Je! Wewe Unaweza Kuufanya?
1 ‘Kufanya nini?’ unauliza. Mithali 3:27 hujibu: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Je! iko “katika uwezo wa mkono wako” kuongeza utendaji wako na kushiriki katika upainia msaidizi au utumishi wa painia wa kawaida? Je! unaweza kufanya hivyo?
2 Ilitia moyo kama nini kusoma katika Kitabu-Mwaka cha 1993 (Kiingereza) kwamba kulikuwa na wastani wa mapainia wa kawaida na wasaidizi 3,504 katika Afrika Mashariki, uwiano wa painia 1 kwa wahubiri 5. Ndiyo, 652 waliingia utumishi wa painia mwaka uliopita. Hilo lafikia karibu wahubiri 2 kwa siku ambao walichunguza hali zao na kutambua kwamba wangeweza kufanya mengi zaidi katika huduma.
3 Kufanya upainia msaidizi ni sehemu nyingine ya kufanyia wengine mema. Mwaka uliopita kulikuwa na kilele cha mapainia wasaidizi 3,430. Hilo ni jambo jema sana. Wahubiri wengi wanatafuta njia za kufanya upainia msaidizi mara nyingi mwakani.
4 Ili kujua kama ‘unaweza kuufanya’ au sivyo, kwanza unahitaji kufikiria tamaa yako ya moyoni. (Mt. 22:37-39) Matendo 20:35 husema: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” Bila shaka, wale ambao hutoa msaada wa kiroho kwa ukarimu kutoka moyoni wana tamaa ifaayo. Ili kuwa mhubiri au painia mwenye mafanikio, tamaa hiyo ni ya lazima.
5 La pili, fikiria hali zako za sasa. Je! unaweza kufanya marekebisho katika mambo yako ya kila siku ili utumikie kwa wakati wote? Si kila mtu anayeweza. Lakini baada ya kujichunguza kwa sala, kila mwaka maelfu hupata njia ya ‘kuufanya.’ (Kol. 4:5; w77-E uku. 701) Kwa mfano, familia fulani huchagua miezi mahsusi kwa baadhi ya washiriki au washiriki wote wa familia kufanya upainia msaidizi. Familia nyingine hudhamini mmoja wa washiriki wao awe painia wa kawaida. Je! familia yenu imefikiria mambo hayo?—Ona Mithali 11:25.
6 Kusaidia wengine waijue kweli ndiko kunakoleta uradhi wa kweli, iwe unatumikia ukiwa mhubiri au painia. Tunajua kwamba shangwe ya kweli hutokana na kuwafanyia wengine mema, hasa ‘ikiwa katika uwezo wa mkono wetu kuyatenda.’