Wafundishe Watoto Wako
Shemu Aliona Kizazi cha Kabla na Baada ya Gharika
SHEMU, mwana wa Noa, aliokoka mwisho wa ulimwengu mmoja na kuishi katika ulimwengu mwingine. Je, unajua kwa nini ulimwengu wa kwanza ambao Shemu aliishi uliharibiwa na jinsi yeye na familia yake walivyookoka na kuishi katika ule uliofuata?—a Acha tuzungumzie jambo hilo.
Shemu alipokuwa kijana Biblia inasema kwamba “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi.” Fikira za watu zilikuwa “mbaya tu wakati wote.” Kwa hiyo, unajua Mungu alifanya nini?— Alileta gharika iliyouangamiza ulimwengu huo mwovu. Mtume Petro aliandika hivi: “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.”—Mwanzo 6:5; 2 Petro 3:6.
Je, umeelewa kwa nini Mungu aliuharibu ulimwengu huo?— Wanadamu walikuwa wabaya na walifikiria mambo ‘mabaya kila wakati.’ Yesu alizungumza kuhusu jambo hilo. “Kabla ya gharika,” alisema, watu walikuwa “wakila na kunywa” na pia “wakioa na . . . wakiolewa.” Yesu aliongezea hivi: “Hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:37-39.
Watu hao hawakujali au kuona nini?— Noa, baba ya Shemu, alikuwa “mhubiri wa uadilifu,” lakini watu hawakusikiliza mambo aliyokuwa akisema. Noa alimsikiliza Mungu na akajenga safina, chombo kinachoweza kuelea, ambacho kingemlinda yeye na familia yake wakati wa Gharika. Ni Noa tu, mke wake na wana wao—Shemu, Hamu, na Yafethi—na wake zao waliofanya mambo ambayo Mungu aliwataka wafanye. Watu wale wengine walifanya kile ambacho wao wenyewe walitaka kufanya, kwa hiyo wakaangamizwa na Gharika.—2 Petro 2:5; 1 Petro 3:20.
Mwaka mmoja hivi baadaye, Shemu na familia yake walitoka kwenye safina na kuanza kuishi kwenye nchi kavu. Watu wote wabaya walikuwa wameharibiwa, lakini mambo yalibadilika upesi. Kanaani, mwana wa Hamu, ndugu ya Shemu, alifanya jambo baya sana hivi kwamba Noa akasema: “Alaaniwe Kanaani.” Nimrodi, mjukuu wa Hamu, alikuwa mbaya pia. Alimpinga Yehova, Mungu wa kweli, na kuwaambia watu wajenge mnara mrefu unaoitwa Babeli ili wajifanyie jina. Unafikiri jambo hilo lilimfanya Shemu na baba yake wahisi namna gani?—Mwanzo 9:25; 10:6-10; 11:4, 5.
Walihuzunika, na Yehova pia alihuzunika. Je, unajua Yehova alifanya nini?— Alivuruga lugha ya watu ili wasielewane. Kwa hiyo, watu walilazimika kuacha kujenga. Kila kikundi kilielekea sehemu tofauti ikitegemea walizungumza lugha gani. (Mwanzo 11:6-9) Lakini Mungu hakubadili lugha ya Shemu na familia yake. Kwa sababu hiyo waliweza kuishi pamoja na kusaidiana kumtumikia Mungu. Je, umewahi kujiuliza Shemu alimtumikia Yehova kwa miaka mingapi?—
Shemu aliishi kwa miaka 600. Aliishi miaka 98 kabla ya Gharika na miaka 502 baada ya Gharika. Tunaweza kuwa na hakika kwamba alimsaidia Noa kujenga safina na kuwaonya watu kuhusu Gharika iliyokuwa ikija. Lakini unafikiri Shemu alikuwa akifanya nini kwa zaidi ya miaka 500 aliyoishi baada ya Gharika?— Noa alimtaja Yehova kuwa “Mungu wa Shemu.” Lazima Shemu awe aliendelea kumtumikia Yehova na kuwasaidia watu wa familia yake wafanye vivyo hivyo. Baadaye, familia ya Shemu ikaja kutia ndani Abrahamu, Sara, na Isaka.—Mwanzo 9:26; 11:10-31; 21:1-3.
Fikiria kuhusu ulimwengu wa leo ambao umezidi kuwa mwovu tangu siku za Shemu. Ulimwengu huu utapatwa na nini?— Biblia inasema kwamba “unapitilia mbali.” Lakini ona ahadi hii: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” Kwa hiyo, tukifanya mapenzi ya Mungu, huenda tukawa kati ya wale watakaookoka na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Kisha, kwa msaada wa Mungu tunaweza kuishi milele duniani kwa furaha!—1 Yohana 2:17; Zaburi 37:29; Isaya 65:17.
[Maelezo ya chini]
a Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.
Maswali:
○ Shemu aliishi katika ulimwengu wa aina gani kwanza, na ni sababu gani mbili zilizomfanya Mungu aharibu ulimwengu wa wakati huo?
○ Shemu aliishi kwa muda gani, na alikuwa mtu wa aina gani?
○ Ulimwengu huu utapatwa na nini hivi karibuni?
○ Tunapaswa kufanya nini ili tuokoke mwisho wa ulimwengu huu?