Masimulizi Yanayochochea Imani na Ujasiri Mashahidi wa Yehova Nchini Ukrainia
LEO watu wa Mungu hunyanyaswa kama vile Wakristo wa karne ya kwanza walivyonyanyaswa. (Mathayo 10:22; Yohana 15:20) Lakini si nchi nyingi ambazo zimekuwa na mnyanyaso mkali na ulioendelea kwa muda mrefu kama nchi ya Ukrainia, ambako kwa miaka 52 kazi ya kuhubiri Ufalme ilikuwa imepigwa marufuku.
Kitabu 2002 Yearbook of Jehovah’s Witnesses kinasimulia mambo yaliyowapata watu wa Mungu katika nchi hiyo. Kitabu hicho kinasimulia kuhusu imani, ujasiri, na nguvu ambazo watu hao walionyesha chini ya hali ngumu sana. Yafuatayo ni baadhi ya maelezo ya uthamini yaliyopokewa na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Ukrainia:
“Nimemaliza kusoma kitabu 2002 Yearbook. Nililia niliposoma kuhusu kazi yenu nchini Ukrainia. Ningependa kuwaambia jinsi nilivyotiwa moyo na kielelezo chenu cha bidii na imani yenu yenye nguvu. Ninajivunia kuwa katika familia ileile ya kiroho pamoja nanyi. Ninawashukuru kwa moyo wangu wote!”—Andrée, Ufaransa.
“Sina maneno yanayoweza kuelezea shukrani zangu kwenu na kwa Yehova kwa ajili ya kitabu 2002 Yearbook. Nililia niliposoma mambo mbalimbali yaliyowapata akina ndugu ambao walitumia miaka yao ya ujana gerezani na katika kambi za mateso. Ninavutiwa na ujasiri wao. Ingawa nimekuwa Shahidi kwa miaka 27, bado ninaweza kujifunza kutoka kwa ndugu na dada hao. Waliimarisha imani yangu katika Baba yetu wa mbinguni, Yehova.”—Vera, Yugoslavia ya zamani.
“Ninaandika barua hii kwa furaha kwa sababu ya kielelezo chenu kizuri cha uvumilivu na uaminifu wakati wa miaka hiyo yote ya upinzani. Tumaini lenu kamili kwa Yehova na azimio lenu la kudumisha uaminifu linawaletea heshima. Isitoshe, unyenyekevu wenu chini ya majaribu huimarisha imani yangu kwamba Yehova hawaachi watu wake. Kwa sababu ya kielelezo chenu kizuri cha ujasiri, uthabiti, na ustahimilivu, tunaweza kukabiliana na matatizo yetu madogo kwa urahisi zaidi.”—Tuteirihia, Polynesia ya Ufaransa.
“Baada ya kusoma kitabu Yearbook, ilinibidi niwaandikie. Niliguswa moyo sana na mambo yote yaliyowapata ndugu hao ambayo yanatia moyo sana. Ninajivunia kuwa mshiriki wa tengenezo lenye uaminifu na umoja, linaloongozwa na Baba mwenye upendo na mwenye kutujali, ambaye hututia nguvu wakati unaofaa. Nilihuzunika kwamba watumishi wengi wa Yehova wenye bidii na ujasiri waliteseka sana na hata wakafa. Lakini pia nilifurahi kwamba kwa sababu ya ujasiri na bidii ya ndugu hao, watu wengi sana walijifunza ukweli na kumjua Baba yetu mwenye upendo.”—Colette, Uholanzi.
“Ilinibidi mimi na mke wangu kuwaandikia ili kuwaeleza kwamba tuliguswa moyo tuliposoma masimulizi kuhusu Ukrainia katika Yearbook. Nyinyi ndugu waaminifu mmeweka kielelezo bora cha uvumilivu chini ya majaribu makali yaliyoendelea kwa muda mrefu. Kupatana na maneno ya Mithali 27:11, ni lazima Yehova awe anafurahi sana kujua kwamba ndugu wengi waaminifu wa Ukrainia wamedumisha uaminifu-maadili ijapokuwa matendo yote maovu ya Ibilisi.”—Alan, Australia.
“Macho yangu yalijaa machozi niliposoma kuhusu ndugu wa Ukrainia. Walivumilia mambo mengi sana—kuteswa gerezani kwa miaka mingi, kukandamizwa, na kutenganishwa na familia. Ningependa kuwaambia ndugu wote ambao bado wanatumikia katika makutaniko yenu kwamba ninawapenda na kuwaheshimu sana. Ujasiri na uthabiti wao unanifurahisha sana. Ninajua kwamba wanatiwa nguvu na roho ya Yehova. Yehova yu karibu nasi naye anataka kutusaidia.”—Sergei, Urusi.
“Nilisoma kitabu 2002 Yearbook na kulia. Ndugu na dada wengi katika kutaniko letu wamezungumza juu yenu. Tunawathamini sana. Ninafurahi sana kuwa mshiriki wa familia kubwa ya kiroho kama hiyo.”—Yeunhee, Korea Kusini.
“Nimeguswa moyo sana na imani, uvumilivu, na upendo wenu thabiti kwa Yehova na Ufalme wake. Nyakati nyingine tunakosa kuthamini uhuru tulio nao na chakula kingi cha kiroho ambacho Yehova hututolea. Lakini nyinyi mmekuwa wenye uthamini. Kielelezo chenu cha imani hutusaidia kutambua kwamba tukiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wetu, atatutia nguvu kukabiliana na majaribu ya kila aina.”—Paulo, Brazili.
“Nilipata pendeleo la kusoma mambo yaliyowapata katika kitabu 2002 Yearbook. Niliguswa moyo sana, hasa na mambo yaliyompata Dada Lydia Kurdas. Nilivutiwa sana na dada huyo.”—Nidia, Kosta Rika.
“Leo nilimaliza kusoma kitabu 2002 Yearbook. Nilipokuwa nikikisoma, imani yangu katika Yehova iliimarishwa. Sitasahau kamwe simulizi juu ya mbegu za shaka zilizopandwa kuhusu wale wenye kuongoza. Simulizi hilo lilinifunza kwamba sipaswi kamwe kutilia shaka akina ndugu wenye kuongoza. Asanteni sana! Chakula hiki cha kiroho kinatia moyo na hututayarisha kwa ajili ya wakati ambapo imani yetu inaweza kujaribiwa.”—Leticia, Marekani.
“Tunashukuru sana kwa kitabu hicho bora cha Yearbook. Wahubiri wengi walisoma kwa mara ya kwanza kuhusu kazi ya ndugu zetu nchini Ukrainia. Ndugu wa hapa waliimarishwa sana. Wengi, hasa kati ya vijana wamepanua utumishi wao. Baadhi yao wameanza upainia wa kawaida au msaidizi. Wote walitiwa moyo na masimulizi kuhusu ndugu na dada waliomtumikia Yehova wakati wa marufuku.”—Halmashauri moja ya utumishi ya kutaniko, Ukrainia.
Naam, uaminifu wa ndugu zetu nchini Ukrainia umewatia moyo watu wa Yehova duniani pote. Kwa kweli, kusoma kwa ukawaida masimulizi yenye kuchangamsha moyo ambayo yanapatikana katika kitabu Yearbook kila mwaka ni njia bora ya kuimarisha imani na uvumilivu wetu katika nyakati hizi muhimu.—Waebrania 12:1.