Kupanda na Kutia Maji—Hatua za Kuelekea Kufanya Wanafunzi
1 “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu.” (1 Kor. 3:6) Ndivyo mtume Paulo alivyotambulisha hatua tatu za msingi katika mpango wa kufanya wanafunzi wa Kristo. Zile hatua mbili za kwanza, kupanda na kutia maji, zinahusisha pendeleo na daraka walilo nalo watumishi wa Mungu walio wakfu na kubatizwa.
2 Hilo hutaka kuhubiri hadharani na nyumba kwa nyumba, vivi hivi, na katika njia nyinginezo. Lahusisha pia kufundisha watu hatua kwa hatua kushika mambo yote aliyoamuru Yesu. (Mt. 28:19, 20) Hatua hiyo ya pili yaweza kutimizwa tu kwa kufanya ziara za kuwarudia wale waonyeshao kupendezwa, kuwahusisha katika mazungumzo ya Biblia, na kuongoza mafunzo ya Biblia nao. Je! wewe unajithibitisha kuwa mfanyakazi mwenzi mshikamanifu, ukishirikiana na Yehova kwa kupanda mbegu za kweli na halafu kufuatia kwa utiliaji maji na upaliliaji unaohitajiwa?—1 Kor. 3:9.
TAMBUA UWEZEKANO NA UHITAJI
3 Katika Afrika Mashariki wakati wa mwaka wa utumishi wa 1990, tuligawanya vitabu na vijitabu zaidi ya 340,000 na magazeti karibu milioni moja! Pia tulikuwa na watu zaidi ya 40,000 kwenye Ukumbusho, wakipita kwa mbali sana ule wastani wa wahubiri 13,222 kwa mwaka huo. Ugawanyaji wa fasihi ni sehemu muhimu ya kazi yetu ya kupanda mbegu. Mbegu za kweli zilizopandwa hivyo huwa na uwezekano mkubwa sana wa kuzaa wanafunzi wapya, lakini je! sisi, tukiwa wafanyakazi wenzi wa Mungu, twahisi tukisukumwa na moyo tufanye ziara za kurudia watu hao na kusitawisha kupendezwa kwao katika mazungumzo ya Biblia? Wahubiri wa kundi katika Afrika Mashariki sasa wana wastani wa mafunzo ya Biblia kati ya 0.6 na 2.0. Kukiwa na jumla ya idadi ya watu zaidi ya milioni 160 ni wazi kwamba bado twahitaji kufikia na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani yenye maendeleo. Ijapokuwa wengine, kwa sababu ya vizuizi mbalimbali, huenda wasiweze kuongoza funzo moja au mafunzo zaidi ya Biblia nyumbani, yafaa kila mmoja wetu achunguze hali zake binafsi.
4 Inapendeza kuona yanayotukia katika sehemu fulani. Makundi yana eneo lenye kuzaa na yanaripoti wastani wa kuanzia funzo moja hadi mawili ya Biblia kwa kila mhubiri. Ongezeko katika wanafunzi wapya hupatana na kadiri ya idadi ya mafunzo ya Biblia yanayoongozwa. Hilo laweza kuonwa kwa kulinganisha wastani wa idadi ya wahubiri na idadi ya mafunzo ya Biblia katika nchi mbalimbali kama ilivyoripotiwa katika Kitabu-Mwaka 1991 (Kiingereza).
5 Upendo wetu kwa watu wanaoitikia ujumbe wa Ufalme tunaohubiri wapaswa kuwa ndio msukumo wetu wa kuongoza mafunzo ya Biblia. Ni lazima tushiriki kwa unyofu hangaikio lenye upendo la Yehova kwa watu na kuthamini kwamba wokovu wao wafungamana na ukuzi wao wa kiroho. (1 Pet. 2:2) Kama mimea halisi ambayo hutaka maji ili kusitawisha ukuzi, watu ambao huonyesha kupendezwa kwa mara ya kwanza katika ujumbe wa Ufalme kwa kawaida hawataanza kuhudhuria mikutano wasipoelekezwa kwa ukawaida kwenye tengenezo la Mungu kupitia mafunzo ya Biblia.
6 Utii kwa upande wetu wahusika pia. Yesu alisema kwamba walio katika upande wa kweli husikiliza sauti yake. (Yn. 18:37) Aliamuru wanafunzi wake kuhubiri na kufundisha; na aliwatayarisha ili kutimiza kazi hiyo. Kwa kielelezo chake chenye kutokeza akiwa mwalimu na kwa kuwahangaikia sana watu, Yesu alituwekea kiolezo tufuate katika kusaidia wengine. (Luka 6:40; Yn. 13:13; 14:12) Jitihada zetu zaweza kuchangia wokovu wetu sisi wenyewe na wa wale tufundishao pia.—1 Tim. 4:16.
MISAADA YA KUANZISHA MAFUNZO YA BIBLIA
7 Ili kukamilisha kazi yake, fundi stadi huteua vifaa vyake vya kazi kutoka kwa vile alivyo navyo vya namna nyingi. Tukiwa walimu, tuna vichapo vingi, kutia na broshua na trakti, vilivyokusudiwa kutusaidia vikiwa vifaa vya kazi ili kufikia mioyo ya watu walio na elimu na maoni mbalimbali.
8 Baadhi ya wahubiri wamepata matokeo mazuri katika kutumia trakti na broshua kuwa utangulizi wa mazungumzo ya Biblia. Kwa mfano, ile trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani hutaja au kunukuu maandiko mbalimbali zaidi ya 20 kuonyesha tumaini hilo zuri ajabu. Maandiko hayo yaweza kutumiwa kusitawisha mazungumzo kadhaa ya Biblia yenye kuchochea moyo. Kwa njia rahisi na yenye kuvutia jicho, broshua zetu zaweza pia kuwafahamisha watu kweli za msingi za Biblia na kuwachochea watake kujua habari zaidi.
9 Je! wajua mtu fulani mwenye elimu kidogo au mwenye kasoro ya macho? Je! umejaribu kutumia broshua Furahia Milele Maisha Duniani! kuanzisha mazungumzo ya Biblia ya hatua kwa hatua na mtu huyo? Ile broshua “Tazama!” ni kifaa kingine kizuri chenye mafungu ya kufungua ambayo kwa ustadi huhusisha mwenye nyumba katika kujifunza juu ya ahadi za Mungu kwa wakati ujao. Na bila shaka kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotolewa katika 1982, kimekuwa na mafanikio sana katika kusaidia asilimia kubwa ya wale zaidi ya 1,700,000 ambao wamebatizwa tangu wakati huo.
KUTENDA TUKIWA NA DARAKA KUELEKEA WENYE KUPENDEZWA
10 Huenda ukaliona kuwa jambo lenye kunufaisha kuangalia kadi yako ya Maandishi ya Mhubiri wa Kundi na kuandika hesabu ya vitabu, vijitabu (kutia broshua), na magazeti uliyoangusha wakati wa miezi 12 iliyopita. Je! maangusho hayo yalikuwa ndiyo mwisho? Au ulienda zaidi ya ile hatua ya kupanda? Kwa hao watu mmoja mmoja walioonyesha kupendezwa vya kutosha kuchukua baadhi ya fasihi yetu, ni wangapi ulioonana nao tena bila kukawia? Je! ulifuatisha utiaji maji unaohitajiwa kisha kusali kwamba Yehova aikuze?—Linganisha Matendo 16:14 na 2 Wathesalonike 3:1.
11 Labda hufanyi ziara za kurudia au kuongoza funzo la Biblia kwa sababu wahisi kwamba hustahili vya kutosha. Yaelekea, sana-sana hiyo ni kwa sababu ya mtazamo wako wala si ukosefu wako wa uwezo. Yehova hakutuma nje watu wake kazini bila kuwatayarisha na kuwastahilisha vya kutosha. Kupitia Neno takatifu na tengenezo lake, yeye hututayarisha kwa “kila kazi njema.” (2 Tim. 3:16, 17; 2 Kor. 3:5, 6) Kwa roho takatifu, kurasa zilizochapwa, na mafundisho ya mdomo na maonyesho kutoka jukwaani, bila kutaja vielelezo halisi vya watumishi stadi waliojitoa walio tayari kutusaidia, Yeye hutupa tunachohitaji. Hatuhitaji elimu ya juu ya ulimwengu huu ili kuongoza funzo la Biblia. Twahitaji kukubali elimu ya kiroho ya hali ya juu zaidi inayotolewa kupitia tengenezo la Yehova.—Linganisha Matendo 4:13.
12 Kutumia kibinafsi yale tunayoandaliwa katika Huduma ya Ufalme Yetu, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mikutano ya Utumishi, na njia nyinginezo za mafundisho kwahitajiwa. Mtume Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania waziwazi hivi: “Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu.” (Ebr. 5:12) Mtu anayefanya kazi ya ufundi kwa miaka kadhaa anatazamiwa awe amepata kadiri fulani ya ustadi katika matumizi ya vifaa vyake vya kazi. Maendeleo katika kujifunza jinsi ya kuendeleza mazungumzo ya Biblia yatadhihirika tuonyeshapo kupendezwa kwa unyofu na kujitahidi kwa bidii.—Mit. 12:24; 22:29.
13 Kurudi na kuzungumza zaidi habari za Biblia na wale wanaoonyesha kupendezwa na ujumbe wa Ufalme hugharimu kitu fulani kwa namna ya wakati na jitihda. Lakini yatupasa kuthamini kwamba kuwa kwetu katika kweli ni wonyesho wa upendo na fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Hizo zilionyeshwa kupitia mtu fulani aliyetumia saa nyingi akitufundisha kweli kwa subira. Vivyo hivyo, upendo wapaswa utulazimishe tukomboe wakati unaohitajiwa na kuutumia kwa kazi hii yenye maana zaidi ya kufanya wanafunzi.—2 Kor. 5:14, 15; Efe. 5:15, 16.
14 Mahali ambako yawezekana, makundi mengi yamefuata dokezo la Sosaiti la kufanya mipango ili kutoa ushahidi jioni. Saa za mapema jioni kwa kawaida ni wakati wenye kufaa kufanya ziara za kurudia kwa watu ambao wameonyesha kupendezwa. Maandishi ya nyumba kwa nyumba yenye kuandaa habari kuu kuhusu watu mmoja mmoja waliotolewa ushahidi, ni ya maana ili kufanya ziara za kurudia zenye mafanikio na kuanzisha mazungumzo ya Biblia. Usiweke mbali maandishi hayo katika kitabu au katika Biblia na kuyasahau. Kusahau kufanya ziara ya kurudia mpaka majuma mengi baadaye unapokuwa katika ujirani huo humwacha mtu huyo katika hali ya kuweza kutembelewa na wajumbe wa Shetani, ambao hupenda sana kung’oa kile ambacho huenda kikawa kimepandwa katika moyo wa mtu huyo. (Luka 8:12) Je! wewe utazuia mbinu za Shetani kwa kurudi bila kukawia? Ukihisi daraka lako na kuthamini pendeleo lako, utarudi bila kukawia, inapowezekana.—1 Kor. 9:16, 23.
JINSI YA KUANZA FUNZO LA BIBLIA
15 Kuanza funzo la Biblia hakuhusu mpango mgumu wenye kutatanisha. Watu fulani huenda wakakubali kwa urahisi toleo lako la moja kwa moja la kuongoza funzo la Biblia nyumbani nao. Hata hivyo, wahubiri wengi hawapendelei kutaja funzo bali kuelekeza tu mazungumzo ya Biblia kufikia funzo.
16 Upendo kwa watu na tamaa ya unyofu ya kuwasaidia huhitajiwa. Pia kujitayarisha vizuri ni kwa lazima. Hiyo yapasa kutia ndani kupitia maandishi ambayo huenda ukawa uliweka juu ya yale ambayo umekwisha kuzungumza pamoja na mtu huyo na kuamua juu ya njia ambayo utatumia katika kuwa na mazungumzo zaidi. Fikiria mambo mbalimbali ambayo utasema. Je! utateua maandiko zaidi machache juu ya habari mliyozungumzia wakati uliopita? Au je! ungeweza kufungua trakti au kitabu alicho nacho mtu huyo na kuzungumza pamoja naye mafungu machache ya kwanza? Waweza kuchagua habari ambayo ameonyesha kupendezwa nayo. Mwanzoni, tumia dakika 10 au 15 tu. Wakati waweza kuongezwa hatua kwa hatua, ikitegemea kina cha kupendezwa kunakoonyeshwa. Uamuzi wako mzuri wapasa ukusaidie utambue jinsi ya kuendelea na kadiri ya wakati ambao utatumia.
17 Madokezo mengi yenye kusaidia yametolewa kwa muda wa miaka iliyopita kukusaidia ufanye maendeleo hatua kwa hatua katika kufanya wanafunzi. Yakiwa sehemu ya mfululizo, matoleo ya Oktoba na Novemba 1990 ya Huduma ya Ufalme Yetu yalikuwa na makala zenye kusaidia zilizokuwa na vichwa “Fikia Mioyo Kupitia Mafunzo ya Biblia Yenye Mafanikio” na “Kuelekeza Wanafunzi wa Biblia Kwenye Tengenezo la Yehova.” Huduma ya Ufalme Yetu ya Februari 1987 ilikuwa na makala “Kutayarishia na Kuongoza Mafunzo ya Biblia ya Nyumbani.” Kuchunguza kifupi Index chini ya “Mafunzo ya Biblia” kutakuelekeza kwenye habari zaidi zenye kusaidia.
18 Kikiwa kiolezo cha namna ya kuongoza funzo la Biblia, sikiliza yale yanayofanywa kwenye Funzo la Kitabu la Kundi. Bila shaka, kwenye funzo a Biblia nyumbani, huna kiasi cha habari ulichotangulia kugawiwa cha kuzungumza. Kwa hiyo mwendo wako wa kuzungumza habari wapaswa kulingana na uwezo na uhitaji wa mwanafunzi. Kuongezea, mwangalizi wa utumishi na wahubiri wengine na mapainia wenye ujuzi watafurahia sana kwenda pamoja nawe na kukupa madokezo yenye kutumika juu ya kuongoza mafunzo ya Biblia yenye mafanikio.
19 Kwa kutambua kwamba Yehova hutimiza lile fungu la maana sana katika jitihada zetu za kusaidia watu, twapaswa kusali si ili tumpate mtu fulani wa kufunza tu bali pia ili wenye kupendezwa tuliowapata wafanye maendeleo. Maoni na hisia zetu zapasa kuwa kama za mtume Paulo alipokuwa akimtolea ushahidi Mfalme Agripa: “Namwomba Mungu kwamba, ikiwa kwa machache au ikiwa kwa mengi, si wewe tu ila na hao wote wanaonisikia leo wawe kama mimi.” (Mdo. 26:29) Paulo alitaka wasikilizaji wake wawe wanafunzi wa kweli wa Kristo, iwe hiyo ilitaka wakati mfupi au kipindi kirefu zaidi cha usaidizi wa kibinafsi.
20 Kuongoza mafunzo ya Biblia hutuwezesha “kutoa kikamili ushahidi wa habari njema za fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24, NW) Idadi ya watu isiyojulikana bado inaweza kugeuzwa kutoka gizani na kuingia nuruni na kutoka kwenye nguvu ya Shetani kumwelekea Mungu. (Mdo. 26:18) Wewe, mtumishi wa Yehova uliye wakfu na kubatizwa, ni lazima ufanye sehemu yako kwa kupanda mbegu za kweli kisha kufuatisha utiliaji maji unaohitajiwa kwa njia ya mazungumzo ya Biblia na mafunzo ya Biblia nyumbani ya ukawaida. Kwa njia hiyo unaweza kupata shangwe kuu ya kuona watu wakiwa wanafunzi na kujiunga nawe katika kusaidia wengine bado wawe wanafunzi wa Yesu Kristo.