Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 2/15 kur. 81-87
  • Je! Wewe Unayatumiaje Maisha Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unayatumiaje Maisha Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NINI KINACHOHITAJIWA KWA MAISHA
  • MITHALI ZINATOA KANUNI ZA KUISHILIA
  • FUNZO LA BIBLIA LITAGEUZA MAISHA YAKO
  • YEHOVA ANAWASAIDIA WALIO WATIIFU
  • NJIA YA FURAHA
  • Hekima ya Kweli Inapaza Sauti Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Pata Hekima na Ukubali Nidhamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • “Bwana Huwapa Watu Hekima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kitabu Cha Biblia Namba 20—Mithali
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 2/15 kur. 81-87

Je! Wewe Unayatumiaje Maisha Yako?

“[Hekima] ni mti wa uzima kwao [waishikao] sana.”​—Mit. 3:18.

1-3. (a) Kwa sababu gani imetupasa tushukuru kwa uhai tulio nao sasa? (b) Je! Mungu anashiriki moja kwa moja katika uzazi wa kila mtoto? (c) Kwa sababu gani Yehova anawapa wengine uzima?

JE! WEWE unashukuru ya kwamba u hai? Je! umeweza kuwaza juu ya namna uhai ulivyo thawabu kubwa? Uhai unapopitishwa kutoka kwa wazazi mpaka kwa watoto namna za michanganyiko ya tabia na sifa zinazopitishiwa katika mpango wa uzazi ni nyingi sana katika hesabu. Kutokana na mstari mrefu wa hali zilizowapasa babu zako, wewe umetokea. Ni jambo la kutolea shukrani kweli kweli, kwa maana, kwa mfano, kama wazazi wako au wazazi wao wangalioa au kuolewa na wenzi tofauti, wewe usingalizaliwa wakati wo wote. Au kama mama yako angechukua mimba katika wakati tofauti, yule ambaye angezaliwa angalikuwa mtoto mwingine, siyo wewe.

2 Yehova ndiye Chanzo na Mpaji wa uzima. (Zab. 36:9) Yeye aliwapa Adamu na Hawa, kama kuumba kwake kwa moja kwa moja, uwezo wa kupitisha uhai kwa watoto wao. Katika Yohana 1:13 mtume anaonyesha kwamba wanadamu wanazaliwa kulingana na “mapenzi ya mwili,” mapenzi ya wazazi wao. Kwa hiyo, utu mbalimbali unaotokezwa hauamriwi tangu mwanzoni na Mungu, wala yeye hashiriki moja kwa moja katika uchukuaji wa mimba na uzazi wa watoto. Wakati na hali vinaongoza michanganyiko ya mambo katika chembe ya uzazi. Kwa hiyo imempasa mtu ashukuru sana kwamba yeye anaishi, kwamba anayo sehemu kati ya wale walio hai.

3 Yehova anaona ubora wa uhai sana. Yeye ndiye Mungu mwenye furaha, naye ataka wengine wawe wenye furaha. (1 Tim. 1:11) Yeye anafurahia kuona wengine wakifurahia kuishi. Kwa hiyo yeye anawapa wengine uzima kwa kusudi fulani. Lo! ni umuhimu wa kadiri gani anaoushikamanisha na kuishi katika njia ifaayo! Wanadamu wasipoyatumia maisha yao ovyo ovyo katika kufuatia mambo ya kipumbavu, lakini waishi katika njia ambayo Mungu aliwafanya waishi, yeye atawapa uzima wa milele.

NINI KINACHOHITAJIWA KWA MAISHA

4-6. (a) Nini kingine anachohitaji mwanadamu zaidi ya chakula cha kimwili ili aishi? (b) Kwa sababu gani mwanadamu anahitaji nguvu za kiroho kutoka kwa Mungu?

