Je, Unapenda Uhai?
“ACHENI nione nuru.” Haya ndiyo maneno ambayo yasemekana Giacomo Leopardi, mshairi Mwitalia, aliwaambia wale waliomhudumia kabla hajafa. Maneno hayo yadokeza jinsi mwanadamu anavyoupenda uhai, ambao wafananishwa na nuru.
Kupenda uhai ni msukumo wenye thamani unaofanya watu wengi waepuke hatari na kufanya yote wawezayo kuendelea kuishi. Kwa habari hiyo, mwanadamu si tofauti sana na wanyama, ambao wana silika yenye nguvu ya kutaka kuendelea kuishi.
Lakini ni uhai wa aina gani ambao kwa kweli twastahili kuwa nao na kuupenda? Si kuishi tu kifiziolojia—kupumua tu na kutembea. Wala kutosheka kwa ujumla hakutokani na ule mtazamo wa kutaka kujinufaisha maishani kadiri tuwezavyo. Falsafa ya Waepikurea, “acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa,” kwa kawaida haiwaridhishi watu. (1 Wakorintho 15:32) Ingawa kwa hakika mwanadamu ana mahitaji kadhaa ya kimwili yaliyo ya msingi, yeye pia ana mapendezi ya kitamaduni na ya kijamii, mbali na mahitaji ya kiroho, yanayohusu imani katika Mtu Mkuu Kuliko Wote. Kwa kusikitisha, mamia ya mamilioni, labda mabilioni ya watu wanapata mahitaji ya lazima tu ya maisha kwa sababu ya hali mbaya za kijamii na za kimazingira katika sehemu nyingi za ulimwengu. Watu wowote wanaotaka kutosheleza mahitaji yao ya kimwili tu—kula, kunywa, kuwa na mali, au kutosheleza tamaa za kingono—kwa kadiri fulani wanaishi kama wanyama, maisha yasiyoweza kuwaridhisha. Kwa hiyo, hawatumii rasilimali zenye maana zaidi zipatikanazo maishani ili kuridhisha akili na hisia za kibinadamu. Isitoshe, wowote wanaotaka kutosheleza tamaa zao za ubinafsi hawashindwi tu kunufaika kabisa maishani, bali pia hudhuru jamii ambamo wanaishi, nao hawaendelezi masilahi ya wengine.
Akithibitisha hilo, hakimu mmoja anayeshughulika na watoto wahalifu asema kwamba “matatizo ya maadili, kutukuzwa kwa violezo vya kuigwa visivyofaa, na kufanikiwa kwa njia za kutajirika upesi,” huelekea “kuendeleza roho iliyokuzwa sana ya kushindana.” Roho hiyo hutokeza tabia inayodhuru jamii na kuharibu vijana, hasa wanapoanza kutumia dawa za kulevya.”
Unajua kwamba maisha yana vivutio vingi—kwenda likizo sehemu zenye kupendeza, kusoma au kufanya utafiti wenye kupendeza, ushirika wenye kupendeza, muziki mzuri. Na kuna shughuli nyingine zinazoridhisha kwa njia mbalimbali. Wale walio na imani kubwa katika Mungu, na hasa Mungu wa Biblia, Yehova, wana sababu zaidi za kupenda uhai. Imani ya kweli ni chanzo cha nguvu na utulivu uwezao kuwasaidia watu wakabiliane na nyakati ngumu. Wanaomwamini Mungu wa kweli wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa.” (Waebrania 13:6) Watu wanaojua upendo wa Mungu huhisi anawapenda. Wao huitikia upendo wake, unaowaletea furaha nyingi. (1 Yohana 4:7, 8, 16) Wanaweza kuishi maisha yenye shughuli na yanayonufaisha wengine, ambayo ni chanzo cha uradhi. Ni kama vile Yesu Kristo alivyosema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Kwa kusikitisha, maisha ya sasa yahusisha mambo mengine pia. Kuteseka, ukosefu wa haki, umaskini, ugonjwa, na kifo zimeenea sana—kutaja tu baadhi ya sehemu zenye kuumiza zinazofanya maisha yawe magumu sana. Mfalme Solomoni wa taifa la Israeli la kale, aliyekuwa tajiri, mwenye uwezo, na hekima, alikuwa na rasilimali zote ziwezazo kufanya watu wawe na furaha. Hata hivyo, kuna kitu fulani kilichomsumbua—kung’amua kwamba wakati wa kufa angelazimika kumwachia mtu mwingine vitu vyote alivyokuwa amejipatia kwa ‘kazi yake yote’ aliyoifanya “kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi.”—Mhubiri 2:17-21.
Kama Solomoni, wengi wanafahamu ufupi wa uhai, ambao hupita upesi sana. Maandiko yasema kwamba Mungu “ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo [yetu].” (Mhubiri 3:11) Huku kufahamu umilele humfanya mwanadamu afikirie kwa uzito ufupi wa uhai. Hatimaye, kwa kutopata majibu yenye kusadikisha juu ya maana ya uhai na kifo, mtu aweza kulemewa na hisia za kutazamia mabaya na ubatili. Hilo laweza kufanya maisha yawe yenye kusikitisha.
Je, kuna majibu kwa maswali yanayomsumbua mwanadamu? Je, kutapata kuwako hali zinazofanya uhai uwe wenye kupendeza na wenye kudumu?