Tayarisha Wanafunzi wa Biblia Kwa Ajili ya Huduma
1 Mradi wa mwisho katika kuongoza mafunzo ya Biblia ni kufanya wanafunzi wapya, wafanyakazi watakaojiunga nasi kufundisha wengine. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo kusudi la funzo si kuwapa watu ujuzi tu; lapasa kuwa kukaza kikiki imani yenye kuhisiwa moyoni katika wanafunzi wetu na kuwatayarisha kushiriki tumaini lao pamoja na wengine. (2 Kor. 4:13) Ni kwa njia gani zenye kutumika twaweza kuwasaidia wastahili zaidi kufundisha wengine?—2 Tim. 2:2.
2 Weka Huduma Iwe Mradi: Tangu pale mwanzo, elewesha wazi kwamba ibada ya kweli huhusisha “tangazo la peupe kwa ajili ya wokovu.” (Rum. 10:10, NW) Lile jina letu lenyewe, Mashahidi wa Yehova, hudokeza kwamba ni lazima tuseme na wengine. Wasaidie waone kwamba kufundishwa kwao si kwa ajili ya wokovu wao wenyewe tu. Wao wenyewe wawapo walimu, wale wawasikilizao hupata pia fursa ya kupata wokovu.—1 Tim. 4:16.
3 Pitia Yaliyofunzwa: Mapitio ya pindi kwa pindi juu ya yale ambayo yamefunzwa ni msaada wa kufundisha ulio na thamani. Mapitio hayo husaidia mwanafunzi akue kiroho kwa kadiri kweli mpya alizofunzwa zikazikapo ndani ya akili na moyo wake. Sisi wenyewe tumejionea hilo wakati wa kujibu yale maswali ya kupitia yanayotiwa ndani ya Funzo la Mnara wa Mlinzi. Tayarisha maswali sahili, ya moja kwa moja ili mwanafunzi wako ayajibu kwa maneno yake mwenyewe.
4 Pitio lako lingeweza kuwa la namna ya kikao cha utumishi wa shambani. Tokeza swali au ueleze hali ambayo hukabiliwa kwa kawaida wakati wa kutolea wengine ushahidi. Huku wewe ukitenda kama mwenye nyumba, acha mwanafunzi wako aonyeshe yale ambayo yeye angesema. Mpongeze kwa yale aliyofanya vema, na utoe madokezo yenye kutumika yatakayomsaidia awe na matokeo hata zaidi wakati ule mwingine. Mazoezi hayo yatamfundisha jinsi ya kutumia mambo ambayo amejifunza na yatakuza ufundi wake wa kutumia Biblia.
5 Kitabu Kutoa Sababu: Hakikisha kwamba mwanafunzi wako ana nakala ya kitabu Kutoa Sababu, na umzoeze kukitumia. Onyesha jinsi kiandaavyo madokezo juu ya kuanzisha mazungumzo, kujibu maswali ya Biblia, au kushughulika na vipingamizi. Tumia kitabu hicho katika funzo kuonyesha njia za kuongea na wengine kwa njia yenye kusadikisha. Kitabu hicho chaweza kujenga uhakika wake, kuongezea uwezo wake wa kuchukua hatua ya kwanza ya kutangaza ujumbe wa Ufalme.
6 Kazia Umaana wa Mikutano: Mikutano ya kutaniko, hasa Mkutano wa Utumishi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, imepangwa kwa njia ya kututayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani. Mambo yote ya msingi ya kutoa ushahidi wenye matokeo hupitiwa na kufanyiwa maonyesho na wale walio na ujuzi na ufundi. Kazia umaana wa mikutano, na ufanye kadiri uwezavyo kumsaidia kuhudhuria. Hudhurio la kawaida laweza kuandalia mwanafunzi wako kichocheo ahitajicho ili awe mwanafunzi wa kweli wa Yesu.
7 Jambo lisilo la kusahauliwa ni kielelezo chako binafsi. Hiari yako na ukawaida katika kazi ya kuhubiri yaonyesha uthamini wako wa kina kirefu kwa ajili ya ile kweli. Mwendo wa jinsi hiyo humtia moyo mwanafunzi wako afanye mengi zaidi kuonyesha imani yake. (Lk. 6:40) Yote hayo yaweza kusaidia mtu mpya aione huduma kuwa pendeleo na ashukuru kuishiriki kwa kadiri fulani.—1 Tim. 1:12.