4 Ni lazima mwili utunzwe sikuzote kwa kupumua, kunywa na kula. Lakini kuna jambo la lazima zaidi kwa kuendelea kwa uhai. Hili ni nini? Basi, kati ya kuumba kote kwa Mungu kwa kidunia, ni mwanadamu peke yake aliyefanywa katika sura na mfano wa Mungu. (Mwa. 1:26, 27) Kwa hiyo, akiwa tofauti na “wanyama wasio na akili,” mwanadamu alipata sifa bora za upendo, haki, hekima na sifa nyinginezo za Mungu. (2 Pet. 2:12) Yeye alikuwa na uwezo wa kufahamu kwa ajili ya hali ya kiroho. Angeweza kuwaza juu ya sababu gani alikuwa ameumbwa; angeweza kujifunza juu ya ujamaa wake kwa Mungu. Na alipoendelea kupata ujuzi wa Mungu, sifa njema alizopewa na Mungu zingezidi kuongezeka ndani yake.

5 Zaidi ya hayo, uwezo wa mwanadamu kutwaa ujuzi wa Mungu, kufanya maendeleo kwa akili na kwa kiroho, haukuwa na kikomo. Mungu, kutoka kwa ghala Yake kubwa mno isiyopimika, angeweza kuendelea kumpa mwanadamu mambo haya ya lazima mpaka umilele wote. Kwa hiyo hali ya kiroho na hekima ya Mungu vingezidishwa ndani ya mwanadamu wakati wote.​—Rum. 11:33-36.

6 Kwa kulingana na umbo lake, ilimlazimu mwanadamu kupata nguvu za kiroho sikuzote kutoka kwa Yehova, kusudi aendelee kuishi. Alihitaji ujamaa wa kiroho na Mungu. Hata mwanadamu mkamilifu, akiwa na mambo yote ya lazima ya kimwili, angekufa asipokuwa na chakula cha kiroho. Kama mwanadamu angetwaa chakula cha kiroho, Mungu angempa mambo ya kimwili, kama vile alivyowafanyia Adamu na Hawa.​—Mwa. 1:29; 2:9; Mt. 6:33.

7. Ni mwendo gani mbaya alioufuata Adamu, na je! hii ilimfanya Mungu aliachilie kusudi lake kuelekea wanadamu?

7 Wasomaji wa Biblia wanajua kwamba Adamu hakuendelea kukaa karibu na Mungu katika utiifu na hekima na kuiongeza hali yake ya kiroho, bali yeye mwenyewe alijikatilia mbali na Mungu na akailetea jamaa ya kibinadamu dhambi na mauti. (Rum. 5:12) Hata hivyo, Mungu hakuliachilia kusudi lake kuelekea wanadamu. Yeye atawaletea wanadamu watiifu aliyoyakusudia kwao. Kwa sababu hii ameifanya Biblia iandikwe naye amemtuma Mwanawe kama dhabihu ya kufaidi wale ambao wanataka kumtumikia Yeye.​—Rum. 5:8.

MITHALI ZINATOA KANUNI ZA KUISHILIA

8-10. Kwa sababu gani mwandikaji mkubwa wa kitabu cha Biblia cha Mithali alikuwa na nafasi nzuri ya kujua juu ya maisha, na ujuzi wake ulikuwa na kina gani?

8 Kitabu cha Biblia cha Mithali kinatupa sisi kanuni za msingi za kuishilia. Mfalme Sulemani wa Israeli, mtungaji mkubwa wa Mithali, bila shaka alikuwa na ufahamu wa maisha katika namna zake nyingi. Alikuwa na wakati na nafasi ya kuchunguza maisha, naye alifikiri sana. Usiopaswa kusahauliwa ni uhakika wa kwamba Mungu, aliyeviumba vyote kwa hekima yake, alimpa Sulemani hekima kusudi kwamba angeweza kuyafahamu mambo haya.​—Mit. 3:19, 20; 1 Fal. 3:11-14.

9 Ujapokuwa ufalme wa Sulemani ulikuwa na eneo dogo tu katika Mashariki ya Kati, hekima yake ilijulikana na watu wa mataifa mengi, kwa maana inasemwa juu yake:

“Hekima ya Sulemani ikapita hekima ya wana wote wa mashariki, na hekima zote za Misri. . . . Naye akanena mifano elfu tatu, na nyimbo zake zilikuwa elfu moja na tano. Akanena habari za miti tangu mwerezi ulioko Lebanoni hata hisopo umeao ukutani; pia akanena habari za wanyama, na za ndege, na vitambaavyo, na samaki. Wakaja wa mataifa yote ili waisikie hekima ya Sulemani, toka wafalme wote wa ulimwengu, waliokuwa wamepata habari za hekima yake.”​—1 Fal. 4:30-34.

