Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 12/15 kur. 9-13
  • Kupata Amani ya Kweli Katika Nchi Yenye Ghasia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupata Amani ya Kweli Katika Nchi Yenye Ghasia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • “Nitakapokuwa Mtu Mzima, Nitajiunga na IRA!”
  • Kutounga Mkono Upande Wowote Ni Ulinzi Kwelikweli
  • “Kinga Yangu Ilikuwa Ni Bunduki Zangu Tu”
  • “Sikuelewa Ni kwa Nini Hali Iko Hivyo”
  • “Sikuzote Mashahidi Walituelekeza Katika Biblia”
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 12/15 kur. 9-13

Kupata Amani ya Kweli Katika Nchi Yenye Ghasia

“Lile tatizo lenye kutisha la ghasia za kidini haliwezi kudhibitiwa,” ikasema ripoti moja ya mwaka wa 1969. Wakati huo ndipo zile Ghasia, kipindi cha sasa cha msukosuko katika Ireland Kaskazini, zilipoanza kuongezeka.

GHASIA za kidini na mauaji yakawa mambo ya kawaida huku wauaji Waprotestanti na Wakatoliki, “watu wakali kutoka pande zote mbili” zilizogawanyika kisiasa na kidini, wakizidi kung’ang’ania mamlaka katika Ireland. Tangu wakati huo “zaidi ya watu 3,600 wameuawa na maelfu wakalemazwa katika takriban miaka 30 ya ghasia,” The Irish Times laripoti.

Bila shaka, mapambano hayo si mapya. Yameikumba Ireland kwa karne nyingi. Katika miaka ya karibuni Ireland Kaskazini ndiyo imekumbwa na matokeo mabaya zaidi, lakini maisha ya watu kotekote Ireland yameharibiwa na uchungu na kutoelewana ambako mapambano hayo yamesababisha.

Katika hali hiyo, kwa zaidi ya miaka mia moja sasa, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakionyesha suluhisho la kweli la matatizo ambayo yameikumba nchi hiyo yenye ghasia. Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo ndio suluhisho. (Mathayo 6:9, 10) Ghasia zilipoanza mwaka wa 1969, Mashahidi wa Yehova nchini Ireland walikuwa 876. Sasa kuna Mashahidi zaidi ya 4,500, katika makutaniko zaidi ya 100. Hapa pana mambo kadhaa yaliyowapata wengine ambao wameacha shughuli za kisiasa na za kijeshi.

“Nitakapokuwa Mtu Mzima, Nitajiunga na IRA!”

Michael,a alikulia Jamhuri ya Ireland akiwa Mkatoliki. Shuleni alifunzwa mambo fulani kuhusu historia ya Ireland na mapambano kati yake na Uingereza ambayo yamedumu kwa karne nyingi. Akiwa mtoto, alisitawisha chuki nyingi dhidi ya Waingereza, ambao aliwaona kuwa “waonezi wa watu wa Ireland.” Alipofika umri wa miaka kumi, alimwambia nyanya yake, “Nitakapokuwa mtu mzima, nitajiunga na IRA!” (Jeshi la Jamhuri ya Ireland) “Nilipigwa kofi usoni ambalo ninalikumbuka hadi leo,” yeye asema. Baadaye alipata kujua kwamba babu yake alikuwa katika jeshi la Uingereza wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Wakati mmoja ilimbidi nyanya yake asimame mbele ya babu yake ili kumkinga asipigwe risasi na wafuasi wa IRA.

Hata hivyo, Michael alipofika umri mkubwa kidogo alitaka kuwasaidia kwa njia fulani Wakatoliki wenzake katika Ireland Kaskazini. “Wakati huo niliona kwamba,” yeye asema, “wafuasi wa IRA pekee ndio waliokuwa wakijaribu kuwasaidia Wakatoliki wa Ireland Kaskazini.” Kwa kuchochewa na kile alichoona kuwa harakati ya haki, akawa mfuasi wa IRA na kupata mazoezi ya kutumia silaha. Rafiki zake watatu walipigwa risasi na kuuawa na wanajeshi Waprotestanti katika Ireland Kaskazini.

