Je! Wewe Waweza Kuongeza Sifa Yako kwa Yehova Wakati wa Aprili?
1 Mtunga-zaburi Daudi alikuwa na tamaa ya moyoni ya kumsifu Yehova kwa njia ya kukubalika, kwa hiyo alitangaza: “Nitamshukuru BWANA kwa kinywa changu, naam, nitamsifu katikati ya mkutano.” (Zab. 109:30) Aprili ni wakati ufaao wa ‘kuzidi kuongeza sifa zake zote’ kwa kuongeza ushiriki wetu katika huduma ya shambani. (Zab. 71:14) Je! unapanga kuwa miongoni mwa wale ambao hufanya hivyo kwa kuchukua upainia-msaidizi?
2 Panga Sasa: “Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu,” twakumbushwa hivyo kwenye Mithali 21:5. Hili lahitaji umwambie Yehova jambo hilo kwa sala, ukimweka kwanza katika mipango yako. (Mit. 3:5, 6) Kisha, changanua ratiba yako ya karibuni ili ujue ni wapi marekebisho yanaweza kufanywa ili utumie wastani wa saa mbili kwa siku katika huduma. ‘Kukomboa kwako wakati’ kutoka utendaji mwingine kwaruhusu utumie wakati wa ziada kwa kazi ya kuhubiri.—Efe. 5:16.
3 Wasiliana na Ushirikiane: Mtume Paulo alizungumza juu ya watu fulani ambao walikuwa ‘faraja kwake’ katika kutimiza huduma yake. (Kol. 4:11) Zungumzia mipango yako na wengine wanaotaka kujiandikisha wawe mapainia-wasaidizi katika Aprili. Utegemeo wao na uenzi wao waweza kuleta faida za pamoja za kiroho. Mwangalizi wa utumishi anaweza kukusaidia ukiwa na maswali juu ya mipango ya utumishi au eneo la kufanyia kazi.
4 Ushirikiano na utegemezo kutoka kwa familia waweza kusaidia washiriki mmoja-mmoja kufanya upainia msaidizi. Huenda kazi za nyumbani zikahitaji kugawanywa upya kwa muda. Ratiba za kushughulika na kazi hizo huenda pia zikahitaji kurekebishwa. Mazungumzo ya familia juu ya mahitaji haya yanaweza kusaidia katika kutimiza mradi wako. Mawasiliano na ushirikiano mzuri ndio ufunguo wa kufanikiwa.
5 Uwe na Mwelekeo Ufaao: Usiwe mwepesi kuondoa uwezekano wa kufanya upainia msaidizi kwa sababu ya hali zisizopendeza. Vijana walio shuleni, watu waliostaafu, wake-nyumbani walio na watoto, vichwa vya familia wanaofanya kazi wakati wote, wote hao wameweza kujidhabihu—na kwa furaha—kufanya upainia msaidizi katika Aprili. Wao wanakubaliana na mtunga-zaburi kwamba “kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo,” nao hawaoni kuwa jambo gumu sana kuweka jitihada ya ziada inayohitajika ili kutumia muda wa saa 60 katika huduma. (Zab. 33:1) Ikiwa huwezi kujiandikisha, kwa nini usishiriki katika shangwe hiyo kwa kuongeza utendaji wako ukiwa mhubiri wa kutaniko?
6 Kwa walio wengi, upainia msaidizi wakati wa Aprili ni mwanzo wa hatua ya utumishi wa painia wa kawaida. Wakiwa wameongeza utendaji wao, walipata kwamba badiliko la kufanya kazi ya painia wa kawaida ilikuwa rahisi zaidi.
7 Naam, majira yenyewe yanafanya iwe rahisi kwa utendaji wa kitheokrasi ulioongezeka katika Aprili. Twataka kufanya yote tuwezayo ili kusifu Mungu wetu, Yehova. Kufanya upainia msaidizi katika Aprili ni njia nzuri ya kuonyesha uthamini wetu kwa matendo yake mengi ya fadhili zisizostahiliwa kwetu.