Siku ya Pekee ya Kuanzisha Mafunzo ya Biblia
1 Kuanzia Januari, kila kutaniko litachagua siku moja ya mwisho-juma kila mwezi, labda mwisho-juma wa kwanza, ili kujitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia. Ikitegemea hali za kwenu, mnaweza kufanya hivyo Jumamosi au Jumapili. Siku hiyo, wenye nyumba wasipokubali funzo la Biblia, wahubiri bado wanaweza kuwaonyesha kitabu Biblia Inafundisha au kuwaachia magazeti ya karibuni. Wazee na watumishi wa huduma wote wanapaswa kupanga kushiriki kikamili katika utendaji huo na kuwasaidia wahubiri kuanzisha mafunzo ya Biblia.
2 Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itachagua siku moja ya mwisho-juma ambayo itatumiwa kuanzisha mafunzo ya Biblia. Wahubiri watakumbushwa mara kwa mara ili wajitayarishe na kujitahidi kabisa kuanzisha mafunzo ya Biblia nyumba kwa nyumba au pamoja na wale waliopendezwa awali.
3 Jinsi ya Kujitayarisha: Tunaweza kupata mapendekezo ya kuanzisha mafunzo ya Biblia katika nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2006 na kwenye ukurasa wa 12 wa kitabu Kutoa Sababu. Wahubiri fulani wanaweza kuamua kutumia trakti, kama vile Je, Ungependa Kujua Ukweli? Pia, ukurasa wa 3 wa Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 2007 una mapendekezo ya kuanzisha mafunzo ya Biblia unapowatembelea watu waliochukua magazeti. Wazee na watumishi wa huduma watapewa mgawo wa kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani kwa muda wa dakika 10 hadi 15, na katika mkutano huo wanapaswa kuzungumzia au hata kuwa na onyesho la pendekezo moja au mapendekezo mawili ya kuanzisha mafunzo ya Biblia.
4 Bila shaka, si kila mtu atakayekubali funzo la Biblia au kuendelea kujifunza kwa muda mrefu. Hilo halipaswi kutuzuia tusianzishe mafunzo, kwa kuwa Yehova ndiye anayewavuta watu wenye mfano wa kondoo kwenye tengenezo lake. (Yoh. 6:44) Kazi yetu si kupanda tu mbegu za kweli bali pia kuzikuza na kuzitilia maji ili zitie mizizi, na hilo linatia ndani kujifunza Biblia pamoja na watu wenye mioyo minyoofu. Tunapofanya hivyo, tunatumia pendeleo la kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu.—1 Kor. 3:9.