Kutoa Habari Njema—Kuanza Mafunzo kwa Njia ya Moja kwa Moja
1 Yesu alituamuru ‘tufanye wanafunzi.’ (Mt. 28:19) Kutimiza hilo kwa kawaida hutaka kuanzisha mafunzo ya Biblia na wenye kupendezwa. Kutumia njia ya moja kwa moja kuanza mafunzo ya Biblia katika huduma ya nyumba kwa nyumba kwaweza kutusaidia tutimize jambo hilo kwa haraka. Pia kunatumika kutambulisha waziwazi kusudi kubwa la kuzuru.
2 Twaweza kusema nini tunapotumia njia ya moja kwa moja katika kuanza mafunzo ya Biblia? Njia rahisi sana ndio bora zaidi. Twaweza kusema: “Ninapendezwa na kusaidia watu waelewe Biblia na ningefurahia kuongoza funzo la Biblia kwa familia yako nyumbani kwako bila malipo au masharti yoyote. Tunaweza kutumia Biblia yako. Ikiwa huna moja, ninaweza kupanga upate moja.”
3 Njia nyingine yaweza kuwa: “Kusudi langu la kuzuru leo ni kukutia moyo uwe na funzo la Biblia, ambalo litakusaidia uelewe ulimwengu huu unaelekea wapi na yale ambayo Mungu ametuwekea katika wakati ujao. Ningefurahi kukuonyesha jinsi wewe ungeweza kupata faida kubwa zaidi kutokana na Biblia yako. Hakuna masharti au gharama kwako.” Mwenye nyumba akikubali, waweza kutumia trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani au kitabu Creation, labda ukianza na ukurasa wa 234, fungu la 6, au kitabu Kuishi Milele, labda ukianza na ukurasa wa 10, fungu la 11 mahali ambako kitabu Creation hakipatikani kwa lugha inayotumiwa katika eneo. Kurasa za mwanzo za sura hiyo hukazia ahadi ya Yehova ya kurudisha Paradiso.
4 Tumia Trakti za Biblia: Wengi wa- mepata trakti kuwa zenye kusaidia wanapotumia njia ya moja kwa moja. Mwenye nyumba afunguapo mlango, mpe trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani ikiwa imekunjuliwa ili aweze kuona kielezi chote. Uwe na trakti nyingine mkononi, na kusoma au kutaja kifupi swali katika mafungu mawili ya kwanza. Zungumza majibu, na kusoma andiko moja au mawili yanayotegemeza jibu. Ndipo utaje kwamba umefurahia mazungumzo, na kupanga urudi. Eleza kifupi programu yetu ya funzo la Biblia nyumbani, ikifaa, au upange tu utarudi na kuzungumza jambo moja zaidi katika trakti.
5 Unapopanga kurudi, ni vizuri kutaja jambo fulani unalohisi kwamba litampendeza mwenye nyumba. Hilo laweza kuwa kwa namna ya swali. Litamwacha mwenye nyumba katika hali ya kutazamia ziara yako itakayofuata wakati ambapo swali hilo litajibiwa.
6 Kitabu Creation ni chenye kutokeza kwa njia nyingi. Kinatoa ushuhuda thabiti ambao huthibitisha kuwako kwa Mungu. Kinaonyesha sababu kwa nini nadharia ya mageuzi haiwezi kuwa ya kweli. Kinaonyesha sababu kwa nini twaweza kuitumaini Biblia kuwa Neno la Mungu. Vielezi katika sura ya 18 na ya 19 vitanasa fikira za watu wenye mioyo minyofu, na kuchochea kupendezwa katika Biblia na makusudi ya Yehova. Kwa hiyo acheni sisi sote tutumie kwa faida kila fursa kuanzisha mafunzo na kushiriki katika utume wa ‘kufanya wanafunzi.’—Mt. 24:14; 28:19, 20; Mk. 13:10.