Je, Wewe Ni Mwenye Busara?
MUSA alipochagua waamuzi wa Israeli, alijitahidi kutafuta “wanaume wenye hekima na busara na wenye uzoefu.” (Kumbukumbu la Torati 1:13, NW) Uzoefu, ambao ulitokana na umri, haukuwa kanuni pekee ya kuamulia mambo. Hekima na busara pia zilikuwa sifa za maana.
Mtu mwenye busara hufikia uamuzi mzuri katika usemi na mwenendo. Kulingana na Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary, mtu mwenye busara pia “anaweza kunyamaza kwa busara.” Naam, kuna “wakati wa kunena,” na kuna “wakati wa kunyamaza,” na mtu mwenye busara hufahamu tofauti hiyo. (Mhubiri 3:7) Mara nyingi, kuna sababu nzuri ya kunyamaza, kwa kuwa Biblia yasema: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.”—Mithali 10:19.
Wakristo hutumia busara wanaposhughulika na wenzao. Si lazima yule ambaye huongea sana au kwa mkazo zaidi awe ndiye wa maana zaidi. Kumbuka kwamba, Musa alikuwa “mwenye nguvu katika maneno,” lakini hangeweza kuliongoza taifa la Israeli hadi alipositawisha subira, upole, na kujidhibiti. (Matendo 7:22) Kwa hiyo, wale waliopewa mamlaka juu ya wengine lazima hasa wajitahidi kuwa wenye kiasi na kuonyesha roho ya kukubali sababu. –Mithali 11:2.
Wale ambao Yesu Kristo amewakabidhi “mali zake zote” wanafafanuliwa katika Neno la Mungu kuwa ‘waaminifu na wenye busara.’ (Mathayo 24:45-47) Wao hawaendi mbio kuliko Yehova; wala hawabaki nyuma wakati mwelekezo wa Mungu kuhusu jambo fulani unapokuwa wazi. Wanajua wakati wa kunena na wakati wa kungoja kimya ili kupata uelewevu zaidi. Inafaa Wakristo wote waige imani yao na pia wajithibitishe kuwa wenye busara, kama jamii ya mtumwa inavyofanya.—Waebrania 13:7.