Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w01 2/15 kur. 8-11
  • Kuwatafuta Wenye Kustahili Nchini Kenya

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwatafuta Wenye Kustahili Nchini Kenya
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Vichwa vidogo
  • Watu wa Ukoo—Majirani Wetu wa Karibu Zaidi
  • Takataka Zatoa Kitu Chenye Thamani
  • Kuhubiri Kazini
  • Matokeo ya Kustaajabisha Zaidi
  • Kushughulikia Ongezeko
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
w01 2/15 kur. 8-11

Kuwatafuta Wenye Kustahili Nchini Kenya

KENYA ni nchi yenye uzuri wa asili wenye kuvutia. Misitu iliyostawi, nyanda pana zilizo wazi, majangwa yenye joto jingi, na milima yenye vilele vyenye barafu hupamba nchi hii yenye kupendeza. Ni makao ya mamilioni ya kongoni na vifaru walio katika hatari ya kutoweka. Pia mtu anaweza kuona twiga wengi wakitembea kwenye mbuga.

Pia, ndege warukao angani ni wengi, kuanzia tai wenye nguvu wapaao, hadi maelfu ya ndege waimbao wenye rangi za kupendeza wanaotoa sauti tamu na nyimbo zenye kuchangamsha. Na ni nani awezaye kukosa kuwaona ndovu na simba? Huwezi kusahau vitu uvionavyo na sauti usikiazo nchini Kenya.

Lakini, kuna sauti nyingine isikikayo kote katika nchi hii yenye kupendeza. Ni sauti ya maelfu watangazao ujumbe wa tumaini. (Isaya 52:7) Sauti hizo zafikia watu kutoka kwenye makabila na lugha zaidi ya 40. Kwa hiyo, Kenya ni nchi yenye uzuri wa kiroho pia.

Watu wengi wa Kenya wanapenda dini nao huwa tayari kuzungumzia mambo ya kiroho. Ijapokuwa hivyo, limekuwa jambo gumu kupata watu wa kuongea nao, kwa kuwa Kenya, kama vile nchi nyingine, imeanza kubadilika.

Hali ngumu za kiuchumi zimelazimisha wengi warekebishe hali yao ya maisha. Wanawake ambao kulingana na utamaduni wamekuwa wakifanya kazi nyumbani, sasa wanafanya kazi maofisini au barabarani ambako wanauza matunda, mboga, samaki, na vikapu vya kufumwa. Wanaume hufanya kazi za kuchosha kwa muda wa saa nyingi, ili kuruzuku familia zao. Hata watoto, mikono yao michanga ikiwa imebeba njugu-karanga zilizofungwa kwa karatasi na mayai ya kuchemshwa, wanatembea barabarani wakiuza bidhaa zao. Matokeo yamekuwa kwamba ni watu wachache wanaopatikana nyumbani mchana. Hali hiyo imelazimu watangazaji wa habari njema za Ufalme wafanye marekebisho fulani.

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalishauriwa kukazia uangalifu zaidi watu wasiokuwapo nyumbani, ambao wanafanya shughuli zao za kila siku, na vilevile marafiki, watu wa ukoo, wafanyabiashara, na wafanyakazi wenzi. Nao akina ndugu walifuata shauri hilo na wakazungumza na watu kila mahali ambapo wangeweza kupatikana. (Mathayo 10:11) Je, jitihada hiyo ya kupanua utumishi wao imekuwa na matokeo yoyote? Ndiyo! Ona mifano ifuatayo.

Watu wa Ukoo—Majirani Wetu wa Karibu Zaidi

Jiji kuu la Kenya, Nairobi, lina wakazi milioni tatu hivi. Upande wa mashariki wa jiji paliishi meja wa jeshi aliyestaafu ambaye kwa muda mrefu alikuwa hapendi Mashahidi wa Yehova hata ingawa kwa kushangaza, mwana wake mwenyewe alikuwa Shahidi. Februari moja ofisa huyo mstaafu alisafiri mwendo wa kilometa 160 kwenda nyumbani kwa mwana wake huko Bonde la Ufa jijini Nakuru. Wakati wa matembezi yake huko, mwana wake alimpa zawadi—kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.a Baba huyo aliikubali naye akaenda zake.

Aliporudi nyumbani kwake, ofisa huyo wa zamani alimpa mke wake kitabu hicho, naye akaanza kukisoma, bila kutambua kwamba kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pole kwa pole, kweli ya Biblia ikaanza kuvutia moyo wake, naye akaambia mume wake habari hiyo. Akitaka kudadisi tu, yeye pia akaanza kukisoma kitabu hicho. Walipogundua wachapishaji wa kitabu hicho, walikata kauli kwamba hawakuwa wameambiwa kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova. Waliwasiliana na Mashahidi wa sehemu hiyo, na funzo la Biblia likaanzishwa. Kwa kujisomea wenyewe kitabu hicho, walikuja kutambua kwamba kutumia na kuuza tumbaku si jambo linalopatana na Ukristo. (Mathayo 22:39; 2 Wakorintho 7:1) Bila kukawia, waliharibu sigareti zote zilizokuwa dukani mwao. Baada ya miezi kadhaa walistahili kuwa wahubiri wasiobatizwa, na punde wakabatizwa kwenye mkusanyiko wa wilaya.

Takataka Zatoa Kitu Chenye Thamani

Katika sehemu fulani za jiji kuu, kuna vijiji vyenye kuenea vilivyo na mamia ya maelfu ya watu. Huku, waweza kupata nyumba nyingi sana zilizojengwa kwa udongo, mbao, mabamba ya chuma, au mabati. Kazi inapopungua viwandani, watu hujitafutia kazi zao wenyewe. Wafanyakazi wa jua kali hufanya kazi kwa jasho kwenye jua, wakitengeneza makatambuga (malapa) ya magurudumu yaliyochakaa ya gari au taa za koroboi kutokana na mikebe iliyotupwa. Wengine huchokora rundo la takataka wakitafuta karatasi, mikebe, na chupa za kutengenezwa upya tena.

Je, takataka zaweza kutoa kitu cha thamani? Ndiyo! Ndugu mmoja akumbuka: “Mwanamume aliyeonekana kuwa mwenye nguvu, mchafu, na asiye nadhifu aliyebeba gunia kubwa la plastiki lililojaa magazeti yaliyotupwa aliingia kwenye uwanja wa Jumba la Kusanyiko. Baada ya kuniambia kwamba jina lake ni William, aliniuliza: ‘Una magazeti ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi?’ Nilikuwa na wasiwasi kidogo, nikajiuliza alikuwa na kusudi gani. Nilipomwonyesha nakala tano za Mnara wa Mlinzi, alitazama kila moja na kusema: ‘Nitayachukua yote.’ Nikiwa nimeshangaa, nilienda chumbani mwangu na kurudi na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.b Nilimwonyesha picha ya Paradiso na kumweleza kwamba sisi hujifunza Biblia na watu bila malipo. Kisha nikadokeza hivi: ‘William, kwa nini usije kesho, tuanze kujifunza?’ Alifanya hivyo!

“Jumapili moja alikuja mkutanoni kwa mara ya kwanza. Nilikuwa nikitoa hotuba ya watu wote siku hiyo. William alipoingia, alitazama wasikilizaji kwa haraka, akaniona kwenye jukwaa, kisha akatoka nje ya jumba upesi. Nilimwuliza baadaye kwa nini alifanya hivyo. Alijibu kwa haya: ‘Watu walikuwa safi sana. Nikaogopa.’

“William alipoendelea na funzo lake, kweli ya Biblia ilianza kubadili maisha yake. Alioga, akakata nywele zake, akavaa nguo safi na nadhifu, na akaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Wakati kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele kilipotolewa, tukaanza kujifunza hicho. Kufikia hapo, alikuwa ametoa hotuba mbili katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na akawa mhubiri asiyebatizwa. Nilisisimka sana kumkaribisha akiwa ndugu yangu wa kiroho alipobatizwa kwenye siku ya kusanyiko la pekee.”

William alikuwa ameona wapi kwa mara ya kwanza thamani ya gazeti Mnara wa Mlinzi? “Nilipata matoleo fulani miongoni mwa karatasi zilizotupwa kwenye takataka.” Naam, alipata kitu cha thamani katika njia hiyo isiyo ya kawaida!

