“Saa Yake Ilikuwa Haijaja Bado”
“Hakuna aliyemwekea mkono amshike, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.”—YOHANA 7:30.
1. Matendo ya Yesu yalitegemea mambo gani mawili?
‘MWANA wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi,’ Yesu Kristo akawaambia mitume wake. (Mathayo 20:28) Alimwambia gavana wa Roma, Pontio Pilato, hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu alijua barabara ni kwa nini angekufa na ni kazi gani aliyohitaji kufanya kabla hajafa. Pia alijua alikuwa na muda mwingi kadiri gani wa kutekeleza kazi yake. Huduma yake duniani akiwa Mesiya ingechukua muda wa miaka mitatu na nusu tu. Ilianza kwa ubatizo wake wa maji katika Mto Yordani (mwaka wa 29 W.K.) mwanzoni mwa lile juma la 70 la mfano lililotabiriwa, na kumalizika kwa kifo chake kwenye mti wa mateso katikati ya juma hilo (mwaka wa 33 W.K.). (Danieli 9:24-27; Mathayo 3:16, 17; 20:17-19) Hivyo, matendo yote ya Yesu duniani yalitegemea hasa mambo mawili: kusudi lake la kuja na kufahamu wakati barabara wa kutenda.
2. Yesu Kristo anafafanuliwaje katika Gospeli, naye alionyeshaje kwamba alifahamu kazi yake?
2 Masimulizi ya Gospeli yanamfafanua Yesu Kristo kuwa mtu wa vitendo ambaye alisafiri kotekote nchini Palestina, akihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu na kufanya kazi nyingi zenye nguvu. Wakati wa huduma ya Yesu ya mapema yenye bidii, inasemwa hivi kumhusu: “Saa yake ilikuwa haijaja bado.” Yesu mwenyewe alisema hivi: “Wakati wangu upasao bado haujaja kikamili.” Karibu mwishoni mwa huduma yake, alitumia usemi “saa imekuja.” (Yohana 7:8, 30; 12:23) Ni lazima kule kufahamu saa, au wakati wa kufanya kazi aliyopewa, kutia ndani kifo chake cha kidhabihu, kuwe kuliathiri yale ambayo Yesu alisema na kufanya. Kujua mambo hayo kwaweza kutupa ufahamu wenye kina juu ya utu wake na njia yake ya kufikiri, kukitusaidia ‘kufuata hatua zake’ kwa ukaribu zaidi.—1 Petro 2:21.
Kuazimia Kufanya Mapenzi ya Mungu
3, 4. (a) Ni nini kinachotukia arusini huko Kana? (b) Kwa nini Mwana wa Mungu anakataa dokezo la Maria kwamba apaswa kufanya jambo fulani kuhusu upungufu wa divai, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
3 Ni mwaka wa 29 W.K. Siku chache tu zimepita tangu Yesu awateue wanafunzi wake wa kwanza. Sasa wote wamekuja kijijini Kana katika wilaya ya Galilaya kuhudhuria karamu ya arusi. Maria, mama ya Yesu, amekuja pia. Kunakuwa na upungufu wa divai. Akidokeza kwamba Yesu anapaswa kufanya jambo fulani, Maria amwambia mwana wake: “Hawana divai.” Lakini Yesu anamjibu: “Nina jambo gani na wewe, mwanamke? Saa yangu haijaja bado.”—Yohana 1:35-51; 2:1-4.
4 Jibu la Yesu, “Nina jambo gani na wewe, mwanamke?” ni aina ya swali la zamani linaloonyesha kukataa yale yanayodokezwa au kupendekezwa. Kwa nini Yesu anakataa maneno ya Maria? Sasa ana umri wa miaka 30. Majuma machache mapema, alibatizwa, akatiwa mafuta kwa roho takatifu, na kujulishwa na Yohana Mbatizaji kuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29-34; Luka 3:21-23) Sasa lazima aongozwe na Mwenye Mamlaka Kuu Zaidi aliyemtuma. (1 Wakorintho 11:3) Hakuna yeyote, hata mshiriki wa familia wa karibu, ambaye angeweza kuruhusiwa kuingilia kazi ambayo Yesu alikuja duniani kufanya. Katika jibu lake kwa Maria, Yesu anaonyesha azimio lililoje la kufanya mapenzi ya Baba yake! Na tuazimie vivyo hivyo kutimiza ‘wajibu wetu wote’ kwa Mungu.—Mhubiri 12:13, NW.
