Je! Wewe Husababu kwa Kutumia Maandiko?
1 Askari-jeshi mwenye ujuzi anayeenda vitani atajihami kabisa kwa silaha na kujikinga. Msanii stadi anayejitayarisha kufanya kazi kwenye mradi mkubwa wa ujenzi atachukua vyombo anavyohitaji ili kukamilisha kazi hiyo. Mtumishi wa Yehova anayefanya kazi katika huduma ya shambani atakuwa na “upanga” wake mkononi na atautumia kwa ustadi kila mara apatapo fursa. (Efe. 6:17) Je! wewe binafsi hufanya hivyo? Ushirikipo katika utumishi, je, wewe huacha Neno la Mungu liseme ili roho takatifu iweze kugusa mioyo ya wasikilizaji wako?—Mit. 8:1, 6.
2 Kuhubiri si kazi rahisi sikuzote. Katika maeneo fulani mara nyingi watu hawako nyumbani, na mara nyingi wale wanaofungua mlango huwa wana shughuli, ikifanya kuwe na fursa ndogo ya mazungumzo marefu ya Biblia. Kwa kuwa Biblia ndicho kitabu chetu kikuu cha mafundisho, twaweza kuitumiaje zaidi katika utumishi na kuruhusu ujumbe wayo uliopuliziwa uwe na uvutano juu ya wasikilizaji wetu?
3 Kwenye Kila Fursa: Kwenye kila mlango, tungependa kutumia Biblia ili kumchochea mwenye nyumba. Ni lazima tuwe tayari kufanya hivyo haidhuru ni kichapo kipi kitolewacho. Ikiwa mtu huyo ana shughuli na hakuna wakati wa kutosha kufungua Biblia na kusoma mstari mmoja au miwili, je, waweza kunukuu au kueleza andiko kabla ya kutoa fasihi? Hilo peke yalo laweza kumfanya mtu huyo atue na kusikiliza. Kwa njia hiyo waacha Neno la Mungu liseme.—Ebr. 4:12.
4 Kwenye Ziara za Kurudia: Twapaswa kujitayarisha kabla ya kufanya ziara za kurudia. Hata hivyo, mara nyingi habari ambazo hatujatayarisha kuzungumzia zitazuka. Huo ndio wakati kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko chaweza kuthibitika kuwa chombo chenye thamani. Tukinukuu au kusoma maandiko yanayotegemeza kutoka katika kitabu Kutoa Sababu hilo litasaidia watu waone kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu na si wachuuzi wa lile Neno.—2 Kor. 2:17.
5 Turudipo mahali ambapo hakuna habari hususa iliyokuwa imezungumziwa, huenda ukafungua tu kitabu Kutoa Sababu kwenye kichwa kifaacho, kama vile “Yesu Kristo,” “Siku za Mwisho,” au “Ufufuo,” na utumie mojawapo vichwa vidogo ili kuanzisha mazungumzo. Wenye nyumba waweza kualikwa kusoma baadhi ya maandiko kutoka kwenye Biblia yao wenyewe. Kwa njia hiyo Biblia itawapendeza na kuwa yenye maana kwao, na roho takatifu ya Yehova itatiririka ikiwa wana mwelekeo wa kufuatia uadilifu.
6 Daraka letu la kuhubiri habari njema na kuonya waovu ni zito. Huo ni ujumbe wa Yehova, si wetu. Acha Neno lake, ule upanga wa roho, likusaidie wewe.