10 Sasa, si kwamba Sulemani alitaja tu kuumba huku kwa Mungu katika usemi wake; alikufahamu vile vile na ukuzi wake, tabia na njia, na vile vile mahali pake katika kazi za Mungu za kuumba. Vitabu vya Mithali na Mhubiri vile vile vinaifunua busara yake katika mwanadamu na tamaa zake na njia. Sulemani aliifahamu miendo ya hekima na ya upumbavu ambayo mwanadamu angeweza kuichukua, pamoja na matokeo yake.

11. Kwa sababu gani twaweza kuwa na matumaini yote katika kuyatumia maneno ya Sulemani katika maisha zetu?

11 Zaidi ya hayo, Mungu alikusudia kwamba Sulemani aseme na kuandika kwa ajili ya faida yetu, na kwa roho Yake aliyaongoza maneno ya Sulemani kwamba yanapita sana hekima ya mwanadamu wa kawaida. Yanafaa kuandikwa kama maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu katika Biblia, Neno la Mungu la kweli.

12. Mungu anataka nini kutoka kwa mwanadamu ili akipate kibali chake Yeye cha uzima wa milele?

12 Yehova Mungu anataka nini kwa mwanadamu kusudi aingie katika ujamaa mwema na Yeye na kuwa na tumaini la uzima wa milele? Sulemani anatuambia: “Kutenda haki na hukumu humpendeza [Yehova] kuliko kutoa sadaka.” (Mit. 21:3) Mungu hakumwomba mwanadamu afanye jambo lisilowezekana. Kupitia kwa nabii wake Mika, Yehova aliyahakikisha maneno ya Sulemani, akisema: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” Wawezaje kufanya hivi?​—Mik. 6:8.

13, 14. Ni azimio gani alilolifikia Sulemani juu ya maisha, na kwa sababu gani?

13 Pengine umeuchunguza ulimwengu na maisha kama wingi wa watu wanavyoyaishi. Unaona kuvunjika moyo, udhalimu na ubatili. Watu wengi wenye bidii kwa sababu hii, wamechoka, na leo hakuna ajuaye litakalofuata kutukia. Hata walio matajiri na walio wakuu wa dunia hawawezi kufanya lo lote kuzuia uzee na kifo. Mfalme Sulemani aliliona hili, naye akasema:

“Nikauchukia uhai; kwa sababu kazi inayotendeka chini ya jua ilikuwa mbaya kwangu; yaani, mambo yote ni ubatili na kujilisha upepo. Nami nikaichukia kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo chini ya jua; maana sina budi kumwachia yeye atakayenifuata. Naye ni nani ajuaye kama huyo atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo atatawala juu ya kazi yangu yote niliyojishughulisha nayo, ambamo ndani yake mimi nimeonyesha hekima chini ya jua. Hayo nayo ni ubatili.”​—Mhu. 2:17-19.

14 Sulemani hakuuchukia uhai wenyewe, lakini maisha kama yanavyoishiliwa chini ya taratibu ya mambo iliyopo. Yesu Kristo, aliyekuwa mkubwa zaidi kuliko Sulemani, alionyesha kwamba hii taratibu ya mambo i chini ya uongozi wa Shetani Ibilisi. Nyuma ya mwendo wake wa uaminifu, ambamo ‘aliushinda ulimwengu’ kwa kushika uaminifu kwa Mungu, yeye alisema: “Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje.” Tena alisema kwamba mtawala wa ulimwengu huu hakuwa na kitu kwake. Karibuni hii taratibu ya mambo pamoja na mtawala wake itaharibiwa.​—Yohana 16:33; 12:31; 14:30; 2 Kor. 4:4; Ufu. 11:18; 12:9.

15, 16. Ni jambo gani la kwanza analolihitaji mtu ili kuingia katika njia ya uzima?

15 Basi, twaweza kuishi namna gani kusudi tuepuke kuongozwa na “mkuu wa ulimwengu” na kuwa wenye kumpendeza Mungu, tuishi duniani chini ya taratibu mpya yenye haki mtawala wa ulimwengu huu atakapoondolewa katika cheo chake kisichoonekana cha uongozi wa hii taratibu ya mambo?

16 Ebu na tuyageukie tena maneno yenye hekima ya Sulemani kwa jibu. Yeye anatuambia: “Kumcha [Yehova] ni chanzo cha maarifa.” (Mit. 1:7) Kumcha Yehova ni kumweka yeye kwanza katika maisha ya mtu, kujifunza njia zake na kanuni na kumtii yeye kupita wengine wote. Akiwa na nia hii mtu yumo katika hali ambapo anaiona haja yake ya kiroho, haja ya chakula cha kiroho kutoka kwa Mungu ili aishi. (Mt. 5:3) Kisha Sulemani anasema hivi juu ya kuitafuta hekima ya Yehova: “Ukiendelea kuitafuta kama fedha, na kama hazina zilizofichwa ukiendelea kuitafuta, ndipo utakapoelewa kumcha Yehova, nawe utayapata maarifa yenyewe ya Mungu.”​—Mit. 2:3-5, NW.

FUNZO LA BIBLIA LITAGEUZA MAISHA YAKO

17. Ni maulizo gani ambayo lazima mtu ajiulize kwa uzito, ikiwa anataka uzima?

17 Hii ni wazi sana na nyepesi kufahamika. Maana yake ni kwamba, ili kupata uzima, lazima ujifunze Biblia. Ni kweli, kila mtu ana shughuli nyingi. Lakini angalia kwamba lazima tuitake hekima kama hazina, kama vile msakaji wa hazina alivyo na nia ya kujinyima wakati na nguvu na kuichimbua. Kwa hiyo, jiulize mwenyewe, ‘Je! mimi nayatumiaje maisha yangu? Je! naujaza wakati wangu kwa jumla na mambo yasiyoitosheleza haja yangu ya ujamaa wa kiroho na Mungu? Ikiwa ndivyo, nawe ‘huwezi kupata wakati’ kwa funzo la Biblia, basi, kwa sababu hiyo, unasema kwamba huutaki uzima. Hakuna awezaye kukupangia wakati wako; yakupasa kuchukua wakati kwa njia fulani ufanye hivyo. Ndipo wengine wanapoweza kukusaidia.​—Efe. 5:15, 16.

18. Kwa sababu gani si vigumu kupata ujuzi wa Biblia?

18 Unapoanza kuipata hekima hii kutoka kwa Biblia, unaiona Biblia nyepesi sana kufahamika na yenye unyofu. “Maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu,” yasema mithali. (14:6) Hii ni kweli. Nyuma ya kujifunza kwa muda unaanza kuunganisha habari mpya na mambo uyajuayo tayari. Ukweli wa Biblia ni wenye busara sana, unakamatana sana, kwamba ‘vipande’ vinaanza kuungana pamoja kwa haraka sana, na kusudi lote la Yehova linaanza kufahamika wazi. “Ndipo utakapofahamu haki na hukumu, na adili, na kila njia njema,” asema Sulemani.​—Mit. 2:9.

19. Unapoanza kuifahamu Biblia, ujuzi huu utaanza kukusaidia namna gani?

19 Unapoendelea kujifunza, inakuwa vyepesi zaidi kwako kuweka wakati kando kwa ajili ya mambo mema. Vile vile, hekima yako iliyopatikana karibuni itakuondosha kwenye mambo yasiyofaa. Usemi mbaya wala mizaha mibaya si sehemu ya usemi wako tena. Unaepuka kufanya hata mambo “madogo” yasiyo ya uaminifu. Mambo mengi uliyoyatamani wakati uliopita sasa yanaonekana kuwa mambo yasiyo na ubora wa kweli, wenye kuendelea. Sulemani aliutaja ukweli huu, akisema: “Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi. Ili kukuokoa na njia ya uovu, na watu wanenao yaliyopotoka; watu waziachao njia za unyofu, ili kuziendea njia za giza.”​—Mit. 2:10-13.

