab. 119:97; 133:1.
16. Wazee wanawezaje kusaidia wenye haya?
16 Je! una haya za kupita kiasi, na ugumu wa kuzungumza na kufurahia ushirika na wengine? Ukimwuliza mzee, huenda akaweza kukusaidia uchukue hatua ya kwanza mara nyingi zaidi katika kusema na wengine. Pengine anaweza kukuonyesha jinsi ya kuona furaha ya kweli katika mashirika yako mikutanoni, na vilevile nyakati nyingine. “Moyo wa furaha huchangamsha uso,” na uso wako mwenyewe unapong’aa utaona furaha nyingi zaidi na zaidi ya kupata marafiki kati ya watu wa Yehova mwenyewe. (Mit. 15:13) Wazee, mwaweza kuchukua hatua ya kwanza kusaidia watu wenye haya wawe wenye kusema zaidi na wengine.—Yohana 13:34, 35; Flp. 2:4.
KUSAIDIA WOTE KATIKA UTUMISHI WA SHAMBANI
17. Wazee wanaweza kusaidia kwa njia gani ‘kutengeneza upya’ kwa habari ya matatizo yanayoonekana katika kazi ya kuhubiri injili?
17 Kulingana na Waefeso 4:8, 11, NW, “wahubiri wa injili” wametiwa kati ya “zawadi katika wanaume” za Kristo. Kwa kweli, katika cheo chao kama wahubiri wa injili, wazee wana pendeleo si la kuweka mfano wa juhudi katika kuutangaza Ufalme tu, bali pia kusaidia ndugu na dada zao wasitawishe uwezo mbalimbali katika utumishi huu. Tayari, huenda wengine wakawa wenye juhudi katika kueneza magazeti na vitabu mlango kwa mlango. Huenda wengine wakawa na uwezo wa kuzaliwa wa kutembelea tena wenye kupendezwa na kuanza mafunzo mapya. Huenda wengine wakawa bora zaidi katika kufundisha penye mafunzo ya Biblia na kuelekeza wapya mikutanoni. Wazee wanaweza kuzoeza watangazaji wa Ufalme wapanue utendaji wao na wawe wenye ujuzi pande nyingine. Wanaweza kusaidia washiriki wa kundi waache kuvunjika moyo kwa sababu eneo ni gumu, au wakati magumu makubwa ya maisha yanapozuia utumishi wao.—Isa. 32:1, 2.
18. Wazee wamepaswa kutia wengine moyo wawe na nia na hakika gani?
18 Wazee wanaweza kutoa mafundisho yanayofaa juu ya kujitayarisha kwa ajili ya kazi ya shambani, pengine kufanya mazoezi na wapya jinsi ya kutoa mahubiri ya Biblia. Wanaweza kuwatia moyo wawe na nia safi juu ya utumishi wa Yehova. Kugawa vitabu vingi shambani hakuonyeshi sikuzote mtu amepata matokeo mazuri, kwa maana ni jambo la kutamanika pia kuanza mafunzo ya Biblia na kufundisha vizuri kwa kusudi la kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19) Wazee wanaweza kutia wote moyo waendelee ‘kuzihubiri habari njema’ kwa bidii na kukesha wakiona haraka kuu ya nyakati. (Marko 13:10, 32-37) Wazee na wengine wote kundini wafanyapo kazi kwa bidii katika utumishi wa shambani, twaweza kuwa na hakika ya kupata uongozi wa malaika na baraka ya Yehova tunapokusanya “walio wake.”—2 Tim. 2:19; Mt. 25:31-33; Marko 4:3-8.
19. Wazee wanawezaje kutia moyo wanaotazamiwa kuwa mapainia na walio mapainia?
19 Je! unataka kupanua mapendeleo yako, pengine uwe “painia” mtangazaji wa wakati wote wa habari njema au “painia msaidizi”? Tena, mzee aweza kukusaidia kwa kukupa mawaidha yanayofaa. Kwa kuwa ana ujuzi, kwa kawaida huwa anafahamu sana marekebisho ambayo mtu apaswa kufanya, matatizo yaliyoko na namna ya orodha inayopaswa kupangwa. Wazee wanaweza kusaidia kufanya mipango ili wewe ufanye kazi na wahubiri wengine wa wakati wote wa Ufalme. Utumishi wako nao waweza kukujenga, nanyi nyote mwaweza kufurahi pamoja mkipata matokeo mazuri.—1 Tim. 4:15.
UNAPOKUWA NA MAULIZO YA BIBLIA
20. Wazee wanawezaje kusaidia kutafuta majibu ya maulizo ya Biblia?
20 Je! unaona ni vigumu kupata majibu ya maulizo ya Biblia? Wazee huenda wakaweza kukuonyesha jinsi ya kutumia ifaavyo Watch Tower Publications Indexes (fahirisi). Au ikiwa Indexes hazipatikani katika lugha yako, wazee wanaweza kukuonyesha njia nyingine zifaazo za kutafuta majibu. Mara nyingi, huenda mzee akaweza kukuonyesha mara moja andiko unalotaka. Ukitafuta msaada wa mzee kwanza, si mara nyingi itakapokuwa lazima uandikie Watch Tower Society upate jibu fulani.—Yohana 5:39; Matendo 17:11.
