Ziara za Kwanza Zenye Matokeo
1 Kuanzisha mazungumzo katika huduma kunaweza kutokeza mwito wa ushindani kwa sababu watu hushughulikia sana mambo yao au wana maoni dhahiri kuhusu dini. Tunaweza kuwa na nini akilini kitakachotusaidia kufanya ziara yetu ya kwanza iwe na matokeo?
2 Kwa kuwa kipindi hiki ni cha sikukuu, unaweza kuanza mazungumzo yako kwa kusema:
◼ “Katika wakati huu wa mwaka, bila shaka dhabihu ya Yesu imo akilini mwetu. Unafikiri Yesu anafanya nini sasa?” Ruhusu itikio. Halafu unaweza kushiriki na mwenye nyumba Ufunuo 6:2, linaloeleza Yesu kuwa ameketi juu ya farasi mweupe akienda kukamilisha ushindi wake. Eleza juu ya sehemu yake akiwa mfalme na faida za kudumu zitakazoletwa na utawala wake kwa ainabinadamu yote yenye utii.
3 Unapotoa matoleo ya Machi 15 au Aprili 1 yenye makala kuhusu uhuru, unaweza kusema:
◼ “Watu ulimwenguni pote wanang’ang’ania uhuru. Lakini ahadi za uhuru mara nyingi hukatisha tamaa na huwa za muda mfupi. Ibada ya Yehova, Mungu wa kweli, huleta uhuru wa kudumu.” Soma 2 Wakorintho 3:17, na uonyeshe kwamba toleo hilo la Mnara wa Mlinzi hukazia ahadi ya Mungu na huonyesha kwa nini matukio ya ulimwengu huthibitisha kwamba ukombozi wetu u karibu.
4 Unaweza kutoa “Mnara wa Mlinzi” la Machi 1, 1992, kwa kukazia habari ya usalama, ukisema:
◼ “Je! unafikiri wakati utafika ambapo hatutalazimika kukabiliana na uhalifu na jeuri? [Ruhusu itikio la mwenye nyumba.] Biblia inaonyesha suluhisho la kudumu hapa kwenye Zaburi 37:9-11.” Soma andiko na ufungue kurasa 8, 9 katika makala ya Mnara wa Mlinzi ili usome sehemu zilizochaguliwa. Halafu toa uandikisho.
5 Kumbuka kwamba mradi wetu ni kuongoza mafunzo ya Biblia. Kwa kuwa wengi watakuwa wakifanya upainia msaidizi katika Aprili, tutakuwa na fursa nyingi hata zaidi za kuwapata watu mmoja mmoja wanaopendezwa kujifunza Biblia. Lakini hata ikiwa hali zetu hazituruhusu kufanya upainia msaidizi katika Aprili, sisi sote tunaweza kuweka mradi wa kuanzisha funzo la Biblia.
6 Wahubiri wengine wametumia trakti ili kuanza mafunzo ya Biblia kwenye ziara ya kwanza.
Unapotoa trakti “Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani,” huenda ukasema:
◼ “Sisi ni wafanyakazi wa kujitolea katika ujirani wenu. Acha nikupe trakti hii, ambayo hueleza jinsi kazi yetu ilivyo. Je! unafikiri ulimwengu utapata kuwa namna hiyo?” Baada ya kupata itikio, unaweza kuzungumzia mafungu ya kwanza machache na mtu huyo, ukikazia Mathayo 6:9, 10 na Zaburi 37:29.
7 Chunguza kwa makini jinsi utakavyoanzisha mazungumzo. Madokezo mazuri yametolewa katika kitabu Kutoa Sababu kurasa 9-15. Kutumia matangulizi hayo kwa ustadi kutasaidia kufanya ziara zako za kwanza ziwe na matokeo.