Kuhubiri Kazini

Je, sisi huwa macho sikuzote kupata fursa za kuhubiri mahali tunapofanya kazi? James, mzee katika kutaniko moja la Nairobi, alipata kweli ya Biblia kupitia njia hiyo. Kisha, amekuwa mwenye ustadi katika kutumia njia hiyo kufikia wengine. Kwa mfano, katika pindi moja, James aliona mfanyakazi mwenzake akija ofisini akiwa amevaa beji yenye maneno “Yesu Huokoa.” Akimwiga mweneza-evanjeli Filipo, James alimwuliza mfanyakazi mwenzake hivi: “Kwa kweli unaelewa maana ya maneno hayo?” (Matendo 8:30) Swali hilo lilifungua njia ya mazungumzo mazuri. Funzo la Biblia lilianzishwa, na mtu huyo akabatizwa baadaye. Je, James amefanikiwa kuhubiria wengine? Mwache aeleze:

“Mimi na Tom tulikuwa tukifanya kazi katika kampuni moja. Mara nyingi tulisafiri kwenye basi la kazini pamoja. Asubuhi moja, tulikuwa tumeketi pamoja. Nilikuwa nikisoma kimojawapo cha vitabu vyetu, nami nikakishikilia kwa njia ambayo nilihakikisha kwamba Tom angekitazama. Kama tu nilivyotumainia, Tom alivutiwa, nami nilifurahi kumwazima kitabu changu. Alipendezwa sana na yale aliyosoma na kukubali funzo la Biblia. Sasa yeye na mke wake ni watumishi wa Yehova waliobatizwa.”

James aendelea: “Mara kwa mara wakati wa pumziko la chakula cha mchana kwenye kampuni yetu, kuna mazungumzo yenye kupendeza sana. Wakati huo ndipo nilipokutana na Ephraim na Walter katika pindi tofauti-tofauti. Wote walijua kuwa mimi ni Shahidi. Ephraim alitaka kujua ni kwa nini kulikuwa upinzani mwingi dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Walter alitaka kujua tofauti kati ya Mashahidi na dini zile nyingine. Wote waliridhika sana na majibu ya Maandiko niliyowapa na wakakubali kujifunza. Ephraim alifanya maendeleo ya haraka. Baada ya muda, yeye na mke wake walijiweka wakfu kwa Yehova. Sasa yeye anatumikia akiwa mzee, na mke wake ni painia wa kawaida. Hata hivyo, Walter, alikabili upinzani mkali sana mpaka akatupa kitabu chake cha kujifunza. Ingawa hivyo kwa sababu ya kusisitiza kwangu, alianza kujifunza tena. Sasa yeye pia anafurahia pendeleo la kutumikia akiwa mzee.” Kwa ujumla, watu 11 wamekuwaWakristo wa kweli kwa sababu James alitumia fursa za mahubiri ya vivi hivi kazini.

Matokeo ya Kustaajabisha Zaidi

Katika kijiji kidogo ufukoni mwa Ziwa Victoria, marafiki na watu wa ukoo walikusanyika kwenye maziko. Shahidi mmoja mzee-mzee alikuwa miongoni mwa waombolezaji. Alimwendea mwalimu wa shule anayeitwa Dolly na kumweleza hali ya wafu na kusudi la Yehova la kuondoa kifo milele. Alipoona itikio lake zuri, ndugu huyo alimhakikishia hivi: “Unaporudi kwenu, mmoja wa mishonari wetu atakutembelea na kukufunza Biblia.”

Jiji la nyumbani kwa Dolly ni la tatu kwa ukubwa nchini Kenya. Wakati huo ni mishonari wanne tu Mashahidi waliokuwa huko. Kwa kweli ndugu huyo mzee-mzee hakujulisha mishonari yeyote kwenda kumtembelea Dolly. Alikuwa na uhakika tu kwamba ingetokea hivyo. Na ndivyo ilivyokuwa! Baada ya muda mfupi, dada mmoja mishonari alikutana na Dolly naye akaanza kujifunza naye. Sasa Dolly amebatizwa, binti yake mchanga amejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na wana wake wawili pia wamebatizwa. Pia amepata shangwe ya kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia.

Kushughulikia Ongezeko

Kukaziwa kwa mahubiri ya vivi hivi kumewezesha maelfu wengi kusikia habari njema Kenya. Zaidi ya wahubiri 15,000 sasa wana bidii katika kazi hii ya maana zaidi, na zaidi ya watu 41,000 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mwaka uliopita. Nchini Kenya, hudhurio la mikutano mara nyingi ni maradufu ya wahubiri wa Ufalme. Hilo limefanya kuwe na uhitaji wa Majumba ya Ufalme zaidi.

Majumba ya Ufalme yanajengwa katika majiji makubwa na katika sehemu za mashambani. Moja ya sehemu hizo ni mji wa Samburu ulioko karibu kilometa 320 kaskazini-mashariki mwa Nairobi. Mwaka wa 1934 mji huo ukaitwa Maralal, maana yake “kumetameta” katika Kisamburu, kwa sababu paa la kwanza la mabati lililojengwa huko liling’aa juani. Miaka 62 baadaye, jengo jingine lenye paa la mabati lilijengwa Maralal. Hilo pia “hung’aa” na “kumetameta” kwa sababu ni mahali pa ibada ya kweli.

Wahubiri 15 walijitahidi zaidi kujenga Jumba la Ufalme la kwanza sehemu hii ya mbali ya Kenya. Fedha hazikutosha, kwa hiyo iliwabidi akina ndugu wategemee vifaa vilivyopatikana huko. Walitengeneza kuta kwa udongo mwekundu uliofanywa laini kwa maji na kukandikwa vizuri kwenye miti iliyosimamishwa wima. Kuta zililainishwa na kupigwa plasta kwa mchanganyiko wa samadi ya ng’ombe na majivu, yaliyozifanya ziwe ngumu na kudumu kwa miaka mingi.

Ili kupata vigingi vya kujengea, akina ndugu walichukua kibali cha kukata miti. Lakini msitu uliokuwa karibu ulikuwa umbali wa kilometa kumi. Ilibidi akina ndugu na dada watembee msituni, wakate miti, waisawazishe, na kuibeba hadi mahali pa ujenzi. Wakati mmoja, walipokuwa wakitembea kutoka porini, ndugu hao walisimamishwa na polisi, ambaye alidai kwamba muda wa kibali chao ulikuwa umekwisha. Polisi alimwambia painia mmoja wa pekee kwamba amekamatwa kwa sababu ya kukata miti. Dada mmoja wa hapo ambaye anajulikana sana na jamii na polisi, alisema kwa sauti: “Ukimkamata ndugu yetu, lazima utukamate sote, kwa kuwa sisi sote tulikata miti!” Ndipo ofisa huyo akawaacha wote waende zao.

Kulikuwako wanyama wa mwitu msituni, kwa hiyo ilikuwa hatari kutembea huko. Siku moja dada alikata mti. Mti huo ulipoanguka chini, aliona mnyama akiruka na kukimbia. Aliona kwa haraka rangi ya kikahawia akafikiri alikuwa ameona swalapala, lakini baadaye alitambua kutokana na alama za miguu kuwa alikuwa simba! Zijapokuwa hatari hizo, akina ndugu walikamilisha jumba, nalo “lametameta” likiwa mahali panapomletea Yehova sifa.

Februari 1, 1963, ilikuwa siku ya maana zaidi katika historia ya kitheokrasi ya Kenya. Siku hiyo ofisi ya tawi ya kwanza ilifunguliwa, chumba kimoja tu chenye ukubwa wa meta mraba 7.4. Oktoba 25, 1997, kulikuwa na tukio jingine muhimu katika historia ya kitheokrasi ya Kenya—kuwekwa wakfu kwa majengo ya Betheli mapya yenye ukubwa wa meta mraba 7,800! Mradi huo uliokamilishwa ulikuwa umalizio wa kazi ngumu ya kujitolea ya miaka mitatu. Wajitoleaji kutoka nchi tofauti-tofauti 25 waligeuza uwanja uliokuwa umejaa udongo, na magugu, wenye ukubwa wa eka 7.8 kuwa mahali penye kupendeza pa majengo mapya ya ofisi ya tawi, yenye kuandaa makao kwa washiriki 80 wa familia ya Betheli.

Tuna sababu nzuri za kushangilia yale ambayo Yehova amefanyia watu wake. Anastahili sifa kwa sababu ya kuchochea mioyo ya watumishi wake kupanua na kuzidisha jitihada za kutafuta watu wanaostahili nchini Kenya, ikiifanya kuwa nchi yenye uzuri wa kiroho.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki