Jinsi Unavyoweza Kufikia Miradi Yako ya Kiroho
1 Bila shaka, ukiwa kijana Mkristo miradi yako maishani inachochewa na upendo wako kwa Yehova na maneno ya Yesu kwa Wakristo wote kwamba ‘wautafute kwanza ufalme.’ (Mt. 6:33) Huenda ukawa na mradi wa kupanua utumishi wako utumike kama painia au utumike mahali penye uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme. Huenda wengine wanafikiria kujitolea kwa ajili ya kazi ya ujenzi wa kimataifa, kutumikia katika ofisi ya tawi, au katika utumishi wa umishonari. Hiyo ni miradi yenye kuridhisha na inayostahili sifa!
2 Jambo linaloweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kiroho ni kuiandika. Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2004, lilisema hivi: “Yale unayofikiria yanakuwa wazi unapochagua maneno ili kuyaeleza. Kwa hiyo, huenda ukataka kuandika miradi [yako] na mbinu za kuifikia.” Isitoshe, kuwa na mradi wa muda mfupi kunaweza kukusaidia kupima maendeleo yako na kukaza uangalifu unapofuatia mradi wa muda mrefu.
3 Miradi ya Muda Mfupi: Ikiwa bado hujabatizwa, fikiria unachohitaji kufanya ili kufikia mradi huo. Huenda ukahitaji kuelewa vizuri zaidi mafundisho ya msingi ya Biblia. Ikiwa ndivyo, weka mradi wa kujifunza kabisa kitabu Biblia Inafundisha, ukichunguza maandiko yote yaliyotajwa bila kunukuliwa. (1 Tim. 4:15) Jiwekee mradi wa kusoma Biblia yote kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo, ambalo ni takwa kwa Wanabetheli na wanafunzi wa Gileadi. Baada ya hapo, dumisha programu ya kusoma Biblia kila siku. (Zab. 1:2, 3) Hebu wazia jinsi hilo litakavyokusaidia kukomaa kiroho! Kila mara unaposoma Biblia na kujifunza anza na umalizie kwa kusali kutoka moyoni, na sikuzote ujitahidi kutumia unayojifunza.—Yak. 1:25.
4 Ikiwa tayari umebatizwa, unaweza kufuatia miradi gani mingine? Je, unahitaji kuboresha ustadi wako wa kuhubiri? Kwa mfano, je, unaweza kuwa na lengo la kuwa na ustadi zaidi wa kutumia Neno la Mungu katika huduma ya shambani? (2 Tim. 2:15) Unaweza kupanuaje utumishi wako? Jiwekee miradi hususa ya muda mfupi inayopatana na umri wako na hali zako na ambayo itakusaidia kufikia miradi yako ya muda mrefu.
5 Alifaulu: Alipokuwa na umri wa miaka 19, Tony alitembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova na hilo likaamsha tamaa yake ya kutumikia Betheli. Hata hivyo, alikuwa akiishi maisha yaliyopotoka na hakuwa amejiweka wakfu kwa Mungu. Tony aliamua kupatanisha maisha yake na njia za Yehova na kuweka mradi wa kustahili kubatizwa. Baada ya kutimiza mradi huo, alijiwekea mradi wa kuwa painia msaidizi na baadaye painia wa kawaida, naye akaandika katika kalenda tarehe aliyopanga kuanza upainia. Hebu wazia shangwe aliyopata alipoalikwa atumikie Betheli baada ya kufanya upainia kwa muda fulani!
6 Wewe pia unaweza kufikia miradi yako ya kiroho ikiwa utatanguliza mambo ya Ufalme. Weka “kazi zako” mbele ya Yehova kupitia sala na ujitahidi kwa bidii kuzifikia.—Met. 16:3; 21:5.
[Maswali ya Funzo]
1. Ni miradi gani ya kiroho ambayo vijana wengi Wakristo hujiwekea?
2. Ni nini kinachoweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kiroho?
3. Taja miradi fulani ya muda mfupi ambayo inaweza kumsaidia mtu astahili kubatizwa.
4. Mkristo aliye na mradi wa muda mrefu wa kutumika Betheli au kuwa mmishonari anaweza kujiwekea miradi gani ya muda mfupi?
5. Kujiwekea miradi ya muda mfupi kulimsaidiaje ndugu mmoja kufikia mradi wake wa kutumikia Betheli?
6. Ni nini kinachoweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kiroho?