20. Mbali na ujuzi wa Biblia, ni msaada gani mwingine unaoupokea unapojifunza?

20 Mazoea haya mabaya yanapotupwa kando unaanza kutamani kushirikiana na wale ambao mazungumzo yao ni mazuri, wale ambao wanaweza kukujenga. Mashirika hayo yanaanza kuwa yenye kufurahisha kweli kweli. Pengine mtu fulani anajifunza Biblia nawe. Yeye na wengine wa imani ile ile watakuwa msaada mkubwa kwako na ulinzi, kwa maana ni kweli kwamba “yeye atembeaye na watu wenye hekima atakuwa mwenye hekima, bali yeye anayeenenda na wapumbavu atapatwa na mabaya.” Hapa neno la Kiebrania kwa ‘mpumbavu’ linamaanisha, si yeye asiye na ujuzi tu, lakini yeye asiyemcha Mungu, asiyeona kweli ya adili.​—Mit. 13:20, NW; linganisha Mithali 10:23; 13:19; 14:8.

21. Imekupasa uoneje unapoonyeshwa makosa na washiriki wako wa Kikristo?

21 Mara kwa mara huenda washiriki wako wapya wa Kikristo wakakazia fikira zako kwa upole kwenye jambo fulani litakalokusaidia kujipatanisha zaidi na maoni ya Mungu ya mambo. Huenda yakawa ni mazoea fulani uliyo nayo, mazoea fulani yaliyo kawaida ya ulimwengu, yanayokaziwa fikira zako. Pengine watakuelekeza kwenye maandiko fulani yanayozungumza juu ya jambo hili. Kuliko kukasirika au kuona uchungu, kumbuka kwamba wewe, kama Wakristo wote, umetoka katika ulimwengu usiomjua Mungu, ulimwengu ambao kwa kawaida unafanya mambo yasiyompendeza Mungu. Wewe umo katika utaratibu wa ‘kufanya upya nia yako.’ (Rum. 12:2) Wewe unajifunza sheria ya Mungu, na juu yake mtu mwenye hekima anasema: “Maana maagizo hayo ni taa, na sheria hiyo ni nuru, na maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima.”​—Mt. 6:23.

YEHOVA ANAWASAIDIA WALIO WATIIFU

22. Mithali zinauonyeshaje umuhimu wa kuadhibiwa?

22 Mungu anatutaka tuwe watiifu kwake, kama vile mwana kwa baba mwema, na, kama vile baba wa kale wa Kiebrania alivyomshauri mwanawe, ndivyo Mungu anavyotuambia: “Mwanangu, usidharau kuadhibiwa na [Yehova], wala usione ni taabu kurudiwa naye. Kwa kuwa [Yehova] ampendaye humrudi, kama vile baba mwanawe ampendezaye.” (Mit. 3:11, 12) Kama mtu anayejitahidi kuwa mwana mtiifu, unashukuru kwamba shauri hilo lilikaziwa fikira zako, kwamba mtu fulani alipendezwa nawe vya kutosha kukuonyesha njia ifaayo ya kufuata. Kilicho bora zaidi ni kuonyeshwa makosa ya mwendo mbaya mapema kuliko kufuata njia yetu wenyewe bila ya kuzuiwa, kwa maana mwandikaji mwenye hekima aliyeongozwa na roho ya Mungu anatuambia: “Maovu yake yeye yatampata mdhalimu, naye atashikwa kwa kamba za dhambi zake. Atakufa huyo kwa kukosa maonyo, naye atapotea kwa wingi wa ujinga wake.”​—Mit. 5:22, 23.

