Sanduku La Swali
◼ Mwangalizi wa utumishi anaweza kusimamiaje kazi ya watumishi wa huduma wanaoshughulikia idara za vitabu na magazeti?
Mambo ambayo mwangalizi wa utumishi anapendezwa nayo si kuzuru vikundi vya mafunzo ya vitabu tu mara moja kwa mwezi na kupanga mikutano ya kawaida ya utumishi wa shambani. Mzee huyo mwenye bidii anapendezwa sana na kila jambo linaloweza kuathiri maendeleo ya kazi ya kuhubiri katika eneo lililogawiwa kundi.
Yeye atahakikisha kwamba kila mwezi ugavi wa kutosha wa vitabu na magazeti ya kampeni unapatikana kwa urahisi na kwamba umo katika hali nzuri. Kwa kusudi hilo yeye husimamia madaraka mengi ya watumishi wa huduma waliogawiwa kushughulikia idara za vitabu na magazeti.
Mwangalizi wa utumishi hutoa uangalifu hususa kwa matangazo ya vitabu vya kampeni vinavyotarajiwa wakati hivyo vinapotangazwa katika Huduma ya Ufalme Yetu. Yeye na ndugu anayetunza vitabu hufanya kazi pamoja ili kuhakikisha kwamba kiasi cha kutosha cha vitabu kitapatikana ili kitumiwe, lakini ni lazima wawe waangalifu wasiagize vingi kupita kiasi. Ikiwa kichapo fulani kitatumiwa shambani kwa mara ya kwanza au ikiwa kitasomwa hivi karibuni kundini, mambo hayo yapaswa kufikiriwa wakati agizo linapopelekwa kwa Sosaiti. Ikiwa kitabu hicho kimepata kutolewa hapo mbeleni, ripoti ya kundi ya utumishi wa shambani ya kampeni iliyopita itaonyesha kama ugavi ulio kundini unatosha. Bila shaka, ufikirio wapaswa utolewe kuhusu mambo kama vile idadi ya wahubiri watakaotumika wakiwa mapainia wasaidizi mwezi huo pamoja na ongezeko katika idadi ya wahubiri na mapainia wa kawaida tangu wakati uliopita ambapo kitabu hicho kilitolewa. Vitabu vyapaswa vipatikane kabla na pia baada ya mikutano ya kundi. Katoni za vitabu zapaswa ziwekwe vizuri katika mahali safi, pakavu na kupangwa ili kuzuia zisiharibike kwa vyovyote.
Pia, mwangalizi wa utumishi atashirikiana na ndugu anayetunza idara ya magazeti. Mara kwa mara, mwangalizi wa utumishi na ndugu anayeshughulikia magazeti wapaswa kulinganisha idadi ya magazeti yanayoagizwa kila mwezi na ile ya magazeti yanayoangushwa kihalisi katika huduma. Inaweza kuwa kwamba baadhi ya wahubiri wapaswa kupunguza kiasi cha magazeti walichoagiza ikiwa yanarundamana kwa kawaida nyumbani mwao. Magazeti hayapaswi kutumiwa ovyo.
Akiwa na kanuni hizohizo akilini, mwangalizi wa utumishi anapaswa akague kibinafsi kiasi cha vitabu vya kampeni ambacho kundi linaagiza kwenye Fomu ya Agizo la Vitabu (S-14-SW). Halafu yeye atampa mwandishi wa kundi fomu hiyo, naye atachunguza kwa uangalifu sehemu zilizobaki za fomu hiyo, akitoa uangalifu hususa kwa idadi ya vifaa vinavyoagizwa kipekee vilivyoorodheshwa.
Bila shaka, kiasi fulani cha kazi ya kuweka kumbukumbu mbalimbali kinahitajiwa ili kutunza idara za vitabu na magazeti inavyofaa. Ikiwa ndugu waliogawiwa wana maswali kuhusiana na jinsi ya kutumia fomu na kuweka rekodi, mwandishi atafurahi kuwasaidia katika sehemu hiyo ya kazi yao.