Hatimaye Michael alivunjwa moyo na mapambano ya kijeshi, akisumbuliwa, kwa mfano, na uhasama mkali ulioendelea miongoni mwa vikundi mbalimbali vya kijeshi. Michael alipokuwa gerezani kwa makosa yaliyohusiana na utendaji wa IRA, yeye aliomba Mungu amsaidie kupata njia ambayo hasa ingemwongoza kwenye amani na haki ya kudumu. Baadaye, Mashahidi wa Yehova wakamtembelea nyumbani. Lakini ubaguzi aliokuwa nao zamani ukatokeza vizuizi. Mashahidi hao walikuwa Waingereza. Aliwachukia sana hivi kwamba ilikuwa vigumu kwake kuwasikiliza. “Sikuwakaribisha sikuzote,” yeye asema, “lakini waliendelea kunitembelea na kuzungumza nami, hivyo nikaanza kuona kwamba Ufalme wa Mungu ungekomesha ukosefu wote wa haki katika siasa na jamii ambao nilikuwa niking’ang’ania kuukomesha.”—Zaburi 37:10, 11; 72:12-14.

Michael alikuwa na wakati mgumu jioni moja alipokutana na kamanda msimamizi wa IRA, aliyesema, “Kuna jambo fulani tunalotaka ufanye.” “Niliona ni lazima nifanye uamuzi papo hapo,” Michael asema, “hivyo nikavuta pumzi kwa nguvu na kusema, ‘Sasa mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova,’ japo sikuwa hata nimebatizwa wakati huo. Nilijua kabisa kwamba nilitaka kuwa mtumishi wa Yehova.” “Unapaswa kusimamishwa kwenye ukuta na kupigwa risasi,” huyo kamanda akajibu. Licha ya tisho hilo, Michael aliacha IRA. Alipata ujasiri wa kufanya hivyo kwa kuacha maneno ya Yehova yaguse akili na moyo wake. “Baada ya muda, mke wangu na baadhi ya watoto wangu pia wakajiweka wakfu kwa Yehova. Sasa tuna amani ya kweli mioyoni mwetu. Nasi tutamshukuru Yehova daima kwa kutuwezesha kujifunza kweli na kushiriki katika kueneza ujumbe wa amani katika nchi yenye ghasia.”—Zaburi 34:14; 119:165.

Kutounga Mkono Upande Wowote Ni Ulinzi Kwelikweli

“Nilikulia mashambani katika Wilaya ya Derry, Ireland Kaskazini,” asema Patrick. “Nikiwa mtoto, kulikuwa na Ghasia nyingi. Ni wazi kwamba hali hiyo iliathiri mtazamo wangu na maoni yangu.” Patrick alisitawisha maoni yenye siasa kali yaliyoathiriwa na uzalendo mbaya sana na ubaguzi mkali dhidi ya Waingereza. Aliona watu wa dini kutoka pande zote mbili za mapambano hayo ya kisiasa wakikiuka kanuni muhimu za Kikristo na vilevile kanuni za msingi za ubinadamu. Kwa sababu hiyo yeye akaacha dini na hatimaye akawa mwatheisti na Mfuasi mkubwa wa Maksi.—Linganisha Mathayo 15:7-9; 23:27, 28.

“Kumbukumbu zangu za mapema zaidi ni juu ya wafungwa Kaskazini wenye kususia chakula, ambao walipendelea sera ya serikali ya jamhuri,” asema Patrick. “Kumbukumbu hizo ziliniathiri sana. Ninakumbuka nikipandisha bendera za Ireland na kuandika mahali popote pale kwenye kuta maneno yenye kupinga Uingereza. Nikiwa na umri wa miaka 15 tu, nilisimamia maziko ya mmoja wa watu hao wenye kususia chakula aliyefia gerezani.” Kama wengineo wengi waliojikuta katika misukosuko na vurugu za wakati huo, Patrick alishiriki katika ghasia na maandamano ya kuteta akifuatia kile alichoona kuwa haki na usawa wa kijamii. Alisitawisha urafiki wa karibu na wazalendo kadhaa wenye siasa kali, ambao wengi wao walikuwa wametiwa gerezani na serikali ya Uingereza.

“Ndipo,” asema Patrick, “kwa sababu za kiuchumi, nikaishia kukaa Uingereza kwa muda fulani. Nilipokuwa huko, polisi wa Uingereza walimtia mbaroni mmoja wa rafiki zangu aliyekuwa ameenda huko kufanya shambulizi la bomu.” Hata ingawa Patrick alikuwa bado anaunga mkono sana harakati ya wazalendo, mtazamo wake ulianza kubadilika. Alianza kuona kwamba hakuwa na sababu yoyote ya kuwabagua Waingereza wote. “Nilianza kuona pia kwamba,” yeye asema, “utendaji wa kijeshi haungesuluhisha kamwe matatizo na kuondoa ukosefu wa haki ulionihuzunisha. Kulikuwa na ufisadi mwingi kupita kiasi na kasoro nyinginezo miongoni mwa wale waliosimamia mashirika ya kijeshi.”—Mhubiri 4:1; Yeremia 10:23.

Hatimaye Patrick alirudi Ireland Kaskazini. “Niliporudi, rafiki yangu alinijulisha kwa Mashahidi wa Yehova.” Kutokana na funzo lake la Biblia pamoja na Mashahidi, Patrick alianza kuona suluhisho kamili la mapambano na kutopatana kwa wanadamu. Kanuni za Biblia zilipogusa akili na moyo wake, yeye alifanya maendeleo ya kiroho haraka. (Waefeso 4:20-24) “Sasa,” yeye asema, “badala ya kula njama ya kupindua mfumo wa utawala uliopo, mimi huhubiri ujumbe wa amani kutoka kwa Biblia, hata katika maeneo ya watu wenye kuitii serikali ambako hapo awali singethubutu kwenda. Kwa kweli, wakati mmoja ambapo kulikuwa na mauaji mengi ya kidini katika Belfast, Mashahidi wa Yehova pekee ndio walioweza kutembea kwa uhuru baina ya watu wenye kuitii serikali na waasi bila kutumia gari za kivita.” Kama Mashahidi wengine katika Ireland Kaskazini wakati huo, Patrick aliona kwamba kutounga mkono upande wowote, kama Wakristo wa mapema walivyofanya, ni ulinzi kwelikweli. (Yohana 17:16; 18:36) Yeye amalizia kwa kusema: “Ni jambo lenye kutuliza sana kujua kwamba kupitia Yesu Kristo, Yehova atawaletea wanadamu wote haki na uhuru wa kweli kutokana na uonevu.”—Isaya 32:1, 16-18.

“Kinga Yangu Ilikuwa Ni Bunduki Zangu Tu”

“Nilikulia upande mwingine wa mgawanyiko wa kisiasa na wa kidini,” asema William. “Niliathiriwa sana na ubaguzi wa Kiprotestanti, nikachukia sana chochote kilichohusiana na Ukatoliki. Hata singeingia katika duka la Mkatoliki, na nilitembelea Jamhuri ya Ireland wakati mmoja tu. Nilishirikiana na vikundi na mashirika mbalimbali ya Waprotestanti, kama Orange Order—shirika ambalo limejitolea kuhifadhi dini na njia ya maisha ya Waprotestanti.” Alipokuwa na umri wa miaka 22, William alijiunga na Kikosi cha Ulinzi cha Ulster, sehemu ya jeshi la Uingereza ambalo wanajeshi wake hutoka Ireland. Askari wengi katika kikosi hicho walikuwa Waprotestanti. William alikuwa tayari kuua ili kutetea urithi wake. “Nilikuwa na bunduki kadhaa na nisingesita kuzitumia ikihitajika. Niliweka moja chini ya mto wangu usiku.”

Lakini ukawadia wakati wa kuchukua hatua muhimu. “Nilianza kutambua kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na kitu fulani cha pekee nilipofanya kazi ya kurekebisha nyumba ya zamani pamoja na mmoja wao. Huyo mfanyakazi mwenzangu alikuwa na uvutano mkubwa kwangu. Tulipokuwa tukijenga nyumba hiyo pamoja, niliweza kumwuliza maswali mengi yaliyonisumbua kuhusu zile Ghasia, dini, na Mungu. Majibu yake sahili na ya wazi yalinisaidia kujua jinsi Mashahidi wa Yehova walivyo hasa—watu wenye muungano, wasiofanya jeuri na wasiounga mkono upande wowote kisiasa, wampendao Mungu na jirani.”—Yohana 13:34, 35.

Miezi minne tu baada ya kuanza kujifunza Biblia, William akaacha mashirika yote ya kidini na ya kisiasa aliyokuwa akishirikiana nayo. “Hiyo ilikuwa hatua muhimu kwangu,” yeye akumbuka, “kwa sababu ilinibidi kuacha desturi ambazo nilikuwa nimezipenda kwa muda mrefu.” Hata hivyo, William angepatwa na jaribu kubwa zaidi baadaye. “Kwa sababu ya hali katika Ireland Kaskazini, niliona kwamba kinga yangu ilikuwa ni bunduki zangu tu. Jeshi la IRA ‘lilinilenga.’ Hivyo ilikuwa vigumu sana kuachana na silaha hizo.” Hata hivyo, mashauri ya Biblia kama yale yapatikanayo kwenye Isaya 2:2-4, yalibadili mtazamo wake polepole. Hatimaye, akaona kwamba Yehova ndiye angemlinda kikweli, kama Alivyowalinda Wakristo wa karne ya kwanza. William akaachana na bunduki.

“Mojawapo ya mambo ninayofurahia sana,” asema William, “ni kwamba sasa nina urafiki mkubwa na wenye kudumu pamoja na watu ambao hapo awali niliwaona kuwa adui za hadi kifo. Pia, inafurahisha kwelikweli kuweza kupeleka ujumbe wa Biblia wa tumaini katika maeneo ambayo hapo awali ‘yalikuwa marufuku’ kwangu. Mimi humshukuru Yehova daima nifikiriapo mambo ambayo kweli imenifanyia mimi na familia yangu.”

“Sikuelewa Ni kwa Nini Hali Iko Hivyo”

Robert na Teresa wametoka katika familia tofauti kabisa. “Mimi nimetoka katika familia inayofuata Uprotestanti kwa dhati,” asema Robert. “Baadhi ya watu wangu wa ukoo wamehusika katika utendaji wa kijeshi. Mimi mwenyewe nilijiunga na Kikosi cha Ulinzi cha Ulster cha jeshi la Uingereza nikiwa na umri wa miaka 19. Nilitumia wakati mwingi katika kikosi hicho nikishika doria katika maeneo ambapo Teresa aliishi. Usiku mmoja nikapewa mgawo wa kufanya kazi tofauti. Usiku huo gari ambalo ningalisafiria likalipuliwa. Askari wawili wakauawa na wengine wawili wakajeruhiwa.”

Robert akaanza kufikiria kusudi la uhai. “Nilimwamini Mungu sikuzote, lakini nilipotazama mambo katika Ireland Kaskazini, sikuelewa ni kwa nini hali iko hivyo. Nikaanza hasa kusali kwa Mungu. Nilimwuliza Mungu kama yeye kweli yuko, na kama yuko, anionyeshe njia ifaayo ya kuishi. Ninakumbuka nikimwambia Mungu kwamba ni lazima kuwe na dini ya kweli mahali fulani!” Baada tu ya siku kadhaa, mmoja wa Mashahidi wa Yehova akamtembelea Robert na kumwachia kichapo fulani. Alipokuja nyumbani akiwa amechelewa katika doria ya usiku huo, Robert alianza kusoma kichapo hicho na kukimaliza saa kumi na moja alfajiri. “Niliitambua kweli mara moja,” yeye asema, “na ningeweza kuona kwamba kila kitu kilitoka moja kwa moja katika Biblia.” (2 Timotheo 3:16) Alianza kujifunza Biblia na baada ya muda mfupi akajiweka wakfu kwa Mungu.

