Tia Moyo Ufuatiaji wa Miradi ya Kiroho
1 Hakujapata kamwe kuwa na vijana wengi hivyo wanaoshiriki katika kuhubiri habari njema za Ufalme! Makumi ya maelfu wanaitikia shauri kwenye Mhubiri 12:1: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.” Ni nini kinachosukuma vijana hao kuwa na ushiriki wa kawaida katika huduma, na kwa nini wengi kati yao wanashiriki katika utumishi wa painia?
2 Hakuna shaka kwamba wengi wanaiga mwenendo wa kijana mwenye kutokeza Timotheo. Mama na nyanya yake walimpa faida ya elimu ya kiroho kuanzia utoto na wakamtia moyo kufuatia miradi ya kiroho. (2 Tim. 3:14, 15) Hivyo, fursa ilipotokea ya mapendeleo zaidi ya utumishi, yeye alistahili na alikuwa tayari.—Mdo. 16:1-3.
3 Vijana wengine zaidi wanaweza kutiwaje moyo kufuatia miradi ya kiroho? Ni msingi wa aina gani unaopasa kuwekwa? Wazazi wanaweza kukuzaje uthamini wa kweli ndani ya watoto wao na kuwasaidia wajiwekee miradi ya kudumu?
4 Weka Msingi wa Kiroho: Wazazi wanapaswa wahakikishe kwamba yale wanayofundisha watoto wao yanatoka kwa Yehova ili yafanye watoto wao ‘wahekimishwe hata wapate wokovu.’ (2 Tim. 3:15) Kwa bidii jaribu kusitawisha ndani yao upendo wenye kina wa Neno la Mungu, Biblia. Hilo hutaka funzo la Biblia la kawaida lenye maana, linalohusu mahitaji yao, pamoja na hudhurio la kawaida la mikutano. Ili vijana wawe na imani yenye nguvu itakayowasukuma kufuatia miradi ya kiroho, ni lazima wawe na programu ya funzo lao la kibinafsi na kukuza uhusiano wao wenyewe na Yehova.—1 The. 5:21; Ebr. 11:1.
5 Vijana Wakristo wataitikia kwa utayari zaidi kufuatia faida za kiroho ikiwa wazazi wao na watu wengine wakomavu kundini wanaweka mfano mzuri na kudhihirisha “furaha ya BWANA [Yehova, NW].” (Neh. 8:10) Kwa kuonyesha shangwe, sisi sote twaweza kusaidia vijana wetu wathamini kwamba matakwa ya Ukristo wa kweli si mazito.—1 Yn. 5:3.
6 Vijana wengi wamevutiwa sana na mapainia, wamishonari, na waangalizi wasafirio waliohubiri pamoja nao katika utumishi wa shambani au waliowatia moyo kwa mazungumzo. Wazazi wanaweza kusaidia kwa kualika nyumbani mwao wafanyakazi wa wakati wote walio mfano mzuri kwenye mlo au nyakati nyingine kwa ajili ya ushirika wa Kikristo. Yesu Kristo aliandaa mfano bora zaidi wa kutoa uangalifu uliosawazika kwa vijana.—Mk. 10:13-16.
7 Kuweka Miradi: Kwa uongozi ufaao wa wazazi, mara nyingi watoto hujiwekea wenyewe miradi ya kiroho mapema maishani. Vijana wakishaamua ni mradi upi wa kiroho wenye kustahili wanaotamani kuutimiza, iwe ni utumishi wa upainia, kutumikia mahali kuliko na uhitaji mkubwa, utumishi wa Betheli au wa umishonari, na kadhalika, wazazi na watu wengine wakomavu wanaweza kuwatia moyo kwa uchangamfu waendelee kujitahidi kufikia miradi yao, wakiandaa madokezo yenye kutumika ili kuwachochea mbele.
8 Kila kundi ni kama familia. Kwa hiyo kila mmoja wetu apaswa apendezwe kuwasaidia vijana waendelee kutembea katika kweli na kufanya maendeleo ya kiroho. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwahakikishia upendo wetu kwao na kuwatia moyo kufuatia miradi ya kiroho.