Je! Utashiriki Katika Ushahidi wa Kivivihivi?
1 Kawaida yetu maishani hutia ndani vipindi hususa vya kuongea na watu juu ya Yehova. Sisi huweka kando wakati wa kutoa ushahidi rasmi nyumba kwa nyumba, tukifanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia. Ingawa hivyo, huwa kuna pindi nyingine zisizo rasmi hivyo tuwezapo kusema na watu juu ya kweli. Sisi hurejezea kuhubiri huko kuwa kutoa ushahidi wa kivivihivi.
2 Wahubiri fulani hupata fursa nyingi za kujitia katika namna hii ya huduma. Sote twaweza kujitahidi kuwa macho kuona pindi hizo tusafiripo kwenda na kurudi kutoka mikusanyikoni, tuchukuapo malikizo, na kuwazuru watu wa ukoo. Je! utatumia kwa faida fursa za kutoa ushahidi wa kivivihivi katika wakati huu?
3 Fanya Mipango ya Mapema: Kujitayarisha na kufikiri mapema kutatuwezesha kutoa ushahidi wa kivivihivi kwa njia yenye matokeo. Kwa habari hii, tuna vifaa vya kutosha vya unamnanamna wa vichapo ili kutusaidia kutimiza hili. Zaidi ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, tuna trakti kadhaa zenye vichwa vya kuchochea fikira ili kuamsha kupendezwa. Kuna broshua zivutiazo watu wa malezi na dini mbalimbali. Pia tuna vitabu vya ukubwa wa mfukoni ambavyo huzungumzia habari karibuni zenye kupendeza. Ni vichapo vipi ambavyo wewe wahisi ukistareheka kuvitumia? Fikirieni hilo mkiwa familia. Halafu mjizoeze mtakalosema pindi ifaayo itokeapo.
4 Jinsi ya Kuanza: Ikiwa tuna miadi ya kufika mahali fulani na twajua tutalazimika kutumia wakati fulani tukingoja, tungeweza kwenda tukiwa na magazeti ya karibuni zaidi na kuwa tayari kuzungumzia makala ya upendezi pamoja na mtu tukutaye. Au tungeweza kutumia trakti au broshua kama msingi wa kuanzia mazungumzo. Katika kikao cha jinsi hiyo, watu fulani wameona kuna matokeo kuanza mazungumzo ya kutoa taarifa ya kuvuta maongezi kwa msingi wa tukio la karibuni halafu kuomba maoni ya mtu huyo. Wengine wameona kwamba kuuliza swali lenye kuchochea fikira kuhusu tukio fulani la hivi karibuni kwaweza kuongoza ndani ya ushahidi mzuri. Katika visa vyote, kuchukua hatua ya kwanza ndiko kwahitajiwa ili kutendesha mambo.
5 Wakati wowote tujitiapo katika ushahidi wa kivivihivi, ni vema kuruhusu mtu yule mwingine fursa ya kujieleza. Twapaswa kuwa wenye uungwana na staha nyakati zote. Tukisikiliza kwa uangalifu yale mtu yule mwingine asemayo, huenda tukaweza kujua mapendezi yake ni nini kisha tuseme maneno yatakayoamsha hamu yake ya kiroho. (Mit. 25:11) Ikiwezekana, twapaswa kupata majina na anwani za wale waonyeshao kupendezwa ili waweze kuonwa zaidi kusitawisha upendezi. Kwa kielelezo, kuhusiana na ile mikusanyiko ya kimataifa katika Nairobi, ofisi imepokea maombi mengi ipeleke fasihi na kutembelea watu katika sehemu zote za Kenya waliopokea ujumbe wa kivivihivi kutoka kwa wajumbe wetu wenye kuzuru. Vilevile, twapaswa pia kuweka kumbukumbu la wakati uliotumiwa katika ushahidi wa kivivihivi ili uweze kuripotiwa kwa usahihi.
6 Tusiachilie kamwe fursa tulizo nazo za kutoa ushahidi wa kivivihivi. Njia hii ya kuhubiri ni yenye kuzaa matunda, na watumishi wa Yehova wapaswa kuishiriki. Kama vile ilivyokuwa kwa Yesu, upendo wetu kwa wanadamu wenzetu na utusukume kusema katika kila pindi ifaayo!—Mt. 5:14-16.