5. Yesu Kristo anafanya muujiza gani huko Kana, nao unaathirije wengine?
5 Akifahamu maneno ya mwana wake, Maria anamwondokea mara moja na kuwaambia wale wenye kuhudumu: “Lolote lile awaambialo nyinyi, fanyeni.” Kisha Yesu anatatua tatizo hilo. Anawaagiza wahudumu waijaze mitungi maji, naye anayageuza kuwa divai nzuri sana. Huu unakuwa wonyesho wa kwanza wa nguvu za Yesu za kufanya miujiza, ukiashiria kwamba roho ya Mungu i pamoja naye. Imani ya wanafunzi wapya inaimarishwa wanapoona muujiza huo.—Yohana 2:5-11.
Mwenye Bidii kwa Ajili ya Nyumba ya Yehova
6. Kwa nini Yesu anaghadhibikia yale anayoona kwenye hekalu huko Yerusalemu, naye anachukua hatua gani?
6 Muda si muda, masika ya mwaka wa 30 W.K. yanafika, na Yesu na wenzake wako njiani kwenda Yerusalemu kuadhimisha Sikukuu ya Kupitwa. Wakiwa huko, wanafunzi wake wanamwona Kiongozi wao akitenda kwa njia ambayo labda hawajawahi kumwona akitenda. Wafanya-biashara Wayahudi wenye pupa wanauza wanyama na ndege wa dhabihu ndani ya hekalu. Nao wanawatoza waabudu waaminifu Wayahudi bei ghali sana. Akiwa amejawa na ghadhabu, Yesu anachukua hatua. Anatengeneza mjeledi kwa kamba na kuwafukuzia mbali wauzaji hao. Anamwaga sarafu za wabadili-fedha na kupindua meza zao. “Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!” anawaamuru wale wanaouza njiwa. Wanafunzi wa Yesu wanapomwona akitenda kwa bidii hivyo, wanakumbuka unabii juu ya Mwana wa Mungu: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila mimi kabisa.” (Yohana 2:13-17; Zaburi 69:9) Sisi pia tufanye bidii kutoruhusu maelekeo ya ulimwengu yachafue ibada yetu.
7. (a) Ni nini kinachomchochea Nikodemo kumtembelea Mesiya? (b) Tunajifunza nini kutokana na ushahidi ambao Yesu anamtolea mwanamke Msamaria?
7 Huko Yerusalemu, Yesu afanya ishara za ajabu, na watu wengi wanamwamini. Hata Nikodemo, mshiriki wa Sanhedrini, au mahakama kuu ya Wayahudi, anavutiwa na Yesu na anakuja kwake usiku ili kujifunza zaidi. Kisha Yesu na wanafunzi wake wanakaa katika “nchi ya Yudea” kwa miezi minane hivi, wakihubiri na kufanya wanafunzi. Hata hivyo, baada ya Yohana Mbatizaji kutiwa gerezani, wanaondoka Yudea kwenda Galilaya. Wanaposafiri kupitia wilaya ya Samaria, Yesu anatumia fursa fulani kumtolea ushahidi mwanamke Msamaria. Hilo linawasaidia Wasamaria wengi kuwa waamini. Sisi pia na tuwe chonjo kutumia fursa zinazotokea kuzungumza juu ya Ufalme.—Yohana 2:23; 3:1-22; 4:1-42; Marko 1:14.
Ufundishaji Mwingi Galilaya
8. Yesu anaanza kazi gani Galilaya?
8 Yesu ana mambo mengi ya kufanya katika utumishi wa Baba yake wa mbinguni kabla ya “saa” yake ya kufa. Huko Galilaya, Yesu anaanza huduma kubwa zaidi kuliko ile aliyoanzisha Yudea na Yerusalemu. “[A]enda akizunguka kotekote katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu miongoni mwa watu.” (Mathayo 4:23) Maneno yake yenye kuchochea: “Tubuni, nyinyi watu, kwa maana ufalme wa mbingu umekaribia,” yavuma wilaya nzima. (Mathayo 4:17) Baada ya miezi michache, wanafunzi wawili wa Yohana Mbatizaji wanapokuja kupata ripoti ya moja kwa moja kumhusu Yesu, yeye anawaambia: “Shikeni njia yenu mwende, ripoti kwa Yohana yale mliyoona na kusikia: vipofu wanapata kuona, vilema wanatembea, wenye ukoma wanasafishwa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa, maskini wanaambiwa ile habari njema. Na mwenye furaha ni yeye ambaye hakukwazika juu yangu.”—Luka 7:22, 23.
9. Kwa nini umati unamfuata Kristo Yesu, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
9 ‘Maongezi mazuri kumhusu Yesu yanasambaa katika nchi yote yenye kuzunguka,’ na umati mkubwa kutoka Galilaya, Dekapolisi, Yerusalemu, Yudea, na ng’ambo ya Mto Yordani unamfuata. (Luka 4:14, 15; Mathayo 4:24, 25) Watu hao wanamjia kwa sababu ya mafundisho yake ya kustaajabisha na pia kwa sababu ya maponyo yake ya kimuujiza. Ujumbe wake ni wenye kuvutia na kutia moyo vilevile. (Mathayo 5:1–7:27) Maneno ya Yesu yanavutia sana na kupendeza. (Luka 4:22) Umati huo “u[na]shangaa juu ya njia yake ya kufundisha,” kwa kuwa anatumia Maandiko kwa mamlaka. (Mathayo 7:28, 29; Luka 4:32) Ni nani asingeweza kuvutiwa na mtu kama huyo? Sisi pia na tusitawishe ustadi wa kufundisha ili wanyofu wavutwe kwenye ile kweli.
10. Kwa nini watu wa mji wa Nazareti wanajaribu kumwua Yesu, na kwa nini wanashindwa?
10 Hata hivyo, si wote wanaomsikiliza Yesu wanakubali anayosema. Hata mapema katika huduma yake, anapofundisha katika sinagogi la mjini kwake Nazareti, kuna jaribio la kumwua. Ingawa watu wa mjini wanastaajabia ‘maneno yake yenye uvutio mwingi,’ wao wanataka kuona miujiza. Lakini, badala ya kufanya kazi nyingi za nguvu huko, Yesu anafichua ubinafsi na ukosefu wao wa imani. Wakiwa wamejawa na hasira, wale walio katika sinagogi wanainuka, wanamkamata Yesu, na kumpeleka haraka kwenye mlima kusudi wamwangushe chini kichwa-mbele kutoka sehemu yenye mwinamo mkali. Lakini anawaponyoka na kwenda zake salama. “Saa” ya kifo chake haijaja bado.—Luka 4:16-30.
11. (a) Kwa nini viongozi fulani wa kidini wanakuja kumsikiliza Yesu? (b) Kwa nini Yesu anashtakiwa kwamba amevunja Sabato?
11 Mara nyingi viongozi wa kidini—waandishi, Mafarisayo, Masadukayo na wengineo—wanakuwepo pia mahali Yesu anapohubiri. Wengi wao wanakuwepo, si kusikiliza na kujifunza, bali kutafuta makosa na kujaribu kumnasa. (Mathayo 12:38; 16:1; Luka 5:17; 6:1, 2) Kwa mfano, anapozuru Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 31 W.K., Yesu anamponya mtu ambaye amekuwa mgonjwa kwa miaka 38. Viongozi wa kidini Wayahudi wanamshtaki Yesu kwamba amevunja Sabato. Yesu anajibu: “Baba yangu amefuliza kufanya kazi hadi sasa, na mimi nafuliza kufanya kazi.” Sasa Wayahudi wanamshtaki kwamba amekufuru kwa kuwa amesema yeye ni Mwana wa Mungu alipomwita Baba. Wanataka kumwua Yesu, lakini yeye na wanafunzi wake wanaondoka Yerusalemu kwenda Galilaya. Vivyo hivyo, tunapotumia nguvu zetu kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, ni hekima kuepuka mapambano yasiyofaa na wapinzani.—Yohana 5:1-18; 6:1.
12. Yesu anahubiri eneo la Galilaya kwa njia gani kubwa?
12 Kwa muda wa mwaka mmoja na nusu hivi unaofuata, Yesu anafanya huduma yake sanasana huko Galilaya, akizuru Yerusalemu tu kuhudhuria ile misherehekeo mitatu ya kila mwaka ya Wayahudi. Kwa jumla, amefanya safari tatu za kuhubiri Galilaya: ya kwanza akiwa na wanafunzi wake 4 wapya, ya pili akiwa na mitume 12, na nyingine kubwa zaidi ambapo mitume waliozoezwa wanatumwa pia. Wanatoa ushahidi mkubwa kama nini huko Galilaya!—Mathayo 4:18-25; Luka 8:1-3; 9:1-6.
Kutoa Ushahidi kwa Ujasiri Huko Yudea na Perea
13, 14. (a) Wayahudi wanajaribu kumkamata Yesu pindi gani? (b) Kwa nini maofisa wanashindwa kumkamata Yesu?
13 Ni vuli ya mwaka wa 32 W.K., na “saa” ya Yesu haijaja bado. Msherehekeo wa Matabenakulo unakaribia. Ndugu wa kambo wa Yesu wanamhimiza: “Pita mbele uvuke kutoka hapa uende kuingia Yudea.” Wanataka Yesu aonyeshe nguvu zake za kufanya miujiza kwa wote ambao wamekusanyika kwenye msherehekeo huko Yerusalemu. Hata hivyo, Yesu anafahamu hatari iliyopo. Hivyo anawaambia ndugu zake: “Mimi bado sipandi kwenda kwenye msherehekeo huu, kwa sababu wakati wangu upasao bado haujaja kikamili.”—Yohana 7:1-8.
14 Yesu anakawia kwa muda huko Galilaya kisha anaenda Yerusalemu “si waziwazi bali kama katika siri.” Wayahudi hata wanamtafuta kwenye msherehekeo, wakisema: “Yuko wapi mtu yule?” Katikati ya msherehekeo, Yesu anaenda hekaluni na kuanza kufundisha kwa ujasiri. Wanajaribu kumkamata, labda ili wamtie gerezani au wamwue. Hata hivyo, hawafaulu kwa sababu ‘saa yake bado haijaja.’ Wengi sasa wanamwamini Yesu. Hata maofisa ambao Mafarisayo wamewatuma wakamkamate wanarudi mikono mitupu, wakisema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.”—Yohana 7:9-14, 30-46.
15. Kwa nini Wayahudi wanachukua mawe kumvurumishia Yesu, na baadaye anaanzisha kampeni gani ya kuhubiri?
15 Mapambano kati ya Yesu na wapinzani wake Wayahudi yanaendelea anapofundisha kuhusu Baba yake katika hekalu wakati wa msherehekeo. Siku ya mwisho ya msherehekeo, Wayahudi wanakasirishwa na maneno ya Yesu kuhusu maisha yake kabla ya kuwa mwanadamu nao wanachukua mawe ili wamvurumishie. Lakini anajificha na kuponyoka bila madhara. (Yohana 8:12-59) Yesu anakaa nje ya Yerusalemu na kuanzisha kampeni kubwa ya kutoa ushahidi huko Yudea. Anateua wanafunzi 70 na, baada ya kuwaagiza, anawatuma wawili wawili kwenda kuhubiri eneo hilo. Wanatangulia kwenda kila mahali na kila jiji ambako Yesu, akiandamana na mitume wake, anapanga kwenda.—Luka 10:1-24.
16. Yesu anaponyoka hatari gani wakati wa Msherehekeo wa Wakfu, naye anashughulika na kazi gani kwa mara nyingine tena?
16 Katika majira ya baridi kali ya mwaka wa 32 W.K., “saa” ya Yesu inakaribia. Anakuja Yerusalemu kwa Msherehekeo wa Wakfu. Wayahudi bado wanataka kumwua. Wanamzingira Yesu anapotembea katika safu ya nguzo za hekalu. Wanachukua mawe wamwue wakimshtaki tena kuwa amekufuru. Lakini Yesu anaponyoka kama alivyofanya kwenye pindi zilizotangulia. Upesi anazunguka akifundisha kutoka mji hadi mji na kijiji hadi kijiji katika wilaya ya Perea, ng’ambo ya Yordani kutoka upande wa Yudea. Na wengi wanamwamini. Lakini ujumbe wa dharura kuhusu rafiki yake mpendwa Lazaro unafanya arudi Yudea.—Luka 13:33; Yohana 10:20-42.
17. (a) Yesu anapata ujumbe gani wa dharura anapohubiri Perea? (b) Ni nini kionyeshacho kwamba Yesu anafahamu kusudi la hatua anayopaswa kuchukua na wakati barabara wa matukio?
17 Ujumbe huo wa dharura unatoka kwa Martha na Maria, dada za Lazaro, wanaoishi Bethania ya Yudea. “Bwana, ona! yule ambaye una shauku naye ni mgonjwa,” aliyetumwa anasema. “Ugonjwa huu hauna kifo kikiwa lengo lao,” anajibu Yesu, “bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kupitia huo.” Ili kutimiza kusudi hilo, Yesu anaendelea kukaa kimakusudi mahali alipo kwa siku mbili. Kisha anawaambia wanafunzi wake: “Twendeni tuingie Yudea tena.” Kwa mshangao wanamjibu: “Rabi, juzijuzi tu Wayudea walikuwa wakitafuta sana kukupiga kwa mawe, na je, wewe unaenda huko tena?” Lakini Yesu anafahamu kwamba ‘saa za nuru ya mchana’ zinazobaki, au muda ambao Mungu ametenga kwa ajili ya huduma yake duniani, ni mfupi. Anajua barabara anachopasa kufanya na kwa nini.—Yohana 11:1-10.
Muujiza Ambao Hakuna Yeyote Angeweza Kuupuuza
18. Hali ikoje Bethania Yesu anapofika huko, na kunatukia nini anapofika?
18 Huko Bethania, Martha ndiye wa kwanza kumlaki Yesu, akisema: “Bwana, kama ungalikuwa hapa ndugu yangu asingalikufa.” Maria na wale waliokuwa wamekuja nyumbani kwao wanafuata. Wote wanalia. “Mmemlaza wapi?” Yesu anauliza. Wanajibu: “Bwana, njoo uone.” Wanapofika kwenye kaburi la ukumbusho—pango lililofunikwa kwa jiwe—Yesu aagiza hivi: “Liondoeni mbali jiwe.” Bila kufahamu jambo ambalo Yesu anakusudia kufanya, Martha anakataa: “Bwana, kufikia sasa lazima awe anuka, kwa maana ni siku nne.” Lakini Yesu anauliza: “Je, sikukuambia kwamba kama ungeamini ungeona utukufu wa Mungu?”—Yohana 11:17-40.
19. Kwa nini Yesu anasali kwa sauti kabla ya kumfufua Lazaro?
19 Jiwe linalofunika mlango wa kaburi la Lazaro linapoondolewa, Yesu anasali kwa sauti kubwa ili watu wajue kwamba kile anachotaka kufanya kinatimizwa kwa nguvu za Mungu. Kisha anapaaza sauti: “Lazaro, njoo huku nje!” Lazaro anatoka nje mikono yake na miguu yake ikiwa bado imefungwa nguo za maziko na uso wake umefunikwa kwa kitambaa. “Mfungueni mmwache aende,” Yesu anasema.—Yohana 11:41-44.
20. Wale wanaomwona Yesu akimfufua Lazaro wanafanyaje?
20 Wanapoona muujiza huo, Wayahudi wengi ambao walikuwa wamekuja kumfariji Martha na Maria wanamwamini Yesu. Wengine wanaenda zao kuwaambia Mafarisayo yaliyotokea. Mafarisayo wanafanya nini? Mara moja wao na makuhani wakuu wanapanga mkutano wa dharura wa Sanhedrini. Kwa wasiwasi, wanahuzunika: “Twapaswa kufanya nini, kwa sababu mtu huyu hufanya ishara nyingi? Tukimwacha hivyo, wao wote wataweka imani katika yeye, na Waroma watakuja na kuondolea mbali mahali petu na taifa letu pia.” Lakini Kayafa, Kuhani wa Cheo cha Juu, anawaambia: ‘Nyinyi hamwoni kwamba ni kwa manufaa yenu mtu mmoja afe kwa ajili ya watu kuliko taifa lote liangamizwe.’ Kwa hiyo, kuanzia siku hiyo na kuendelea wanashauriana wamwue Yesu.—Yohana 11:45-53.
21. Muujiza wa kufufuliwa kwa Lazaro unakuwa mwanzo wa nini?
21 Kwa hiyo, kwa kukawia kufika Bethania, Yesu anafanya muujiza ambao hakuna yeyote awezaye kuupuuza. Kwa nguvu kutoka kwa Mungu, Yesu anamfufua mtu ambaye amekuwa mfu kwa siku nne. Hata Sanhedrini iliyo maarufu inalazimika kuutambua muujiza huo na inamhukumia kifo Mfanya-Miujiza huyo! Hivyo, muujiza huo unakuwa mwanzo wa badiliko kubwa katika huduma ya Yesu—badiliko kutoka wakati ambapo “saa yake ilikuwa haijaja bado” hadi wakati ambapo “saa imekuja.”
Ungejibuje?
• Yesu alionyeshaje kwamba alifahamu kazi aliyopewa na Mungu?
• Kwa nini Yesu anakataa dokezo la mama yake kuhusu divai?
• Tunaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo mara nyingi Yesu alishughulika na wapinzani?
• Kwa nini Yesu anakawia kuchukua hatua kuhusu ugonjwa wa Lazaro?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Yesu alitumia nguvu zake kutekeleza jukumu alilopewa na Mungu