21, 22. (a) Ni maulizo gani yanayofaa kuachiliwa tu? (b) Toa mifano ya maulizo yanayoweza kujenga imani?
21 Walakini, yako maulizo mengine yanayofaa kuachiliwa tu. Maulizo ya kufikiri-fikiri hivi na hivyo na vile, bila msingi, ‘aleta maswali ya kuchunguza badala ya kutoa cho chote kwa Mungu kuhusiana na imani.’ (1 Tim. 1:4, NW) Katika kujenga imani, kuna faida gani kupelekea wazee au Sosaiti matatizo kama haya: Ingalikuwaje kama Adamu angalikula kati ya mti wa uzima kabla hajafukuzwa Edeni? Yehova angalifanyaje kama Yesu asingalikuwa mwaminifu alipokuwa duniani? Pesa za namna fulani zitatumiwa katika Taratibu Mpya, na namna gani mashine, magari, televisheni na kompiuta? Je! maji yaliyokuwa juu ya dunia yakiizunguka yangalianguka kama Adamu asingalitenda dhambi? Malaika husafiri kwa mwendo gani, na inachukua muda gani kwa kiumbe cha kiroho kusafiri kutoka mbinguni mpaka duniani?
22 Badala yake, wale wanaotafuta kweli kwa unyenyekevu watakuwa wakiuliza maulizo ya aina ambayo watafutaji wanyofu wa kweli walimwuliza Yesu.—Mt. 9:14; 13:10; Marko 9:11; 10:9, 10; Yohana 3:4; 16:17, 18; Matendo 1:6.
ITIKIA MASHAURI YA WAZEE
23. (a) Ni nini kinachoongoza wazee waangalie kundi? (b) Wazee wanawezaje ‘kutengeneza upya’ wengine “katika roho ya upole”?
23 Wazee wamepaswa wapendezwe zaidi sana na kusaidia wote wafikie mradi wa uzima wa milele. Hiyo haimaanishi lazima wachunguze-chunguze kila upande wa faragha wa maisha za watu. Lakini huenda kukawa na nyakati ambazo wazee wanaona ni lazima wazungumze na watu fulani juu ya mwenendo wao. Wakiona kwamba mtu fulani kundini afanya mambo yanayoweza kuhatirisha hali yake ya kiroho au mwishowe kumwangusha katika kweli, ni wajibu wao kumwonya mtu huyo. Hivyo wanaweza kumsaidia ajizuie kabla hajafikia hatua ya kupotea kabisa na kuingia katika dhambi nzito. “Ndugu, hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumtengeneza upya mtu huyo katika roho ya upole, huku kila mtu akijiangalia mwenyewe, usije wewe pia ukashawishwa.” (Gal. 6:1, NW) Mashauri na mawaidha yaweza kutolewa, na yapaswa yatiiwe, katika “roho ya upole.”
24. (a) Kwa sababu gani wazee wanajitoa kwa ajili ya “kondoo”? (b) Lakini ni dhambi gani wanazopaswa kupelekea halmashauri ya hukumu?
24 Hivyo mzee aweza kusaidia sana kwa kuonyesha mtu maelekeo fulani, hata katika mambo madogo, yanayoweza kuongoza kwenye matatizo makubwa. “Ndugu zangu, ikiwa mtu wa kwenu amepotelea mbali na kweli, na mtu mwingine akamrejeza; jueni ya kuwa yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu, ataokoa [nafsi] na mauti, na kufunika wingi wa dhambi.” (Yak. 5:19, 20) Wachungaji wadogo wa Kristo wanafahamu sana kwamba “haipendezi mbele za Baba yenu aliye mbinguni kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee,” na kwamba kuna “furaha mbinguni kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.” (Mt. 18:14; Luka 15:7) Kwa hiyo wazee hawa wanajitoa wenyewe kwa ajili ya kondoo. Lakini wanapelekea halmashauri ya hukumu kundini kesi za dhambi nzito.
25. Mzee aweza kutoa msaada gani juu ya ‘kutengeneza upya’ mtoto mtukutu?
25 Mwana mdogo wa mama Mkristo, mke wa mtu asiyeamini, huenda akawa mtukutu katika Jumba la Ufalme. Mzee aweza kuzungumza na mama huyo kwa fadhili na busara, akimsaidia na tatizo lake. Akikubali kupokea shauri, mzee aweza kupendekeza njia zifaazo za kufundisha nyumbani, ili mtoto asaidiwe kusitawisha adabu njema, kuheshimu wengine na, juu ya yote, sifa ya upendo. Huenda kujifunza kwa kawaida na watoto kukasaidia “mtoto-matata.” Inaweza kuonekana karibuni kwamba mambo yamerekebishwa nyumbani anapoonyesha mwenendo mwema mikutanoni penye Jumba la Ufalme.—Mit. 22:15; 23:13, 14; Kum. 11:18, 19.
26. Kutakuwa na matokeo gani ya kutii mashauri ya wazee kwa unyenyekevu kwa habari ya mitindo ya mavazi na nywele, na kadhalika?
26 Nyakati nyingine huenda ikawa lazima wazee waeleze mtu habari za mitindo ya mavazi au mapambo yanayoleta hali ya ulimwengu kundini au yanayoweza kuleta maoni mabaya kwa watu wa nje. (1 Tim. 2:9, 10; Rum. 12:2) Huenda ikawa vigumu kwao kutoa shauri hilo kama ilivyo vigumu kwa wengine wenye roho ya kujitegemea kulikubali. Lakini ni nini kitakacholeta mapatano, umoja na amani kundini? Ni kufuata kwetu mashauri ya “wazee” kwa unyenyekevu, wanaofikiria hali njema yetu ya kiroho. Na kumbuka, “thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha [Yehova] ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.”—Mit. 22:4; 1 Yohana 2:15-17.
27. Wazee wanawezaje kusaidia sana kwa kutia ndugu wengine moyo kundini?
27 Yawapasa wazee watie ndugu wengine moyo kwa uchangamfu wajaribu kufikia mapendeleo zaidi kundini. “Ikiwa mwanamume ye yote anafikilia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.” (1 Tim. 3:1, NW) Wote wana uwezo mbali-mbali unaoweza kusitawishwa kwa msaada wa roho ya Yehova, na ndugu wote walio wakf wamepaswa kutaka sana kuwa wenye mafaa kama iwezekanavyo katika kundi la Kikristo. Wazee wanaweza kuamsha nia hii ya kuelekea mema katika wengine, wakiwazoeza wakubali na kutimiza madaraka.—Mt. 6:33; Flp. 3:13.
28. Kwaweza kuwa na faida gani za kiroho wazee wakitia wengine moyo wafanye maendeleo kupitia kwa shule ya Kitheokrasi?
28 Kundi lote la Mungu—vijana na wazee, ndugu na dada—watathamini uchungaji wa fadhili. Kwa mfano, huenda mwanamke Mkristo akawa mwenye haya za kuandikwa katika Shule ya Kitheokrasi. Lakini mzee akimtia moyo kwa upendo na ufahamu, huenda akapata ushujaa wa kushiriki katika pendeleo hili. Mashauri ya kutia moyo kutoka kwa mzee anayesimamia Shule yaweza kusaidia wengi wawe wafanya kazi wenye uwezo zaidi shambani. Kuitikia mashauri kwa nia na kitiamoyo cha wazee kwaweza kuleta faida nyingi za kiroho.
‘KUA KATIKA MAMBO YOTE’
29. Mradi wa wazee na wengine wote kundini wapaswa kuwa nini?
29 Wazee wanapendezwa sana na nini? Wanataka kuona wote kundini wakiendelea ‘kukua,’ wawe zaidi kama Kristo katika utumishi wao na njia yao ya maisha. Wawe wameanza kushiriki miezi michache tu iliyopita, au wameshiriki miaka mingi, wote wanapaswa kuwa na mradi wa kufanya maendeleo ya kiroho. Tengenezo la Mungu linasonga mbele. Halipunguzi mwendo kamwe. Kwa hiyo, sababu gani sisi tupunguze mwendo?
30. Kwa sababu gani yawapasa wote waitikie uchungaji wa wazee kwa nia?
30 Maisha—nafsi—zinahusika. Ndiyo sababu wazee wanapendezwa sana sana na kila mtu aliyemo kundini. Kwa hiyo wote wamepaswa wasikilize sana Waebrania 13:17: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” Wao wanaweka mfano kwa juhudi yao katika utumishi wa Mungu na uchungaji wao wenye fadhili. Kukesha kwa ajili ya nafsi zenu si kuchunguza-chunguza mambo yenu ya faragha, bali ni kukesha kwa habari ya hali njema yenu ya kiroho, ambayo yawapendeza sana kwa njia ya udugu. Wachungaji wanafurahi kweli kweli kundi linapoitikia uangalizi wao wenye upendo. Kwa kweli, tunatiwa moyo ‘tuiige imani yao.’—Ebr. 13:7.
31. Kundi lapaswa kuwa na nia gani, basi, juu ya wazee?
31 Hizi “zawadi katika wanaume,” yaani, wazee kama ‘wahubiri wa injili, wachungaji na waalimu’ kundini, ni mpango wa wakati ufaao kweli kweli kutoka kwa Yehova kupitia kwa Kristo Yesu. Kwa kuwatambua kama mpango wa namna hiyo, acheni tuutegemee mfano wao wa juhudi, tusisite kuwaendea na matatizo na maulizo yetu. Wao ‘wamepewa’ kwetu kweli kweli kwa upendo, ili tupate ‘kukua katika mambo yote ndani ya yeye aliye kichwa, Kristo.’—Efe. 4:7, 8, 11, 15, NW.
[Picha katika ukurasa wa 514]
Kuongoza katika utumishi wa shambani, kufanya kazi na wengine, ni sehemu ya maana ya kazi ya wazee