“Sikuzote Mashahidi Walituelekeza Katika Biblia”

Kwa upande mwingine, Teresa alitoka katika familia ya Wakatoliki, ambao waliunga mkono waasi sana. “Nikiwa msichana mdogo, nilijiunga na Sinn Féin.”b Teresa akiri: “Jambo hilo likafanya niunge mkono utendaji wa kijeshi. Nilisaidia kuchangisha fedha kwa ajili ya mapambano ya kijeshi. Nilikuwa nikiwapasha habari wafuasi wa IRA juu ya yale yaliyokuwa yakiendelea katika eneo letu. Nilihusika pia katika ghasia na kushambulia polisi na wanajeshi walioshika doria.”

Wakati baadhi ya familia ya Teresa walipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, hamu yake ya kutaka kujua ikachochewa pia. Nguvu za Neno la Mungu zikawa na uvutano mkubwa juu yake. “Sikuzote Mashahidi walituelekeza katika Biblia ili kupata majibu kwa maswali yetu,” yeye asema. “Ahadi ipatikanayo kwenye Danieli 2:44 ilinizindua sana. Niliona kwamba Ufalme wa Mungu ndio njia hasa ya kuondoa ukosefu wa haki niliokuwa nikipambana nao.” Alichukizwa sana na baadhi ya ukatili uliokuwa ukifanywa na wanajeshi. Kwa mfano, Teresa hangeweza kuelewa ni kwa nini mtu mwenye huruma na adabu angefurahia habari kuhusu tendo la kigaidi lenye kuua au kulemaza wanajeshi au watu wengine na vilevile kuleta huzuni na uchungu kwa familia. Yeye pia aliikubali kweli ya Biblia na kuacha kanuni za Mungu zirekebishe maoni yake. Alijiweka wakfu kwa Mungu na muda si muda akabatizwa.—Mithali 2:1-5, 10-14.

Teresa alikutana na Robert walipohudhuria mikutano kwenye mojawapo ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika Ireland Kaskazini. Teresa aeleza hivi: “Nilipokutana na Robert mara ya kwanza, ilikuwa vigumu kuamini kwamba nilikuwa nikizungumza kwa utulivu na kwa amani na mtu ambaye hadi hivi karibuni ningalimwona kuwa mwanajeshi wa Uingereza. Bila shaka, Neno la Mungu limenisaidia kuondoa chuki na ubaguzi zilizokuwa zimetia mizizi.” Yeye na Robert waliona kwamba badala ya kugawanywa na chuki na ubaguzi unaotokana na desturi na tamaduni tofauti, sasa walipatana katika mambo mengi. Kati ya mambo yote, upendo kwa Yehova Mungu ndio uliokuwa wenye nguvu zaidi. Wakafunga ndoa. Sasa wanashirikiana kupeleka ujumbe wa amani wa Mungu kwa watu wa aina zote na wenye itikadi tofauti katika nchi hiyo yenye ghasia.

Wengine katika Ireland wamepatwa na mambo kama hayo. Kwa kusikiliza na kukubali mafundisho ya Neno la Mungu lililopuliziwa, wao wamejiepusha na “falsafa na udanganyo mtupu” wa wanadamu. (Wakolosai 2:8) Sasa wao wanatumaini kabisa ahadi za Mungu zilizorekodiwa katika Biblia. Wanafurahi kuzungumza na yeyote atakayesikiliza tumaini lao la wakati ujao wenye amani—ambao hautakuwa na jeuri yoyote ya kidini au jeuri ya aina yoyote ile.—Isaya 11:6-9.

[Maelezo ya Chini]

a Majina yamebadilishwa.

b Chama cha kisiasa chenye uhusiano wa karibu na Jeshi la IRA.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mapambano ya kijeshi yametukuzwa katika michoro kotekote katika Ireland Kaskazini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki