Tumia Kitabu Kutoa Sababu Kwenye Ziara za Kurudia
1 “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji.” Ndivyo Paulo alivyosema. (1 Kor. 3:6) Maneno hayo matano huandaa muhtasari rahisi wa hatua mbili za kwanza katika kufanya wanafunzi. Mara nyingi, kazi ya ziara za kurudia imeitwa kazi ya “kutilia maji.” Ni kiunganishi cha maana sana kati ya ziara ya kwanza na mtu huyo kuwa mwanafunzi aliyebatizwa. Kazi ya ziara za kurudia hutuwezesha ‘kueneza maarifa’ kulisha mbegu ya kupendezwa kulikoonyeshwa hadi inapotoa mizizi na funzo la Biblia linaanzishwa.—Mit. 15:7.
2 Wengine huenda wakasita kuzuru tena mahali kupendezwa kulipoonyeshwa kwa sababu ya kukosa uhakika wa yale ya kusema. Kitabu chetu cha uongozi Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kimethibitika kuwa cha maana sana katika kufanya utiaji maji huo. Kwa kawaida, kabla mwenye nyumba hajakubali kupata funzo la Biblia linaloongozwa kwa kawaida, mfululizo wa ziara fupi lazima ufanywe. Kitabu Kutoa Sababu huandaa mihtasari ya vichwa vya Kimaandiko vinavyoweza kuzungumzwa pamoja na mwenye nyumba. Jitayarishe vema kwa ajili ya ziara ya kurudia, labda ukitumia dokezo moja au mawili kati ya yafuatayo.
3 Ikiwa uliangusha nakala ya “Mnara wa Mlinzi” la Machi 1, 1992, kuhusu kichwa usalama, wakati unaporudi unaweza kusema:
◼ “Nilifurahia mazungumzo yetu nawe kuhusu usalama wa juu zaidi na wa muda mrefu zaidi unaoahidiwa katika Biblia. Swali linalopasa kutuhangaisha kila mmoja wetu ni, Tunaweza kufanya nini ili tuwepo tufaidike na badiliko hilo? Angalia yale Yesu alisema kwenye Yohana 17:3. Baada ya kusoma andiko hilo unaweza kutumia moja ya makala katika toleo la karibuni la Mnara wa Mlinzi ili kuonyesha jinsi gazeti hilo husaidia mtu kupata maarifa juu ya Mungu, au maana ya hali za ulimwengu, au kusudi la uhai, au jinsi matatizo yetu yatakavyotatuliwa.” Toa uandikisho.
4 Kwenye ziara nyingine ya kurudia, baada ya kumuuliza mwenye nyumba yeye anaelewa Ufalme wa Mungu kuwa nini, kama inavyoonyeshwa katika Sala ya Bwana, fungua kurasa 325-32. Kadiri wakati uruhusuvyo, eleza maandiko yaliyo chini ya “Je! Ufalme wa Mungu ni Serikali Halisi?” na “Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?” Elewesha waziwazi kwamba tofauti na mawazo yasiyo sahihi, Ufalme haumo moyoni mwa mtu. Ufalme ni serikali halisi! Badala ya kupitia habari yote kwa wakati mmoja, uliza maswali mtakayozungumzia baadaye.
5 Ikiwa mazungumzo ya hapo kwanza yalihusu wakati ujao wa dunia, unaweza kuuliza:
◼ “Je! wanadamu wataruhusiwa na Mungu waiharibu dunia kwa njia fulani?” Halafu ufungue ukurasa 87 wa kitabu Kutoa Sababu na kuzungumzia jibu la Kimaandiko. Au huenda mwenye nyumba akauliza: “Ikiwa mamia ya mamilioni watafufuliwa kutoka kwa wafu, hao wote wataishi wapi?” Jibu laweza kupatikana katika kitabu Kutoa Sababu, ukurasa 341.
6 Jaribu usimweleze mwenye nyumba kweli yote kwa wakati mmoja. Mwachie maswali fulani ya kujibiwa katika ziara zitakazofuata. Tukiwa wafanyakazi wenzi pamoja na Mungu, tutapanda na kutilia maji kwa ustadi kwa kutumia kwa matokeo kitabu Kutoa Sababu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ataifanya ikue.