Kuanzisha Mafunzo ya Biblia Nyumbani
1 Mojapo njia zenye kuthawabisha na kuridhisha zaidi kwa Wakristo wa kweli ni kufundisha mtu kweli kupitia funzo la Biblia nyumbani. Hata hivyo, huenda ikawa wengine hawashiriki katika sehemu hii ya huduma yenye kuthawabisha kwa sababu wanahisi kwamba hawawezi kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia. Wahubiri na mapainia wengi wenye kutokeza walihisi hivyo wakati mmoja. Hata hivyo, kwa kumtumaini Yehova na kutumia madokezo yaliyo kwenye Huduma ya Ufalme Yetu, walijifunza jinsi ya kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia, nao waliongeza shangwe yao katika huduma. Waweza kuwa na mradi huohuo.
2 Kutumia Njia ya Moja kwa Moja na Trakti: Mojapo njia rahisi zaidi za kuanzisha funzo ni kwa kutumia njia ya moja kwa moja. Kile ambacho watu fulani wanahitaji tu ni mwaliko mchangamfu wa kujifunza Biblia. Hili laweza kufanywa kwa kumuuliza mwenye nyumba hivi tu: “Je! ungependa kuwa na funzo la kibinafsi la Biblia nyumbani na kuongeza ujuzi wako wa Biblia na kusudi la Mungu kwa dunia hii?” Au ungeweza kumwambia mwenye nyumba kwamba ungekuwa na furaha kumwonyesha jinsi funzo la Biblia la nyumbani linavyoongozwa. Ijapokuwa huenda wengi wakakataa toleo hili, lakini hebu wazia shangwe yako kwa kumpata mtu atakayelikubali!
3 Njia nyingine ya kuanzisha funzo la Biblia ni kwa kutumia mojapo trakti zetu. Ijapokuwa ni ndogo kwa ukubwa, zatoa ujumbe ambao ni wenye nguvu na wenye kusadikisha. Funzo laweza kuanzishwaje katika trakti? Ni kwa kumpa tu mwenye nyumba trakti ambayo wasadiki itampendeza. Kisha, chukua hatua ya kwanza, na kumwalika mwenye nyumba asome fungu la kwanza pamoja nawe. Fungueni Maandiko yaliyoonyeshwa bila manukuu, na uzungumze jinsi yanavyohusu habari hiyo. Kwenye ziara ya kwanza, unaweza kuangalia fungu moja au mawili tu. Mwenye nyumba akija kufahamu kwamba anajifunza mambo yenye kupendeza kutoka Biblia, huenda ukaweza kuongeza wakati unaotumia katika mazungumzo yenu ya Biblia.
4 Kutumia Biblia Tu: Wakati mwingine mtu hukubali mazungumzo ya Biblia lakini huonekana akikawia kukubali funzo rasmi au kutumia kimojapo vichapo vyetu. Bado unaweza kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia kwa kutayarisha mazungumzo ya kupendeza ya Kimaandiko yanayotegemea sehemu za kitabu Kuishi Milele au kitabu Kutoa Sababu lakini utumie Biblia peke yake unapomzuru mtu mwenye kupendezwa. Mazungumzo hayo yaweza kuchukua dakika 15 au 20, au zaidi, kulingana na hali. Yakifanywa kwa ukawaida na kwa njia ya kuendelea ya kufundisha kweli za Biblia, umeanzisha funzo la Biblia, nalo laweza kuripotiwa. Wakati uwapo wenye kufaa, toa kitabu Kuishi Milele, na uongoze funzo rasmi katika hicho.
5 Zaidi ya kupata fursa mbalimbali katika huduma ya shambani, je, umejitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia na majirani, marafiki, au washiriki wa familia? Je! ilikuwa ni wakati fulani uliopita? Je! umejaribu tena karibuni? Ikiwa njia moja haikufanikiwa, umefikiria kujaribu nyingine?
6 Waweza kufanikiwa kuanzisha mafunzo ukitumia madokezo yanayotolewa, kuendelea katika utumishi wa shambani, na kumtumaini Yehova kwa baraka zake. Usipunguze kamwe uwezo wa ile kweli na msaada ambao Yehova hutoa. Na uongeze shangwe yako katika huduma kwa kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani.