Fuatia Vichapo Vyote Ulivyoangusha
1 Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wajitahidi kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19) Hilo lamaanisha mengi zaidi ya kuangusha fasihi tu; twataka kuwasaidia watu wafanye maendeleo kiroho. Ili kufanya hivyo ni lazima turudi ili kuandaa msaada wa ziada kwa wale waonyeshao kupendezwa.
2 Ikiwa ulionyesha makala fulani katika mojapo magazeti wakati wa ziara yako ya kwanza, ingefaa kuzungumzia habari iyo hiyo unaporudi:
◼ “Nilipozuru wakati uliopita, nilielekeza uangalifu wako kwenye makala fulani katika Mnara wa Mlinzi (au Amkeni!) iliyotusaidia tuthamini uhitaji wa kuichunguza Biblia. Kusudi la Mungu la wakati ujao ulio bora zaidi kwa wanadamu hutegemea serikali yake ya Ufalme. Mika 4:3, 4 larekodi ahadi yake kwamba Ufalme huo utakomesha vita vyote.” Baada ya kusoma andiko hilo, toa broshua “Tazama!”, na uonyeshe picha ya jalada. Zungumzia fungu la kwanza na maandiko yaliyotajwa katika fungu hilo, ukionyesha kwamba Mika 4:3, 4 ni moja kati yayo. Panga kufanya ziara ya kurudia ili kuendelea na mazungumzo katika fungu la 2.
3 Ikiwa mwenye nyumba hana uwezo bado wa kuandikisha magazeti, waweza kuamua kuongeza jina lake tu kwenye orodha ya wale unaowapelekea magazeti kwa kawaida:
◼ “Kwa kuwa ulionyesha kupendezwa na magazeti niliyokuachia wakati uliopita, nilifikiri kwamba ungefurahia matoleo ya karibuni. Nasadiki utapata makala hii kuwa yenye kupendeza hasa.” Onyesha makala fulani ambayo wahisi ingemvutia. Jitolee kurudi ukiwa na matoleo yanayofuata.
4 Ikiwa uliacha trakti kwenye ziara ya kwanza, waweza ama kueleza juu ya trakti yenyewe ama kufuatia trakti hiyo uliyoangusha kwa kurejezea jambo linalofaa katika gazeti la karibuni au broshua.
Kwa kielelezo, ikiwa uliangusha “Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani,” sema tu:
◼ “Nilipokutembelea wakati uliopita, tulisema juu ya ahadi ya Mungu ya ulimwengu bora zaidi. Kama vile tulivyozungumza, hali bora zaidi zitakuja kupitia Ufalme wa Mungu. Je! wewe wafikiri ni nini kinachotakwa kwetu ili tuwe sehemu ya ulimwengu huo wenye amani?” Mruhusu mwenye nyumba atoe elezo, kisha endelea na lile wazo kwenye Zaburi 37:9, 11, 29.
5 Ikiwa uliangusha broshua lakini hukuwa na nafasi ya kuonyesha mpango wa funzo, panga kufanya hivyo katika ziara ya kurudia.
Kwa kielelezo, ikiwa uliacha broshua “Serikali,” mwombe mwenye nyumba alete nakala yake, na useme:
◼ “Angalia yale ambayo ukurasa wa 3 watuambia juu ya kichwa cha ujumbe ambao Yesu alihubiri alipokuwa duniani.” Kisha zungumzia kwa ufupi habari iliyo kwenye ukurasa wa 3. Muulize mwenye nyumba ni nini anachofikiri ahitaji kufanya ili kujifunza zaidi. Kisha useme: “Ni muhimu tuthamini ni kwa nini twahitaji sana Ufalme wa Mungu. Ningependa kurudi na kuzungumzia sababu inayotupasa tutazamie serikali ya Mungu kuwa tumaini letu pekee.”
6 Tuna broshua na habari mbalimbali katika magazeti yetu. Tafuta mambo ya kupendeza katika ile unayopanga kutumia. Hilo litakusaidia uwatie moyo wale wenye moyo mweupe wajifunze zaidi juu ya mambo ambayo Yesu aliamuru.—Mt. 28:20.