Kutoa Habari Njema—Kwa Magazeti
1 Chakula cha kiroho kwa wakati wake. (Mt. 24:45) Shauri na miongozo yenye kutumika ili kuyaweza matatizo ya leo. Mazungumzo ya habari nyingi zinazohusu watu, nchi, dini na sayansi huyafanya yawe yenye kuarifu na kuelimisha. Yanaangalia matukio ya ulimwengu yanapotimiza unabii wa Biblia. Hayo ni maelezo machache yanayokazia thamani ya magazeti yetu. Baada ya kupata manufaa za kibinafsi kutoka Mnara wa Mlinzi na Amkeni! sisi tunataka kufanya kila jitihada kutia magazeti haya mazuri ajabu mikononi mwa majirani wetu ili ‘kuwapa wakati ujao na tumaini.’—Yer. 29:11.
YAJUE MAGAZETI YAKO
2 Twaweza kusadikishaje mtu kwamba atanufaika kwa kusoma magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!? Njia bora ni kumwonyesha mtu huyo jambo hususa ambalo laweza kuwa lenye kumpendeza na lenye kumfaa. Uwe tayari kujirekebisha na kupatanisha makala na gazeti unalopanga kutumia ikiwa maoni, kupendezwa, nia na hali ya mwenye nyumba hutaka hivyo. Kufanya hivyo kwa mafanikio kwataka kwamba sisi tufahamiane kikamili na magazeti na kujitayarisha kimbele. Kujitayarisha huko kwaanza na kusoma sisi binafsi magazeti hayo kabla ya kuyatumia shambani. Uyasomapo, uwe chonjo kuona mambo ambayo ungeweza kutumia katika huduma. Kwa nini usitie alama mambo hayo katika nakala zako mwenyewe za magazeti hayo na kisha urudie mambo uliyotia alama unapojitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani kwa toleo hilo? Usielekeze tu kwenye picha juu ya jalada la mbele na makala kuu, bali pia, angalia makala nyinginezo kama vile mfululizo wa “Vijana Wauliza . . . ” au habari chini ya “Maoni ya Biblia.”
3 Unapofanya usomaji wa binafsi wa magazeti yetu ni vizuri pia kufikiria makala zitakazopendeza kipekee watu fulani katika eneo lenu. Waweza kuanza kwa kufikiria makala moja itakayovutia watu katika kila mojawapo vikundi hivi: wanaume, wanawake, na vijana. Kisha fikiria kama kuna makala ambazo zingeweza kuwapendeza kipekee madaktari, walimu na kadhalika. Hata waweza kufanya orodha ya watu mmoja mmoja ambao wataka kuwatolea magazeti hayo.
SITAWISHA STADI ZAKO
4 Yaonekana ni vizuri zaidi kuwa na utangulizi mfupi katika utoaji wako, uwe wa kupendeza na wenye kuhusiana na makala unayotaka kuonyesha. Ili kutimiza hilo uliza swali linalojibiwa katika makala hiyo na kusoma sentensi moja au mbili kutoka fungu hususa linaloshughulika na jambo hilo. Usiongee kwa haraka mno, na usiongee mengi mno. Sema polepole na kuonyesha kupendezwa kibinafsi na mwenye nyumba. Onyesha jinsi gazeti hilo linavyomhusu mwenye nyumba na jinsi familia nzima italifurahia. (Flp. 2:4) Utoaji wote waweza kuwa mfupi na kulenga maana, usichukue zaidi ya dakika moja au mbili.
5 Ingawa utaonyesha habari hiyo moja tu, inayotegemezwa na makala moja katika gazeti hilo moja tu, hakikisha katika kumalizia kutoa magazeti yote mawili, si moja tu. Jaribu kuepuka kutoa gazeti moja tu kwa wakati mmoja. Mpe mwenye nyumba fursa ya kuona lile gazeti mwenzi ambalo halikuonyeshwa katika utoaji huo hususa. Mwenye nyumba akionyesha kupendezwa katika gazeti hilo uwe tayari kukazia makala hususa ambayo wahisi itampendeza.
FIKIRIA MAGAZETI
6 Tenga angalau siku moja kila juma, ama Jumamosi au siku ya soko, ili kushiriki katika kutoa ushuhuda kwa magazeti. Kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba kwa magazeti katika siku ya magazeti kwa kawaida hutaka eneo zaidi kwa kuwa utoaji wetu kwa ujumla ni mfupi sana. Kwa hiyo, mwangalizi wa utumishi na kiongozi wa funzo la kitabu watataka kuwa na kiasi cha eneo kinachotosha kwa ajili ya kikundi. Makundi yaliyo mengi kwa kawaida hupata kwamba kufanyia maeneo kazi kwa zamu kwa ushuhuda wa magazeti na wa toleo la fasihi huwa na matokeo mazuri sana. Kwa hiyo kwa kadiri itumikavyo, maeneo moja moja yaweza kufanyiwa kazi wakati mmoja kwa magazeti tu na ule wakati mwingine kwa toleo la kawaida. Siku ya kutoa ushuhuda kwa magazeti hukazia kufikia watu wengi zaidi tukiwa na kweli. Kwa ujumla hiyo ndiyo sababu utoaji wetu huwa mfupi na wenye kulenga maana yenyewe. Hivyo usisite kushiriki utendaji wa siku ya magazeti.
7 Madokezo zaidi machache: (1) Jiwekee mradi wa kibinafsi. Ukiwa mhubiri, je, waweza kuangusha, tuseme, magazeti 10 kwa mwezi? Mapainia waweza kujitahidi kufikia 90. (2) Wakati toleo la kawaida la fasihi lisipokubaliwa uwe chonjo kutoa magazeti. (3) Sikuzote beba magazeti tofauti-tofauti katika mkoba wako wa kutolea ushuhuda. (4) Uwe na magazeti kadhaa kwa fursa za kutoa ushuhuda wa vivi hivi. (5) Jitahidi kuwa na watu wa kupelekea magazeti kwa ukawaida.
8 Kweli kweli, Mnara wa Mlinzi na Amkeni! hutimiza fungu lenye nguvu nyingi katika kazi yetu ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote. Sisi ni wenye shukrani kwa kuwa Yehova ameyaandaa yatumiwe katika huduma. Yehova na aendelee kubariki matumizi yetu ya uangalifu na ya bidii ya majarida hayo!