“Tunaweza Kuziamshaje Parokia Zetu?”
SWALI hilo, ambalo hivi karibuni liliulizwa na gazeti la Kifaransa la Katoliki Famille Chrétienne (Familiaya Kikristo), halishangazi wengi. Kadinali Hume wa Uingereza hata aliziita parokia za kanisa “majitu yaliyolala.” Imependekezwa parokia ziwe na watu wa kuhubiria wengine ili kuziamsha kwenye usingizi huo. “Kueneza evanjeli moja kwa moja kwa kutumia njia mpya,” kasisi mmoja Mwitalia aitaja hivyo. Ingawa hivi karibuni papa alihimiza hatua kama hizo zichukuliwe, si wote wanaoona uhitaji wa kuzungumzia imani yao.
Padre Pigi Perini wa Milan, alitembelea Afrika hivi karibuni, ambako mtawa mmoja wa kike alimwambia hivi: “Nimekuwa hapa kwa miaka 40, na sijawahi kuzungumza kuhusu jina la Yesu kusudi nisiharibu utamaduni wa Kiafrika.” Padre huyo amalizia kwa kusema: “Hatuzungumzi tena kumhusu Yesu, hatuna ushirika tena na Yesu, hatuhubiri gospeli tena!” Lakini, kwa wengineo wengi, kuhubiri ni sehemu muhimu ya maisha yao na pia ni njia ya kudumu wakiwa macho kiroho. Pigi Perini akiri: “Unakuta watu wawili sokoni wakizungumza kuhusu Kristo, au wakibeba Biblia mkononi, na unawaza: Ona, Mashahidi wa Yehova!”
Mamilioni ya watu hufurahia kuzungumzia Neno la Mungu pamoja na Mashahidi wa Yehova. Yaelekea Mashahidi wamepanga kuwa na mazungumzo ya Biblia katika jumuiya yako mwenyewe. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, Wakristo hao wenye bidii hutiana moyo ili waeleze wengine imani yao. Mahali pao pa kukutania (paitwapo Majumba ya Ufalme) ni penye uchangamfu na urafiki. Mbona usihudhurie mmojawapo ya mikutano iliyopangwa na Mashahidi wa Yehova na kuona jinsi uwezavyo kupambana na kusinzia kiroho?