Hawaogopi Mwisho Tena
MWISHONI mwa miaka ya 1970, Gary na Karen walisadiki kwamba mwisho wa ulimwengu umekaribia. Kwa hiyo, walitoka jijini na kuhamia mashambani, na wakaamua kujiandalia mahitaji yao bila kutegemea huduma zozote za jamii. Walitaka kuokoka mwisho.
Ili wapate ustadi ambao wangehitaji, walinunua vitabu, wakahudhuria madarasa na mikutano, na wakaongea na watu wengi iwezekanavyo ili kupata mashauri. Walianza kulima shamba dogo na wakapanda miti 50 ya matunda. Waliweka akiba ya mbegu na vifaa mbalimbali. Walijifunza jinsi ya kuzalisha na kuhifadhi vyakula. Rafiki yao mmoja aliwafundisha jinsi ya kuchinja wanyama na kuhifadhi nyama. Karen alijifunza kutambua mimea na mizizi msituni ambayo wangeweza kuila ikiwa vyakula walivyokuwa navyo akibani vingeisha. Gary alijifunza jinsi ya kutumia mahindi kama chanzo cha nishati, kutengeneza jiko la kuni, na kujenga nyumba isiyotegemea huduma za jamii kwa ajili ya umeme, maji, na kadhalika.
Karen anasema: “Niliamini kwamba ustaarabu ungeisha baada ya muda mfupi, kwa sababu hali za ulimwengu zilikuwa mbaya sana wakati huo.” Gary naye anaeleza: “Kama vijana wengine, nilijiunga na vikundi vya wanaharakati ili kujaribu kukomesha ubaguzi wa rangi, Vita vya Vietnam, na ufisadi. Lakini nilikata tamaa upesi. Ilionekana kama wanadamu wangejiangamiza ikiwa hali zingeendelea kuzorota.”
Gary anasema: “Jioni moja sikuwa na shughuli nyingi, hivyo, nilichukua Biblia na nikasoma kuanzia Mathayo mpaka Ufunuo. Katika siku nne zilizofuata, nilisoma sehemu hiyo tena polepole. Asubuhi ya siku ya tano, nilimwambia Karen hivi: ‘Tunaishi katika siku za mwisho. Baada ya muda mfupi, Mungu atachukua hatua ili kusafisha dunia. Tunahitaji kuwatafuta wale watakaookoka.’” Gary na Karen walitembelea kanisa moja baada ya lingine, wakitafuta watu waliotaka kujitayarisha ili kuokoka mwisho.
Punde si punde, Shahidi wa Yehova aliwatembelea, na wakaanza kujifunza Biblia. Karen anasema: “Nilisisimka sana, kwa sababu alieleza Maandiko kwa njia ambayo niliweza kuelewa. Hatimaye, nilielewa ukweli kuhusu siku za mwisho, jambo nililokuwa nikitaka kujua. Nilielewa kwamba kuna tumaini hakika la wakati ujao. Lakini jambo bora hata zaidi ni kwamba nilianza kujenga urafiki pamoja na Baba yangu wa mbinguni, Mungu aliyeumba ulimwengu.”
Gary anasema: “Nilielewa kusudi la maisha yangu. Nilipoanza kujifunza Biblia sikuweza kuacha. Nilisoma kuhusu mambo ambayo Biblia imetabiri, nikachunguza uthibitisho ili kuona kama mambo hayo yanatimia, na hivyo nikasadikishwa kwamba hivi karibuni Mungu atachukua hatua. Niliwaza, ‘Watu hawapaswi kujitayarisha kwa ajili ya msiba, bali kwa ajili ya maisha ambayo Mungu ametuahidi.’” Maoni ya Gary na Karen kuhusu wakati ujao yalibadilika. Badala ya kuwa na wasiwasi kuhusu mwisho wa ulimwengu, sasa wana hakika kwamba Mungu ataondoa matatizo yanayosumbua wanadamu na kufanya dunia iwe paradiso.
Gary na Karen wanafanya nini sasa, miaka 25 hivi baadaye? Karen anasema: “Ninaendelea kusitawisha upendo kwa Yehova Mungu na kujenga imani yangu, na ninajitahidi kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo. Mimi na Gary tunasaidiana ili familia yetu iwe imara na yenye umoja tunapoendelea kumwabudu Mungu. Tunajaribu kuwa na utaratibu na kutosheka na mambo ya lazima ya maisha ili tuwe na nafasi ya kuwafikiria na kuwasaidia wengine.”
Gary anaongeza: “Mara nyingi ninaomba Ufalme wa Mungu uje ili mamilioni ya watu wapate kitulizo. Kila ninapohubiri habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu, ninasali kwamba niweze kuonyesha angalau mtu mmoja tumaini la Biblia. Kwa zaidi ya miaka 25, Yehova amejibu sala yangu kwa fadhili. Mimi na Karen tunaamini kwamba hivi karibuni Yehova ataleta mabadiliko makubwa duniani, lakini hatuogopi mwisho tena.”—Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:11, 12.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Sasa Gary na Karen wanafurahia kuwasaidia wengine kupata tumaini kwa kuwahubiria ujumbe wa Biblia