Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 6/92 uku. 3
  • Sanduku La Swali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sanduku La Swali
  • Huduma Yetu ya Ufalme—1992
Huduma Yetu ya Ufalme—1992
km 6/92 uku. 3

Sanduku La Swali

◼ Je! Mkristo anaweza kutumia kwa kufaa neno la kuamkua kusema, “Shikamoo”?

Katika sehemu fulani za eneo letu neno “Shikamoo” ni salamu au neno la kuamkua lililo la kawaida linalotumiwa leo hasa na vijana wanapowaamkua walio wazee-wazee. Neno hilo pia limetumiwa na wale wanaotegemea wengine wanapowaamkua wakuu wao. Kulingana na kamusi, neno hilo kwa ukamili ni “nashika miguu yako,” na utumizi walo wa kidesturi zamani na hata sasa ni wa kuonyesha heshima, staha, au cheo cha chini na unyenyekevu kuelekea mtu mwenye umri mkubwa zaidi au mtu wa cheo cha juu au mwenye madaraka maishani. Kwa hiyo, ingeonekana kwamba katika sehemu ambako hiyo ni salamu ya kidesturi, Mkristo havunji kanuni zozote za Kimaandiko ikiwa dhamiri yake inamruhusu kutumia salamu kama hiyo kwa kuwaheshimu walio wazee-wazee na wengineo. Bila shaka, hakuna mtu ambaye angepaswa kumpa imla mtu mwingine kuhusu yale yapaswayo kufanywa. Hakuna mtu anayepaswa kuwekea mwingine kanuni za maadili za kufuatwa. Hilo ni jambo la kibinafsi.—Linganisha 1 Kor. 10:29; 2 Kor. 1:24; Rum. 14:4, 5.

Hata ingeonekana kwamba utumizi wa salamu kama hiyo katika kundi la Kikristo kuelekea waabudu wenzi walio wazee-wazee na wengineo ni jambo la kuamuliwa na dhamiri. Bila shaka, hakuna mtu aliye mzee-mzee kimwili au mzee kiroho wa kundi ambaye angedai apewe kipekee salamu ya aina hiyo. Yale tunayopaswa kushika katika kundi la Kikristo leo ni “sheria ya Kristo” na si sheria za kimapokeo au za kidesturi. (Gal. 6:2) Hakuna mtu ambaye angetaka kujaribu kushurutisha utumizi wa mapokeo yasiyo ya Kikristo, ya kikabila au ya kilimwengu katika kundi la Kikristo. Hata hivyo, wakati mapokeo au desturi hazipingani na kanuni za Kimaandiko, basi ni jambo la kutumia dhamiri. (Linganisha kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, sura 16, mafu. 1-3.) Kuhusiana na salamu na namna ya kuamkua, Mkristo hukumbuka maneno ya Yesu kwamba “nanyi nyote ni ndugu” na bila shaka yeye hupendelea kuwasalimu waabudu wenzake kwa maneno “ndugu” au “dada” kulingana na zoea lililoimarika la udugu wa ulimwenguni pote. (Mt. 23:8) Kwa hiyo, linaonekana pia kuwa jambo la akili nzuri kujaribu kuepuka zoea la kuwaita ndugu waliowekwa kutumika kundini kwa majina ya vyeo ya kiheshima, kama vile, “mzee” na “mwangalizi.”

Kwa kuwa neno hilo [shikamoo] larejezea kutoa heshima ya unyenyekevu na kutoa sifa na staha au kumwona mtu kuwa mstahifu, limetumiwa kwa njia ya kumtolea Yehova sifa iliyotukuka zaidi na heshima katika kitabu Upeo wa Ufunuo! kwenye kurasa 81 fungu la 25, na 173 fungu la 7. Hata hivyo, utumizi wa neno “Shikamoo” kuhusiana na Yehova katika muktadha huu haumaanishi neno hilo lazima litumiwe kwa Yehova peke yake.

Kupatana na yaliyo juu na kwa sababu asili ya neno hilo siyo jambo linaloamua, neno “Shikamoo” katika utumizi walo wa kawaida na wa kila siku, laweza kutumiwa likiwa salamu ya kawaida tu au namna ya kuamkua.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki