Kutoa Habari Njema Kutoa Mafunzo ya Biblia Nyumbani
1 Nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Agosti 1991 ilitukumbusha juu ya daraka letu la kupanda na kutia maji katika shughuli ya kufanya wanafunzi wa Kristo. Ilituonyesha kwamba tunapaswa kuchochewa kuongoza mafunzo ya Biblia kwa sababu ya upendo wetu kwa watu wanaoitikia ujumbe wa Ufalme. Kutoa mafunzo ya Biblia nyumbani kutatusaidia kutimiza utume wetu wa kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.
2 Ni vema kuona kwamba wengi wetu wameanza kutumia kihalisi kitia moyo kizuri kilichotolewa. Ripoti zinaonyesha kwamba mafunzo ya Biblia mengi zaidi yanaongozwa. Hesabu ya mafunzo ya Biblia yanayoripotiwa katika Afrika Mashariki iliongezeka kwa asilimia 16 hivi katika 1991 kupita mwaka wa utumishi wa 1990. Bila shaka wale ambao wameanza kuongoza mafunzo kwa mara ya kwanza wanafurahia ushiriki wanaopata katika kazi ya kufanya wanafunzi. Lakini wengi zaidi waweza kushirikije katika jambo hili lenye kuthawabisha la huduma yetu?
3 Tumia Toleo la Mwezi Huu: Mwezi wa Novemba unafaa hasa kwa kutafuta kuanzisha mafunzo mapya ya Biblia. Tutakuwa tukitoa Biblia ya New World Translation na kitabu The Bible—God’s Word or Man’s? Njia nzuri ya kukuza kupendezwa kwa mwenye nyumba kungekuwa ni kutumia madokezo yanayopatikana katika kitabu Kutoa Sababu.
4 Tunaweza kukazia Biblia kwa kutumia matangulizi yaliyodokezwa katika kurasa 9 na 10 za kitabu Kutoa Sababu. Kuna njia tano tofauti tofauti zilizoorodheshwa za kuelekeza fikira kwenye Biblia. Kuwatia watu moyo watafute majibu ya Biblia kwa maswali ya maisha kwaweza kufungua njia ya kuanzisha funzo la Biblia.
5 Chini ya kichwa kidogo “Funzo la Biblia Nyumbani” katika ukurasa wa 10 wa kitabu Kutoa Sababu, kuna madokezo mawili ambayo yaweza kuwa yenye mafaa katika kuelekezea fikira kwenye kitabu God’s Word. Yote mawili yanatia moyo kutumia kitabu hicho kwa njia ya funzo lenye utaratibu. Ikiwa unatumia njia ya moja kwa moja kwa kuanzisha funzo la Biblia, unaweza kufuata madokezo mazuri yaliyo katika Huduma ya Ufalme Yetu ya Septemba 1991.
6 Itibari Katika Yehova: Ili kufanikiwa katika kazi ya mafunzo ya Biblia, ni lazima tukumbuke kwamba mafanikio ya kutoa mafunzo ya Biblia nyumbani yaweza tu kupatikana kwa msaada wa Yehova. Yeye huwa na sehemu ya maana zaidi katika jitihada zetu za kuwasaidia watu. (1 Kor. 3:6) Kwa hivyo, twapaswa kusali si kuhusu tu kupata mtu wa kujifunza naye bali pia kuhusu maendeleo yanayofanywa na wenye kupendezwa ambao tumepata. (Yn. 16:23) Ni lazima tukumbuke sisi tu “wafanya kazi pamoja na Mungu.”—1 Kor. 3:9.