Fanya Mikutano Iwe Yenye Kufundisha Zaidi
1 “Jambo moja lililonivutia ni kwamba wachanga na wazee walishiriki katika mikutano kwenye Jumba la Ufalme kwa kutoa maelezo na kufungua maandiko.” Je! wewe umepata kusikia mtu akisema hivyo kuhusu mkutano wa kwanza aliohudhuria wa Mashahidi wa Yehova? (1 Kor. 14:25b) Wengi wetu tumesikia maneno kama hayo. Na jinsi tulivyokuwa wenye furaha kuwa tulihudhuria mikutano hiyo na kushiriki katika kutoa maelezo!
2 Tunapotayarisha mapema, maelezo yetu yanakuwa yenye maana zaidi, na mikutano inakuwa yenye kufundisha zaidi na kunufaisha wote wanaohudhuria. (Ebr. 10:24, 25) Jambo hili lapasa likazie akilini na mioyoni mwetu umuhimu wa kazi ambazo zinalingana na imani. Hilo litatusaidia sisi kufanya maendeleo katika maisha na utendaji wa Kikristo.—Yak. 1:25.
TUWAPO JUKWAANI
3 Habari mbalimbali zinazungumziwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Akina dada wanapokea migawo katika vitabu Kuishi Milele na Reasoning, vyote viwili vikiwa vitabu tunavyotumia kwa ukawaida katika huduma yetu ya shambani. Wale ambao wanapata migawo hii wanaweza kufanya shule iwe yenye kufundisha zaidi kwa kutumia vikao vinavyofaa ili kutoa mambo ya msingi yaliyo katika habari. Jambo hili litawasaidia wasikilizaji wathamini habari ile na waone jinsi wanavyoweza kuitumia katika huduma ya shambani. Akina ndugu ambao wana hotuba zinazotegemea kitabu Reasoning wanaweza vivyo hivyo kukazia mambo makuu ambayo yatakuwa yenye msaada sana wakati wa kutoa ushuhuda katika eneo la kwenu. Akina ndugu wanaoshughulikia migawo ya kusoma Biblia wanaweza kufanya tangulizi zao, maelezo yanayohusiana na usomaji, na umalizio uwe wenye maana kwa kukazia mambo makuu yenye thamani inayofaa. Labda kwa mojapo ya njia hizi wewe unaweza kufanya shule iwe yenye kufundisha zaidi kwa wote wanaohudhuria.
4 Huenda sisi tukaulizwa tushiriki kutoa wonyesho katika Mkutano wa Utumishi. Ikiwa hivyo, ni jambo la muhimu kujitayarisha. Tunayosema yapasa kusikika, kwa hiyo tunahitaji kutumia maikrofoni inavyofaa. (Linganisha 1 Wakorintho 14:9.) Tunaposhiriki kutoa maonyesho, usiwageuzie wasikilizaji wako mgongo. Sikuzote watazame wasikilizaji. Hivyo, wakati tunapomwonyesha mwenye nyumba mambo yaliyomo kwenye kichapo, wasikilizaji wataona jalada la kichapo. Tunapowatazama wasikilizaji, wao wanaweza kutusikia sisi waziwazi na kuangalia uso wetu.
TUKIWA WASIKILIZAJI
5 Sisi tulio wasikilizaji tunaweza kufanya mikutano iwe yenye kutufundisha zaidi kwa kukaza fikira sana. (1 Tim. 4:16; Ebr. 2:1) Wote wanahitaji kukuza ustadi wa kusikiliza, si kuacha akili zetu zitange-tange. Kunong’onezea wengine ambao wameketi kando yetu ni jambo lenye kuondosha fikira. Kuondoka-ondoka bila uhitaji wa kufanya hivyo ili kwenda msalani au kunywa maji pia kutakatiza kupata kwetu faida ya mikutano na kutaondosha fikira za wengine pia.
6 Ikiwa sisi tuna watoto wadogo nao ni watukutu, huenda tukapenda kuketi karibu na uchochoro (ujia kati ya viti na viti) kuelekea upande wa nyuma wa Jumba la Ufalme ili wasisumbue wengi wa wasikilizaji. Ikiwa wao wanakosa adabu au wanafanya kelele, ni jambo linalofaa wazazi wawatoe nje ya sehemu kubwa ya kuketi katika Jumba la Ufalme. La sivyo, wao wataendelea kutatiza fikira za wengine ambao wanajaribu kuelekeza fikira kwenye mikutano.—Mit. 22:6, 15.
7 Ikiwa tunajitahidi kufanya mikutano iwe yenye kufundisha zaidi kwetu na pia kwa wengine sisi sote tutasaidiwa tukue kiroho. Kisha itasemwa hivi juu yetu sisi, kama ilivyosemwa kwa Wakristo wa Thesalonike, kwamba “imani [yetu] inazidi sana, na upendo wa kila mtu [wetu] kwa mwenzake umekuwa mwingi.”—2 The. 1:3.