23. Kwa sababu gani sala ni ya maana katika kukutana na magumu ya maisha?

23 Kila mtu anakutana na magumu katika kufuata mwendo wa Kikristo, labda katika jamaa yake mwenyewe, katika hali yake na wafanya kazi wenzake au rafiki. Lakini waweza kupata faraja katika shauri lenye hekima: “Mkabidhi [Yehova] kazi zako, na mawazo yako yatathibitika.” (Mit. 16:3) Unaweza kumpelekea Yehova magumu yako katika sala ukiwa na uhakikisho kwamba yeye atakujibu. “Maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake” na “huisikia sala ya mwenye haki.” (Mit. 15:8, 29) Yehova atakutia nguvu naye ‘ataiimarisha’ mipango ufanyayo umtumikie kwa njia ya kukubalika.​—⁠Mhu. 4:9-12.

24. Ni daraka gani linaloonyeshwa wazi katika Mithali 24:27?

24 Wakati uliopita, pengine ulikazia fikira zaidi kwenye mahitaji ya kimwili ya nyumba yako. Lakini sasa unaiona haja yao ya kiroho. Biblia inatoa maoni yaliyosawazika, kwa maana inasema: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” (Mit. 24:27) Kama vile ambavyo mkulima wa Kiebrania alivyolitunza shamba lake, akilitayarisha kwa ajili ya kupanda na uvunaji wa mazao, ndivyo nawe, kwa kazi ya kimwili, unavyoitolea jamaa yako mambo ya kimwili. Lakini daraka lako halikomei hapo. Haja ya kuijenga nyumba yako kwa kiroho ni ya muhimu vile vile. Kufanya hivi, unaona, kunafurahisha zaidi kuliko kazi yako ya kimwili, nako kunathawabisha zaidi, kwa maana unajua unajiokoa, si wewe peke yako, lakini vile vile na wale unaowapenda sana.​—Linganisha 1 Timotheo 4:15, 16.

25. Nini kinachotokea kwa mtu ambaye ‘anamheshimu Yehova kwa mali zake’?

25 Vile vile unakuja kuijua maana ya kweli ya mithali: “Mheshimu [Yehova] kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote.” Kama vile Waisraeli walivyomletea Yehova vitu vyao vilivyo bora, ndivyo Mkristo afanyavyo katika pande zote za maisha yake. “Ndipo,” yasema hekima kutoka kwa Mungu, “ghala zako zitakapojazwa kwa wingi, na mashinikizo yako yatafurika divai mpya.” (Mit. 3:9, 10) Hii haina maana ya msingi ya mali za kimwili, ajapokuwa Mungu anawahakikishia watu wake kwamba mahitaji yao ya maisha yatatolewa. Zaidi inamaanisha mali za kiroho, pamoja na furaha na usalama vinavyoletwa na hizi. “Ulalapo hutaona hofu; naam, utalala na usingizi wako utakuwa mtamu. Usiogope hofu ya ghafula, wala uharibifu wa waovu utakapofika. Kwa kuwa [Yehova] atakuwa tumaini lako, naye atakulinda mguu wako usinaswe.”​—Mit. 3:24-26.

26. Katika kupata hekima kwa Mungu, unajifunza mambo gani juu ya matumizi ya ulimi?

26 Unapoufuata mwendo huu, unasitawisha maishani mwako matunda ya roho ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Unajifunza kupenda kuzungumza juu ya mambo mema, juu ya makusudi ya Mungu. Unaisitawisha tamaa ya kusaidia wengine nawe unayazungumza haya kwa wengine wasioijua mipango mizuri ya Mungu. Ni kama vile mithali isemavyo: “Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri; bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.” (Mit. 15:2) Unajifunza kuepuka taabu kwa kushika lako mwenyewe, kwa maana unajua kwamba “yeye alindaye kinywa chake huilinda nafsi yake; bali afunuaye midomo yake atapata uharibifu,” na “mwenye haki huchukia kusema uongo.” Unakuja kujua kwamba, “asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi.”​—Mit. 13:3, 5; 14:29; 16:32.

NJIA YA FURAHA

27. Ni mageuzi gani katika nia na maoni ya wakati ujao anayoyapata mtu kwa kupata hekima kutoka kwa Mungu, na pamoja na faida gani?

27 Ukiifuata njia hii uliyoipata karibuni ya maisha, unaanza kuwa na taraja lenye kuchangamsha, la kutazamia mema wakati ujao. “Amwaminiye [Yehova] ana heri,” alisema Sulemani. (Mit. 16:20) Unafurahi, si kwa njia ya kijuujuu, kama vile ufanyavyo ulimwengu, lakini ndani sana ya moyo wako, kwa maana unaangazishwa na kweli. “Mng’ao wa macho huufurahisha moyo.” (Mit. 15:30) Mageuzi yako katika usemi yanaonwa na wanaokufahamu. Hata unapata faida kwa afya yako, kwa kuwa matabibu wanaukubali ukweli wa mithali: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili,” na “moyo uliochangamka ni dawa nzuri.” (Mit. 14:30; 17:22) Ingawa ulimwengu kwa jumla unahuzunika, hata unapokuwa katika shida yako siyo huzuni ya ulimwengu isiyo na matumaini. (Linganisha 1 Wathesalonike 4:13.) Mashahidi wa Yehova, wanapomtumikia Mungu, wameona ni kweli kwamba “ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.” (Mit. 15:15) Na karibu mara tatu kwa mwaka, kwenye makusanyiko ya mashahidi wa Yehova, wote wanaufurahia wakati mzuri usio na kifani, “karamu,” kutwaa ujuzi wa Biblia, wakifurahia ushirika mwema na safari.

28. Eleza Mithali 19:17: “Amhurumiaye maskini humkopesha [Yehova]; naye atamlipa kwa tendo lake jema.”

28 Unakuja kuwa na washiriki wengi katika kundi la Kikristo walio “ndugu na dada” kwa kiroho. Kama alivyosema mtume Paulo, “si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo” waliomo kati yao. (1 Kor. 1:26-29) Lakini wawe ni matajiri au maskini, wao ni wanyenyekevu wa moyo, kama alivyokuwa Yesu. Zaidi ya hayo, unawakuta wengine katika ulimwengu waliomo katika hali yenye huzuni kwa sababu ya taabu inayoongezeka duniani. Vile vile wako walio maskini. Unapowafanyia hawa mema, Yehova anaiona fadhili yako. Mwandikaji mwenye hekima anatuambia: “Amhurumiaye maskini humkopesha [Yehova]; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mit. 19:17) Ajapokuwa aliye maskini huenda asiweze kulipa kwa njia yo yote, Yehova anauhesabu wema uliofanywa kama ukimlazimu aulipe, naye anafanya hivyo kwa wingi sana.

29. Ni juu ya nia gani yampasa mtu afikirie sana, juu ya anavyoyatumia maisha yake?

29 Kwa hiyo, je! wewe unayatumiaje maisha yako? au je! wewe unataka maisha yako yaweje? Je! unashukuru kuwa na kadiri fulani ya maisha sasa? Je! una nia ya kujitahidi vya kutosha ujifunze mipango ya Mungu na matakwa kwa uzima wa milele? Ikiwa ndivyo, basi je! unayo nia ya kuendelea katika mwendo ufaao, ukiishika hali yako ya kiroho kwa kujifunza Biblia, kushirikiana na wale wanaomtumikia Mungu katika kuzitangaza habari njema za ufalme wa Mungu na kushiriki kwa kawaida pamoja nao? Je! unayo nia ya kuyaweka maisha yako wakf kwa Yehova Mungu, ukiishi katika kujitoa kwa nafsi yote kwake? Ikiwa ndivyo, Yehova Mungu na Mwanawe watakupenda, na vile vile wale wanaomtumikia Mungu, nao watakusaidia uifuate njia na kukaa katika mwendo unaoongoza kwenye uzima wa milele.

[Picha katika ukurasa wa 82]

Mithali za Sulemani zinatoa kanuni za msingi za kuishilia; akiwa na hekima aliyopewa na Mungu alizungumza juu ya njia za wanyama na tabia za mimea, na vile vile miendo ya hekima na ya kipumbavu ya wanadamu

[Picha katika ukurasa wa 83]

Funzo la kipekee la Neno la Mungu ni la muhimu kwa watu wazima . . .

. . . na kwa watoto

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki