‘Nendeni Mkafanye Wanafunzi’—Je! Wewe Unafanya Hivyo?
1 Mojapo shangwe kubwa ambazo unaweza kuwa nazo ukiwa mhubiri wa Ufalme ni kusaidia mtu fulani atwae maarifa ya kujua ukweli. Mtu huyo anapokua katika maarifa na uthamini, moyo wako utajawa na shangwe na shukrani kwa Yehova. Sisi tunajua kikamili kwamba tunaposhiriki katika kupanda na kutia maji mbegu ya ukweli, Yehova ndiye anayezifanya zikue. Hata hivyo, ni msisimuko ulioje kushiriki kuongoza mtu mwenye moyo wa haki kwenye njia ya uhai!—1 Kor. 3:6-9.
2 Je! wewe ni kichwa cha jamaa? Ikiwa ndivyo, je! wewe unaongoza funzo la Biblia pamoja na jamaa yako? Hili ni jambo la maana sana. Vichwa vya jamaa vina daraka mbele za Yehova kuagiza na kuelekeza washiriki wa jamaa zao katika njia ya uhai. (Kum. 6:4-7; Efe. 5:25-29; 1 Tim. 5:8) Vyo vyote, chukua daraka lako la kuwafanya wawe wanafunzi.
3 Kuongezea funzo la Biblia la jamaa yako, je! unaweza kuongoza funzo la Biblia pamoja na mtu fulani? Swali la maana zaidi huenda likawa: Je! unang’amua pendeleo na daraka lako kufundisha mtu fulani ukweli kwa kutii amri ya Yesu? (Mt. 28:19, 20, NW) Inaonekana kwamba wahubiri zaidi katika Afrika Mashariki wanaweza kuongoza funzo la Biblia la nyumbani. Katika sehemu fulani fulani inahitaji bidii yenye kuendelea ili kupata funzo. Ziara za kurudia-rudia zinahitajiwa. Labda umejaribu lakini hujapata mtu fulani ambaye ana nia ya kujifunza. Unaweza kufanya nini?
MWELEKEO NI WA MAANA
4 Unaweza kuanza kwa kujiuliza mwenyewe: Mwelekeo wangu ni nini kuhusu kazi ya funzo la Biblia? Je! kweli mimi nataka funzo la Biblia? Je! mimi naona sehemu hii ya huduma kuwa ya maana na yenye kuokoa uhai, nikitambua kwamba watu walio wengi katika ulimwengu ni ‘wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zao’?—Efe. 2:1.
5 Wahubiri na mapainia wameandikia Sosaiti wakiiambia jinsi Yehova alijibu sala yao ya bidii walipomwomba waziwazi awasaidie wapate watu wenye kupendezwa ambao wangeweza kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja nao. (Rum. 12:12; 1 The. 5:17) Je! wewe umefanya hivyo? Je! wewe umemwomba Baba yako wa mbinguni kwa nasaha ili uwe na pendeleo la kupata na kufundisha mtu fulani ambaye kweli kweli anatafuta ukweli?—Eze. 9:4.
6 Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1987, kulikuwa na mafunzo ya Biblia 14,519 yaliyoongozwa kwa wastani kila mwezi katika Afrika Mashariki. Hili ni jambo la kusifika kweli kweli. Wakati wa kipindi hicho hicho cha wakati Biblia, vitabu, na vijitabu, 328,321 pia magazeti zaidi ya 600,000 yaliangushwa. Kwa hiyo vichapo vya Sosaiti vinapatikana katika nyumba nyingi ambamo mafunzo hayajaanza kuongozwa. Hivyo, inaonekana wazi kwamba kuna uwezekano mzuri wa kuanzisha mafunzo zaidi ya Biblia ya nyumbani.
7 Je! ingeweza kuwa kwamba tunahitaji kuona uhitaji wa funzo la Biblia na kuweka jitihada kubwa kuanzisha mafunzo katika broshua? Je! wewe unashiriki huduma ukiwa na mwelekeo chanya, uking’amua kwamba malaika wanasaidia kazi kwa kuelekeza watu wa Yehova kwenye milango ya wale ambao wana tamaa ya kusikia “habari njema za milele”? (Ufu. 14:6, NW) Shangwe kubwa ambayo itakuwa yako unaposaidia mtu mwingine kujifunza ukweli italipia zaidi jitihada ambayo umefanya ili ufuate amri ya Yesu ya ‘kuenda na kufanya wanafunzi’ na kuwafundisha.